Friday, March 16, 2012

TANZANIA YABORESHA HUDUMA ZA MAJI

Na.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikiboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ukiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji na kuboresha upatikanaji wa huduma za maji safi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji.

Akiongea wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji kitaifa mkoani Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, aliyemuwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika amesema kuwa “Serikali kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini -MKUKUTA, na mabadiliko mbalimbali ya kisera na kimfumo, imekuwa ikitekeleza mipango mbalimbali ya kuboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ikiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji, kuboresha upatikanaji wa huduma za majisafi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji”.

Amesema kuwa kwa sasa Serikaili inatekeleza mpango wa pamoja wa matumizi ya rasilimali za maji kupitia ofisi zote tisa za mabonde nchini. Amesema pindi mpango huo utakapokamilika utaainisha njia za matumizi bora ya rasilimali maji.

Amesema “katika kuhakikisha rasilimali ya maji inatumika kwa manufaa ya taifa na usalama wa chakula nchini unakuwepo, ninawaomba viongozi wenzangu, vyombo vinavyosimamia rasilimali maji kama vile Mamlaka za Maji, Ofisi za Maji za Mabonde, Vyombo vya Watumiaji Maji na wananchi kwa ujumla kujiandaa kuzikabili changamoto na vihatarishi nilivyotaja”.

Ameitaka jamii kushirikiana katika kuhifadhi, kutunza na kuendeleza mfumo mzima wa maji kuanzia kwenye vyanzo, uzalishaji na ugawaji kwa kuzingatia ongezeko la matumizi ya maji.

Mkoa wa Iringa ni mwenyeji wa maadhimisho ya 24 ya wiki ya maji kitaifa yanayoongozwa na kauli mbiu isemayo ‘maji kwa usalama wa chakula’, shughuli mbalimbali za sekta ya maji pamoja na maonesho zitafanyika katika uwanja wa Samora na maeneo mengine.
=30=

MAAFISA KILIMO WATAKIWA KUFANYA MABADILIKO

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika amewataka maafisa kilimo na wadau wa sekta hiyo kufanya mabadiliko makubwa katika kukuza sekta hiyo ili iwe ya kisasa na kuifanya iwanufaishe wananchi wengi zaidi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Prof. Jumanne Maghembe, wakati akifungua mkutano wa maafisa kilimo wa Tanzania bara, uliofanyika katika hoteli ya royal village, katika Manispaa ya Dodoma.

Prof. Maghembe amesema kuwa asilimia 77.5 ya wananchi wanaokadiriwa kufika mil. 40 wanategemea sekta ya kilimo katika kuendeleza maisha yao na kati yao asilimia 22.5 ndiyo wanaofanya kazi katika sekta hiyo.

Amesema pamoja na ukubwa wa asilimia ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo  bado kilimo kinachangia asilimia 34 tu ya fedha za kigeni nchini. Katika mchango wa kilimo katika pato la taifa, kinachangia asilimia 24 pekee. Amesema “bado kazi inatakiwa kufanywa na sisi tuliomo humu ndani, tumeandaliwa vizuri kitaaluma ili tuweze kutekeleza hili, kushindwa tunaliangusha taifa”.    

Prof. Maghembe amesema kuwa kilimo nchini kinakua kwa asilimia 4.2 tofauti na lengo la kitaifa la kilimo kukua kwa angalau asilimia 6 kwa mwaka.

Pamoja na kuhimiza kilimo cha umwagiliaji, Waziri wa kilimo, Chakula na Ushirika amesema “suala si kuongeza maeneo ya kulima, bali ni kuongeza uzalishaji katika maeneo tunayolima”.

Akiongelea vikwazo vinavyoikabili sekta ya kilimo, amesema kuwa masoko yasiyo ya uhakika dunia na kuwataka wadau hao kujipanga katika kukuza kilimo ili kiweze kuzinufaisha nchi zenye upungufu wa chakula na kuzifanya zisifikirie kununua chakula sehemu nyingine zaidi ya Tanzania.

Akichangia katika mkutano huo huku akisikilizwa kwa umakini mkubwa na mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa nchi haiwezi kuwa na mafanikio katika sekta ya kilimo bila kuendeleza kilimo cha umwagiliaji. Amesema ni vema juhudi zikawekwa katika kufufua kilimo cha umwagiliani pamoja na kuimarisha skimu za umwagiliaji ili kilimo kiweze kushamiri.

Akichangia katika upatikanaji wa soko, Dk. Ishengoma amesema kuwa soko ni changamoto kuwa kwa kufanikisha shughuli za kilimo. Amesema ukitangaza uhakika wa soko la mazao mapema wakulima watalima kwa nguvu kwa sababu watakuwa na uhakika na soko. Akitolea mfano katika mkoa wake wa Iringa, amesema kuwa mkoa huo umehimiza kilimo cha zao la mtama kwa wingi ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa chakula, muitikio umekuwa mzuri baada ya kuwa na uhakika wa soko.

Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni upungufu wa fedha za ufuatiliaji, hatua inayowakwamisha wataalamu wa kilimo katika kutekeleza majukumu yao katika sekta ya kilimo.
=30=

Thursday, March 15, 2012

WIKI YA MAJI IRINGA


Mkoa wa Iringa umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho  ya 24 ya wiki ya Maji kitaifa yatakayofanyika kuanzia tarehe 16 hadi 22 Machi, 2012.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) leo, amesema kuwa uzinduzi na kilele cha maadhimisho vitafanyika katika uwanja wa Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa.
Amesema kuwa maadhimisho yaho yanaongozwa na kaulimbiu isemayo ‘maji kwa usalama wa chakula’ yanalenga kuwaelimisha wananchi kuhusu Sera ya Maji na majukumu ya wananchi katika kuitekeleza sera hiyo. Amesema madhumuni mengine ni kutathmini maendeleo ya utekelezaji waprogramu ya maji, hali ya huduma ya maji na usafi wa mazingira na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma na uhifadhi wa rasilimali za maji.
Dk. Christine amesema kuwa maadhimisho hayo pia yanalenga kutoa ujumbe kwa wadau kuhusu kaulimbiu ya wiki ya maji na siku ya maji Duniani na kuhamasisha wananchi na wadau wengine kushiriki katika kupanga, ujenzi, uendeshaji na matengenezo ya miradi ya maji na usafi wa mazingira. Vilevile, maadhimisho ya wiki ya maji yanalenga kujenga na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wadau wa sekta hiyo.
Akiongelea maandalizi na matukio ya maadhimisho ya hayo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa maandalizi hayo yanaendelea vizuri na uzinduzi na kilele cha maadhimisho vitahusisha viongozi wa kitaifa. Amesema kuwa matukio ya mwaka 2012 yanalenga kuwashirikisha wadau na wananchi wote kwa pamoja kupanga, kujenga, kuendesha na kufanya matengeneza miradi ya maji na kuimarisha usafi wa mazingira sambamba na kutunza vyanzo vya maji.
Dk. Christine amezitaja shughuli zitakazofanyika katika maadhimisho hayo kuwa ni uzinduzi wa miradi ya maji ambayo ujenzi wake umekamilika. Amesema kuwa miradi mingi imetekelezwa kupitia programu ya maendeleo ya sekta ya maji na wadau mbalimbali.
Kuhusu unufaishaji wa miradi hiyo itakayozinguliwa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa miradi hiyo itawanufaisha wananchi wapao 184,900.
Mkuu wa Mkoa amesema kuwa maadhimisho hayo kitaifa yatagharamiwa na Wizara ya Maji, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mamlaka za Majisafi na majitaka nchini, Halmashauri, Taasisi na Mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali na wamiaji maji. Vilevile, amewashukuru wadau wote kwa utayari wao wa kuchangia ili kufanikisha maadhimisho hayo.
=30=


IRINGA MWENYEJI WIKI YA MAJI KITAIFA



Mkoa wa Iringa umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho ya 24 ya wiki ya Maji kitaifa ambapo shughuli na maonesho ya vifaa na teknolojia usambazaji maji na usafi wa mazingima vitafanyika ili kutoa ujumbe uliokusudiwa kwa wananchi.
 
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari ofisini kwake, Mkuu wa Mkoa wa Iringa ambaye ndiye mwenyeji wa maadhimisho hayo Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa maadhimisho hayo yatafanyika katika Mkoa wa Iringa kuanzia tarehe 16-22 Machi, 2012. amesema “kilele cha maadhimisho kitakuwa tarehe 22 Machi ambayo  siku hiyo inafahamika Kimataifa kuwa ni Siku ya Maji Duniani kwa mujibu wa Azimio Na. 193/47 la Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa”. Amesema kuwa uzinduzi na kilele cha wiki ya maadhimisho hayo kitakuwa katika uwanja wa Samora, Manispaa ya Iringa.
 
Amesema miongoni mwa shughuli zitakazofanyika katika maadhimisho hayo ni pamoja na kufanya usafi wa mazingira katika vyanzo vya maji, matanki na visima vya maji katika miji na vijiji mbalimbali mkoani Iringa.
 
Amesema kuwa shughuli nyingine ni maonesho ya vifaa na teknolojia za usambazaji wa maji na usafi wa mazingira vitafanyika katika uwanja wa Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa na kusisitiza kuwa maonesho yatafanyika muda wote wa maadhimishoyo ya wiki ya Maji.
 
Dk. Ishengoma amesema kuwa maadhimisho ya wiki ya maji mwaka 2012 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “maji na usalama wa chakula”. Kuhusu madhumuni ya maadhimisho hayo, amesema kuwa yanalenga kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa programu ya maji, hali ya huduma ya maji na usafi wa mazingira na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma na uhifadhi wa rasilimali za maji. Maadhimisho hayo pia yanalenga kutoa ujumbe kwa wananchi juu ya kaulimbiu ya wiki ya maji na siku ya maji duniani pamoja na kuimarisha mshikamano baina ya wadau wa sekta ya maji.
 
Maadhimisho haya pia yanalenga kuhamasisha wananchi kushiriki katika kupanga, ujenzi na uendeshaji na matengenezo ya miradi ya maji na usafi wa mazingira na kutoa elimu juu ya sera ya taifa ya maji na utekelezaji wake.
 
Kuhusu maandalizi ya wiki ya maji, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa maandalizi yake yanaendelea vizuri na uzinduzi na kilele cha maadhimisho hayo vitawahususha viongozi wa kitaifa. Amesema kuwa shughuli mbalimbali zitafanyika katika maadhimisho hayo zikiwa ni uzinduzi wa miradi ya maji ambayo ujenzi wake umekamilika. Kuhusu ugharimiaji wa miradi hiyo, Dk. Ishengoma amesema kuwa miradi mingi imetekelezwa kupitia programu ya maendeleo ya sekta ya maji na wadau mbalimbali. Amesema jumla ya wananchi 184,900 wananufaika na miradi itakayozinduliwa.
 
Ikumbukwe kuwa kila mwaka kuanzia mwaka 1988, Tanzania imekuwa ikiadhimisha Wiki ya Maji kuazia tarehe 16-22  Machi kwa kuwahusisha wananchi na wadau wote wa maji. 

Monday, March 5, 2012

VP AWATAKA WANAWAKE KUHUDHURIA KLINIKI

Makete
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal amewataka wanawake Mkoani Iringa kuhakikisha wanahudhuria kliniki tokea hatua za awali za ujauzito ili waweze kutapa huduma za kitaalamu mapema.

Kauli hiyo ameitoa katika eneo la Mfumbi wilayani Makete alipokuwa akisalimia wananchi wa wilaya ya hiyo baada ya kuweka jiwe la msingi soko lililojengwa kwa nguvu za wananchi na kupokea taarifa ya Mkoa na wilaya ya Makete alipowasili mkoani Iringa kuanza ziara yake ya siku tatu mkoani hapa akitokea mkoani Mbeya.

Dk. Bilal amewata mkoani hapa kuhudhuria kliniki ili kunufaika na huduma za afya na ushauri kwa wajawazito kutokana na serikali kuwekeza sana katika afya ya mama na mtoto.

Akiongelea maambukizi ya Ukimwi, Makamu wa Rais amesema kuwa taifa bado linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo idadi ya maambukizi ya Ukimwi na kuitaka jamii kuwa makini zaidi na kujilinda. Vilevile, ameitaka jamii kuendelea kushirikiana na juhudi za serikali kupambana na maambukizi ili kupunguza idadi ya vifo nchini.

Katika taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Iringa, iliyowasilishwa kwa Makamu wa Rais na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amesema kuwa mkoa umeongeza vituo vya kutolea huduma za Afya hadi kufikia 420  kwa lengo la kutoa huduma bora za afya kwa kuzingatia mahitaji ya makundi maalumuhasa watoto wachanga na walio na umri chini ya miaka mitano, wazee na wanawake walio katika uzazi.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa katika kutekeleza sera ya zahanati kwa kila kijiji, mkoa umefikia asilimia asilimia 57 ya vijiji vyote kuwa na zahanati wakati asilimia 23 ya kata zote zina vituo vya afya.

Akiongelea huduma za mama wajawazito na watoto, Dk. Ishengoma amesema kuwa katika mwaka 2011 akina mama waliojifungulia kliniki walikuwa ni 54,356 sawa na asilimia 57.3 ya akina mama wajawazito waliotarajiwa kuhudhuria huduma za kliniki.

Amesema kuwa kiwango cha akina mama wajawazito waliojifungulia katika vituo vya tiba imefikia asilimia 76.2.

Amesema kuwa vifo vya wazazi vimepungua kutoka 162/100,000 mwaka 2010 hadi kufikia 138/100,000. Aidha, vifo vya watoto vimepungua kutoka 21/1,000 hadi 17/1,000.

Makamu wa Rais yupo katika ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Iringa.
 =30=




 MAKETE WATAKIWA KUKITUMIA CHUO CHA VETA
Makete
Wananchi wa Wilaya ya Makete wametakiwa kuonesha kuwa wapo tayari kukitumia chuo cha ufundi stadi VETA kwa kujipanga vizuri kukitumia na kukiendeleza chuo hicho ili kiweze kuwanufaisha wakazi wa wilaya ya Makete na taifa kwa ujumla.

Rai hiyo imetolewa na Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal wakati akizungumza na wakazi wa wilaya ya Makete baada ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa chuo cha ufundi stadi VETA wilayani hapa.

Dk. Bilal amesema kuwa “wilaya ya Makete tumepata fursa kubwa kuwa na VETA Makete” na kuutaka uongozi wa wilaya hiyo kujipanga vizuri kuonesha kuwa wao ni namba moja kwa kujenga uhusiano mzuri kati ya VETA Makete na mamlaka ya ufundi stadi nchini.

Amesema kuwa siku zote VETA lazima iwe karibu na jamii inayoihudumia kwa kutokuweka mwanya kati yake ili jamii inufaike na VETA na kinyume chake.
Makamu wa Rais ameutaka uongozi wa VETA wilaya ya Iringa kutafakari kwa kina kile kinachoitajika katika jamii hasa wakati uliopo sasa na kutoka na masuluhisho ya matatizo yaliyopo katika jamii.

Amesema kuwa ili wananchi wapige hatua hawana budi kukifahamu chuo cha VETA na matarajio yake katika kuihudumia jamii ili kuisaidia kupiga hatua ya kimaendeleo.

Aidha, amekitaka chuo hicho kutoa wanafunzi waliopikika na kuiva ili kukabiliana na ushindani uliopo katika soko na kuleta picha nzuri katika jamii. Amesema wakati mambo mengi yanakua kwa haraka, elimu ya ufundi stadi inatakiwa kupanuliwa zaidi kwa kuhusisha teknolojia ya habari kuwafikia watu wengine wali mbali zaidi na kuwafanya wanufaike na huduma hizo.

Katika taarifa ya Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugu amesema kuwa hivi karibuni nchi za afrika Masharki zitafungua milango yake itakayomtaka mtu mmoja kwenda kusaka ajira katika nchi nyingine. Amesema kwa muktadha huo “hatuna budi kuwaandaa vijana wetu katika elimu ya ufundi stadi ili wasiwe watazamaji”. Amesema kuwa serikali inaendelea na upanuaji wa mafunzo stadi ili kuwawezesha vijana wengi kujiunga na mafunzo hayo. Ameongeza kuwa serikali itaendelea kuongeza kasi ya ujenzi wa vyuo vya ufundi na kuboresha utoaji wa elimu bora ya mafunzo stadi nchini.

Chuo cha ufundi stadi VETA wilaya ya Makete ndicho chuo cha kwanza kwa mujibu wa sera ya chama tawala ya kujenga chuo cha VETA kila wilaya nchini na kinatajia kuanza mwezi Julai 2012 kwa kuanza na wanafunzi 160 katika fani za ujenzi, uashi, uselemala, ufundi wa magari.

=30=   


KILIMO CHA MTAMA CHAHIMIZWA IRINGA
 Makete
Mkoa wa Iringa unahimiza kilimo cha mtama, mihogo na mazao mengine yanayovumilia ukame ukiwa ni mkakati wa kukabiliana na hali ya ukame wa mara kwa mara unaosababisha upungufu wa chakula kwa baadhi ya maeneo mkoani hapa.

Katika taarifa ya maendeleo ya mkoa wa Iringa iliyowasilishwa kwa Makamu wa Rais, na Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa ushauri wa kilimo cha mazao yanayovumilia ukame kama mtama, mhogo na mazao mengine umetolewa kwa Halmashauri zenye maeneo ya ukame ili kukabiliana na hali ya ukame wa mara kwa mara.

Amesema viongozi na wataalamu wa wilaya ya Iringa, Kilolo pamoja na Mkoa walitembelea kilimo cha mtama wilaya ya mpwapwa mwezi Mei, 2011 ili kujifunza uzalishaji wa zao la mtama ili waweze kuhimiza kilimo hicho maeneo yote yanayokabiliwa na ukame katika wilaya hizo.

Katika kuhakikisha hamasa inakuwepo katika kilimo hicho Mkuu wa Mkoa wa Iringa alifanya ziara katika wilaya hizo kuhimiza kilimo cha mazao yanayostahimili ukame ili kuzifanya kaya zinazokabiliwa na upungufu wa chakula kuwa na uhakika wa chakula.

Amesema kuwa kila mkulima amehimizwa kulima ekari mbili za mtama kwa lengo la kuwa na uhakika wa chakula. Amesema kuwa kila shule katika maeneo hayo imetakiwa kulima ekari mbili kwa ajili ya chakula cha wanafunzi wakati wa mchana.

Amesema kuwa viongozi wote kuanzia ngazi ya wilaya hadi kijiji nao wamelima ekari mbili za mtama kila mmoja na muitikio wa agizo hilo umepokelewa vizuri.  

Akiongelea sekta ya afya, Mkuu wa Mkoa amesema kuwa hadi kufikia mwaka 2011 akina mama waliohudhuria kliniki ni 54,356 sawa na asilimia 57.3 ya akina mama wajawazito waliotarajiwa kuhudhuria huduma za kliniki. Aidha, amesema kuwa kiwango cha akina mama wajawazito waliojifungulia katika vituo vya tiba imefikia asilimia 76.2.

Amesema kuwa vifo vya wazazi vimepungua kutoka 162/100,000 katika mwaka 2010 hadi kufikia 138/100,000, wakati vifo vya watoto vimepungua kutoka 21/1,000 hadi kufikia 17/1,000.

Akiongelea hali ya maambukizi ya UKIMWI, Dk. Ishengoma amesema kuwa maambukizi yamefikia asilimia 15.7 na mkoa katika kukabiliana na hali hiyo mkoa uliandaa mpango wa miaka minne wa kupambana na maambukizi ya UKIMWI unaoendelea kutekelezwa. Amesema mpango huo ulioandaliwa na wadau wa sekta binafsi na umma ni wa kuanzia Oktoba 2008 hadi Septemba, 2012. 

Katika salamu za Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal kwa wananchi wa Mfumbi wilaya ya Makete amesema kuwa taifa bado linakabiliwa na changamoto mbalimbali pamoja na idadi ya maambukizi ya UKIMWI na kuwataka wananchi kuwa makini zaidi na kujilinda. Amewataka kuendelea kushirikiana na serikali katika kuhubiri mapambano hayo ili kupunguza maambukizi.

Dk. Bilal pia amewataka akina mama wajawazito kuhudhuria kliniki mara kwa mara pindi wanapojigundua kuwa ni wajawazito ili waweze kunufaika na huduma hizo zinazotolewa kwa ajili yao.

Makamu wa Rais, anafanya ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Iringa katika wilaya za Makete, Njombe, Mufindi na Iringa na akiwa wilayani makete ameweka jiwe la msingi mradi wa soko lililojengwa kwa nguvu za wananchi katika kijiji cha Mfumbi, kuzindua nyumba ya walimu  katika sekondari ya Kitulo na kuweka jiwe la msingi chuo cha VETA.
=30=