Friday, July 19, 2013

RC ATAKA JAMII ISHIRIKISHWE KATIKA UTUNZAJI WA BARABARA




Serikali mkoani Iringa imetaka jamii ishirikishwe ipasavyo juu ya dhana ya utunzani wa barabara ili kuhakikisha barabara zinadumu na kupitika muda wote. 

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akifungua kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa wa Iringa (RCC) kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.

Dkt. Christine amesema “katika kuhakikisha tunakuwa na barabara zinazopitika muda wote, nimeona mapungufu ya ushiriki wa jamii juu ya utunzaji wa barabara hizo. Wananchi wamekuwa wakifanya shughuli ndani ya hifadhi ya barabara na kuacha uchafu kwenye barabara na uchafu huo kuziba mifereji na kuharibu barabara”. Aidha, amewataka wajumbe wa kikao hicho kutoa elimu kwa wananchi ili washiriki kikamilifu katika utunzaji wa barabara hizo ili ziweze kudumu na kuwahudumia kwa muda mrefu. Amesema kuwa uchafu unaharibu mazingira, unaziba mifereji ya barabara na kusababisha mafuriko kwenye makazi ya wananchi.

Mkuu wa mkoa wa Iringa ametoa rai kwa viongozi na wananchi kushirikiana na miradi ya ujenzi na ukarabati wa barabara ya Iringa –Dodoma na Iringa-Mafinga. Amesema kuwa ushirikiano huo na elimu kwa wananchi utasaidia kukomesha hujuma za wizi hasa wa mafuta na ementi ili miradi hiyo iweze kuwa ya manufaa kwa mkoa wa Iringa na taifa kwa ujumla na kukamilika kwa muda muafaka.

Aidha, amewataka wajumbe hao kuendela kushirikiana katika kutoa elimu kwa wananchi juu ya Sheria mpya ya hifadhi ya barabara ambayo ni mita 30 kil upande kutoka katikati ya barabara. Amesema “wananchi waendelee kuelimishwa juu ya umuhimu wake kwani wanapojenga na kubomolewa nyumba zao haipendezi. Inawagharimu na kuwaumiza sana” alisisitiza Mkuu wa mkoa wa Iringa.
=30=