Wednesday, September 1, 2010

RAS Iringa awaweka sawa watumishi wake

Wafanyakazi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa wametakiwa kuchukua tahadhari na jitihada za dhidi ya majanga ya moto yanayoweza kujitokeza katika ofisi hiyo.
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka akiongea na wafanyakazi wake


Tahadhali hiyo imetolewa na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Gertrude Mpaka katika kikao baina yake na wafanyakazi wote wa ofisi yake kilichofanyika leo katika ukumbi wa RAS.

Mpaka amesema “nimewaita hapa ili tuelezane na kuchukua hatua za tahadhari katika ofisi zetu na matumizi sahihi ya vifaa vinavyotumia umeme ili moto usitokee na kuunguza ofisi”. Ameongeza kuwa kila mfanyakazi lazima ahakikishe anazima vifaa vyote vya umeme pindi amalizapo kazi na kutenganisha kebo za umeme na soketi za ukutani. Aidha amesisitiza kuwa kikao hicho anakipa umuhimu mkubwa japokuwa ofisi yake imekuwa ikiwakumbusha mara kwa mara wafanyakazi wake kuchukua tahadhari na matumizi sahihi vya vifaa vya moto.

Akiongelea hali ya usalama katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mwangalizi wa Ofisi, Avelyne Ngonyani, amesema kuwa hali ya usalama katika ofisi hiyo ni ya kuridhika baada ya kujiwekea mikakati kadha wa kadha ya kuimarisha usalama. Ngonyani amechukua nafasi hiyo kuwakumbusha wafanyakazi wote kuwa lazima funguo zote za ofisi zihifadhiwe katika ‘combination locks’. Ameongeza kuwa katika kuimarisha usalama kila mfanyakazi lazima asaini kitabu cha mahudhuria pindi aingiapo ofisini na baada ya muda wa kazi pia.

Akichangia katika usalama wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Rasilimali watu, Barnabas Ndunguru amesisitiza kuwa funguo za ofisi ni nyaraka za serikali na ni kosa kwa mfanyakazi yeyote kuondoka na funguo hizo. Aidha amesisitiza kuwa endapo mfanyakazi atahitaji kufanya hivyo au kuendelea na kazi baada ya muda wa kazi basi hanabudi kuomba kibali kutoka kwa mkuu wa utawala ofisini hapo.

Katibu Tawala Mkoa pia amegusia kuwa nchi ipo katika kampeni za uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31, 2010 na kusisitiza kuwa “joto la kampeni za uchaguzi limeanza, hivyo wafanyakazi hatutakiwa kushabikia siaka katika ofisi za umma na katika muda wa kazi japokuwa tuna vyama vya siasa”. Mpaka amechukua nafasi hiyo kuwatakia maandalizi mema ya uchaguzi mkuu na kuwataka wafanyakazi wote wajitokeze kupiga kura.


Baadhi ya wafanyakazi wa ofisi ya RAS Iringa wakimsikiliza RAS wao leo