Friday, January 1, 2016

TADB YATOA MIKOPO YA KILIMO IRINGA




Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa - IRINGA
Sekta ya kilimo ni muhimili wa uchumi nchini pamoja na kukabiliwa na changamoto nyingi katika ukuaji wake hasa upatikanaji mikopo.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza wakati wa utiaji saini makubaliano ya mikopo kati ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania na wakulima wadogo wadogo wa mkoa wa Iringa katika kijiji cha Igomaa wilayani Mufindi.
 
Mkuu wa Mkoa wa Irirnga, Amina Masenza
Masenza alisema “ikumbukwe kuwa umuhimu wa sekta ya kilimo unachagizwa na ukweli kuwa ni sekta ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 75 ya wananchi wanaoishi vijijini, ambao wanategemea kilimo, ufugaji na uvuvi kwa ajili ya maisha yao. Kadhalika, wakulima, wafugaji na wavuvi wanatumia zana na mbinu duni katika shughuli zao, hivyo kushindwa kupata matokeo mazuri ya mazao”. Aliongeza kuwa pamoja na mchango mkubwa wa wakulima kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi, kwa mujibu wa takwimu zilizopo kuhusu hali za maisha ya wakulima nchini siyo ya kuvutia hata kidogo. Wengi mapato yao yapo chini na wanaishi maisha duni sana.

Lengo la serikali ya awamu ya tano ni kuimarisha sekta ya kilimo ili iweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa nchi na kuwanufaisha wakulima, wafugaji na wavuvi katika kuyabadilisha maisha yao  kwa kupitia mikopo na pembejeo za kisasa na mbegu bora zaidi. “Naamini ujio wa benki ya maendeleo ya kilimo (TADB) ni mwanzo tu wa maandalizi ya matokeo halisi ya ndoto na matamanio ya rais wetu, hivyo sina budi kuwapongeza na kuwaunga mkono katika hatua zote mnazozifanya katika kuwakopesha wakulima wadogo wadogo” alisisitiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Akiongelea changamoto iliyopo katika upatikanaji wa mikopo kwa ajili ya kilimo katika taasisi za kifedha, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, alisema kuwa upatikanaji wa fedha ni mgumu kutokana na mikopo mingi kuelekezwa katika biashara za bidhaa na riba kubwa kwenye mikopo ya kilimo. Aliongeza kuwa masharti ya dhamana ni kikwazo kikubwa kwa wakulima wadogo wengi. Alisema kuwa kuanzishwa kwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ni fursa kubwa kwa wakulima nchini.
=30=