Monday, December 21, 2015

RC IRINGA AWATAKIA HERI MAJERUHI WA AJALI YA BASI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza amewatakia heri na kupona haraka majeruhi wote wa ajali ya basi ili waweze kuungana na familia zao na kuendelea na majukumu yao.

Kauli hiyo aliitoa muda mfupi baada ya kufanya ziara ya kustukiza katika hospitali ya rufaa ya Iringa kujionea jinsi majeruhi wa ajali ya basi la kampuni ya New Force wanavyohudumiwa hospitalini hapo.

Masenza akiyeambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa wa Iringa alisema kuwa ajali hiyo imemuhuzunisha yeye binafsi na mkoa kwa ujumla. Alisema kuwa anawaombea kwa Mungu majeruhi wote kupata nafuu na kupona kabisa ili waweze kuendelea na majukumu yao ya ujenzi wa Taifa.

Akiongelea hali ya huduma hospitali hapo, Masenza alisema kuwa ameridhishwa na jinsi majeruhi wa ajali hiyo walivyopokelewa na kutibiwa hospitalini hapo. Aidha, aliwataka madaktari na wauguzi kuendelea kuonesha moyo wa huruma na uwajibikaji wanapowahudumia majeruhi wa ajali hiyo. Aidha, aliwahakikishia majeruhi hao kuwa serikali ipo pamoja nao kuhakikisha wanapata huduma bora ili wapone haraka na kuendelea na majukumu yao.

Ajali hiyo ilitokea kwa basi kugongana na lori ilitokea tarehe 18 Disemba, 2015 mchana baada ya tairi la lori lori namba T 616 DES la kampuni ya Ranfad Ltd kupasuka kupasuka na lori kukosa muelekeo na kuligonga basi la kampuni ya New Force namba T 483 CTF na kusababisha vifo vya abiria 12 na majeruhi 28. Miongoni mwa majeruhi hao, watatu ni raia wa Kongo DRC na mmoja raia wa Afrika Kusini.

=30=

Wednesday, December 9, 2015

SIKU YA UHURU WA TANZANIA BARA ILIVYOADHIMISHWA MKOANI IRINGA

Wananchi wakifanya usafi katika kijiji cha Ruaha Mbuyuni A

Mkuu wa Mkoa wa Irirnga, Mhe. Amina Masenza akiwaongoza maafisa waandamizi kuelekea eneo la kufanya usafi

Zoezi la usafi likiendelea

Zoezi la usafi likiendelea

Mkuu wa Mkoa akichoma taka

Upande wa pili Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bibi Wamoja Ayubu wanne (kulia) akiongoza vikosi vya usalama kuelekea eneo la kusanya usafi

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu wakwanza mbele (kulia)

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi (katikati) katika zoezi la usafi

Zoezini

Wananchi baada ya kuhitimisha zoezi la usafi

Baada ya zoezi la usafi

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Amina Masenza

Wananchi wakisikiliza nasaha za Mkuu wa Mkoa

Mkuu wa Mkoa akiongea na wananchi

Wadau wa sekta ya usafi wakifuatilia nasaha za Mkuu wa Mkoa

Mdau wa siku ya Uhuru wa Tanzania bibi Scolastica

Wananchi wakifuatilia nasaha za Mkuu wa Mkoa

Wananchi wakisikiliza nasaha za Mkuu wa Mkoa wa Iringa

Mkurugenzi Mtendaji (W) Kilolo, Rukia Muwango akijibu hoja za wananchi

Shaban Lubathillah Afisa Ushirika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa akifanya usafi katika Uso wa ofisi hiyo

Wednesday, November 18, 2015



TANGAZO

NDUGU WANA IRINGA

CHAMA CHA MADAKTARI WANAWAKE TANZANIA, WAKISHIRIKIANA NA WIZARA YA AFYA NA USTAWI WA JAMII, WATAFANYA ZOEZI LA UPIMAJI WA HIARI WA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI KWA WAKINA MAMA WOTE WA MJINI IRINGA

ZOEZI HILI LITAFANYIKA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA IRINGA NA HOSPITALI YA FRELIMO SIKU YA TAREHE 19-20/11/2015 KUANZIA SAA NNE ASUBUHI

ZOEZI HILI NI BURE

UKISOMA TANGAZO HILI MFAHAMISHE NA MWENZAKO.

ASANTE NA KARIBU SANA

Tuesday, November 17, 2015

TAARIFA KWA MGENI RASMI MHE. AMINA JUMA MASENZA MKUU WA MKOA IRINGA KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA CHOO DUNIANI, SIKU YA UNAWAJI MIKONO DUNIANI NA WIKI YA USAFI WA MAZINGIRA TANZANIA TAREHE 14/11/2015



Katibu Tawala Mkoa,
Mkuu wa wilaya
Katibu Tawala Wilaya
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Kilolo
Viongozi mbalimbali
Waandishi wa Habari,
Mabibi na Mabwana.

Mhe. Mgeni Rasmi; Uboreshaji wa huduma za Maji, Afya na Usafi wa Mazingira unajumuisha uboreshaji wa huduma zote za upatikanaji wa Maji safi na salama,  Matumizi ya vyoo bora, unawaji wa mikono kwa sabuni katika nyakati muhimu, Uboreshaji wa usafi wa Mazingira katika ngazi ya jamii na Taasisi.  Uboreshaji wa huduma hizi ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa kwa sababu huchangia kujenga afya bora kwa wananchi hivyo kuongeza nguvu kazi ya Taifa.
Mganga Mkuu wa Mkoa, Dkt. Robert Salim


Mhe. Mgeni Rasmi; katika kuhakikisha nchi yetu inafikia lengo la Milenia namba saba (7) ambalo linalenga kupunguza kwa nusu idadi ya watu ambao hawana huduma ya vyoo bora ifikapo mwaka 2015. Tanzania ilianzisha Kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa Mazingira ambayo ilizinduliwa na Mhe. Rais wa Awamu ya nne Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete  tarehe 5 Juni 2012 yenye kauli mbiu ya Usafi ni Ustaarabu unaanza na sisi.  Kampeni hii inalenga kuongeza ujenzi wa vyoo bora katika kaya 1,520,000 na shule 812 ifikapo mwaka 2015.  Ambapo mkoa wa Iringa ulipewa lengo la kufikia kaya 41,984 Na shule 16
Mkoa wa Iringa ulianza kutekeleza kampeni hii mwaka 2012 kwa Halmashauri 2 za Wilaya ya Iringa na Mufindi zilianza utekelezaji.  Katika mwaka 2013 Halmashauri ya Manispaa ya Iringa na Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo zilianza utekelezaji na kufanya Halmashauri zote za Mkoa kuwa zinatekeleza Kampeni hii.  Kwa sasa jumla ya kata 33 kati ya kata 103 kutoka katika Halmashauri za mkoa wa Iringa zimeanza kutekeleza Kampeni hii. Hadi kufikia Septemba 2015 ni jumla ya kaya 21,727 (52%) ya lengo ziliboresha  vyoo vyake kupitia uhamasishaji shirikishi wa jamii “Uchefuaji.

Utekelezaji kwa kila Halmashauri ni Iringa MC kaya  3914 (48%), Iringa DC kaya 5,792 (44.8%), Mufindi kaya  9,613 (68%) na Kilolo kaya 2408 (34.5%).  Vilevile, jumla ya shule 52 zimeweza kujenga vyoo bora kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya mapato ikiwemo fedha maalum ya mfuko wa Kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa Mazingira na jumla ya mafundi 191 wamepatiwa mafunzo ya ujenzi wa vyoo bora kwa kutumia Teknolojia rahisi. Aidha, Takwimu za hali halisi ya uwepo wa vyoo zinaonyesha kuwa jumla ya kaya 201,120 (89%) mkoani Iringa zinavyoo na kati ya hizo ni asilimia 17 tu ndiyo zenye vyoo bora.

Mhe. Mgeni Rasmi; Ukitaza taarifa  ya utekelezaji Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ndiyo ipo chini katika utekelezaji.  Hivyo tumeamua kufanya maadhimisho haya katika wilaya hii ili kutoa hamasa kwa jamii iweze kujenga vyoo bora na kuboresha usafi wa mazingira kwa ujumla.  Aidha takwimu zinaonyesha kwamba katika kata ya Uhambingeto kaya 1227 (57%) kati ya kaya 2116 zina vyoo bora.  Na katika vijiji vyote vya kata hii hakuna kitongoji kilichoweza kufikia kuwa na kaya zote zenye vyoo bora ambalo ndiyo lengo kuu la Kampeni hii. Hali hii inahitaji jitihada za makusudi za uongozi wa kata na vijiji kuboresha hali ya usafi wa mazingira ili kujikinga na magnjwa yakuambukiza.

Mhe. Mgeni Rasmi; Maadhimisho ya Siku ya Choo Duniani, siku ya Unawaji Mikono kwa Sabuni Duniani na Wiki ya Usafi Tanzania ni moja ya  jitihada za Serikali katika kuhakikisha inafanya uhamasishaji wa jamii ili kuiwezesha kuchukua hatua ya kuzifanyia kazi changamoto zilizopo katika kuboresha huduma za maji, afya na usafi wa mazingira.

Kimatiafa siku ya kunawa mikono huadhimishwa kila tarehe 15 Oktoba na siku ya Choo Duniani huadhimishwa kila tarehe 19 Novemba.  Tanzania kwa kuzingatia umuhimu wa uboreshaji wa huduma hizi, iliamua kutenga wiki inayoanzia tarehe 13 hadi 19 Novemba kuwa ni wiki ya usafi Tanzania ambapo maadhimisho yake yalianza rasmi mwaka 2013.  Katika maadhimisho haya Tanzania huadhimisha kwa pamoja Siku ya Choo duniani, Siku ya kunawa Mikono Duniani na Wiki ya usafi Tanzania.

Mhe. Mgeni Rasmi;  Kauli mbiu ya maadhimisho haya huenda sambamba na kauli mbiu ya maadhimisho  ya Siku ya Choo Duniani  ambapo kwa mwaka  huu  kimataifa inasema “ USAFI WA MAZINGIRA NA LISHE. (SANITATION &NUTRITION) Kutokana na Mlipuko wa kipindupindu unaoendelea nchini, kauli mbiu ya Kitaifa imejikita katika ujumbe wa kutokomeza ugonjwa huo. Kauli mbiu hiyo ni “ KIPINDUPINDU HAKIKUBALIKI, PUNGUZA MAAMBUKIZI MAPYA, ZINGATIA USAFI WA MAZINGIRA.
Mhe. Mgeni Rasmi;  Katika kuadhimisha wiki hii shughuli mbalimbali za uhamasishaji zitakuwa zikifanyika shughuli hizo ni pamoja na:
·        Uhamasishaji wa nyumba kwa nyumba na utoaji wa elimu
·        Usafishaji wa pamoja na maeneo ya kuishi na taasisi
·        Usafishaji wa pamoja na maeneo ya wazi
·        Uelimishaji wa jamii kupitia matangazo ya redio
·        Usambazaji wa ujumbe kupitia vipeperushi na mabango unaohamasisha matumizi ya choo bora, usafi wa mazingira na kunawa mikono kwa sabuni nyakati tano muhimu.  Nyakai hizo ni kabla ya kutayarisha  chakula, kabla ya kula, kabla ya kumlisha mtoto, baada ya kutoka chooni na baada ya kumsafisha mtoto aliyejisaidia
·        Maonesho ya bidhaa mbalimbali za usafi wa mazingira.
·        Vilevile Ofisi ya Mkuu wa Mkoa imeandaa warsha maalum kwa waandishi wa habari toka vyombo mbalimbali vya habari vya mkoa wa Iringa kwa lengo la  kufikisha ujumbe wa usafi wa mazingira kwa jamii katika wiki hii.
Aidha katika siku ya leo ya uzinduzi kutakuwa na Zoezi la unawaji wa mikono kwa kuhusisha watu wengi kwa lengo la kutoa Elimu na kuihamasisha jami juu ya njia sahihi ya unawaji mikono kwa sabuni.

Mhe. Mgeni Rasmi;
Naomba kuwasilisha.


Dkt. Robert Salim
MGANGA MKUU WA MKOA WA IRINGA.

HOTUBA YA MKUU WA MKOA WA IRINGA MHE. AMINA MASENZA KATIKA UZINDUZI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA KUNAWA MIKONO DUNIANI, SIKU YA CHOO DUNIANI NA WIKI YA USAFI TANZANIA KATIKA KIJIJI CHA UHAMBINGETO, HALMASHAURI YA WILAYA YA KILOLO MKOANI IRINGA NOVEMBA 14, 2015




Katibu Tawala Mkoa,
Wakurugenzi wa Halmashauri,
Viongozi wa Serikali na Taasisi mbalimbali
Waandishi wa Habari,
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana.

Awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kujumuika na kushiriki kikamilifu katika Siku ya  Uzinduzi wa Wiki ya Usafi wa Mazingira Kimkoa inayofanyika hapa kijiji cha Uhambingeto.

Napenda kutoa pongezi maalum kwa wananchi wa Uhambingeto kwa kufika hapa kwa wingi kushiriki katika uzinduzi huu wa maadhimisho haya kimkoa. Kufika kwenu ndiyo ufanisi wa shughuli hii na mafanikio yake. Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitawashukuru washirika wetu wa maendeleo kwa michango na misaada yao adhimu. Marafiki zetu wametuunga mkono katika juhudi zetu za kuboresha huduma za usafi wa mazingira mijini na vijijini. Ninawaomba, wawakilishi wa mashirika waliopo hapa, wazipokee na kuzifikisha shukrani zetu za dhati, kwa wakuu wa mashirika yao.

 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Amina Masenza

Umuhimu wa Maadhimisho

Ndugu Wananchi;
Maadhimisho ya Siku ya kunawa mikono Duniani, Siku ya choo Duniani na wiki ya Usafi Tanzania, ambayo yameanza rasmi mwaka 2013, ni ushahidi wa umuhimu ambao Serikali na wananchi wanaoutoa katika kuboresha usafi wa mazingira nchini. Kwa miaka mingi tarehe 19 Novemba dunia imekuwa ikiadhimisha  siku ya choo duniani na 15 oktoba siku ya kunawa mikono kwa sabuni Duniani. Mwaka 2013 Umoja wa Mataifa ulipitisha tarehe 19 Novemba kuwa ni siku rasmi ya maadhimisho ya Choo Duniani kutokana na ukweli kuwa kati ya malengo yote ya maendeleo ya milenia ndio lengo pekee ambalo liko nyuma kiutekelezaji. Katika mwaka huo huo Tanzania ilipitisha rasmi wiki ya tarehe 13 hadi 19 Novemba kuwa ni wiki ya Usafi Tanzania. Tanzania huadhimisha kwa pamoja katika wiki hii Siku ya Kunawa Mikono Duniani na Siku ya Choo Duniani. Kwa mwaka huu Maadhimisho haya Kitaifa yanafanyika Mkoani Njombe.

Lengo kuu la maadhimisho haya ni kuhamasisha jamii ili iweze kuchukua hatua katika kukabiliana na changamoto za kukosa huduma za choo bora na uboreshaji wa usafi wa mazingira kwa ujumla, ambapo mkazo huwekwa katika uhamasishaji wa matumizi ya vyoo bora, unawaji wa mikono kwa sabuni, njia sahihi za kutibu na kutunza maji ya kunywa majumbani, na usafishaji wa maeneo yanayotuzunguka.

Maadhimisho haya pia yanatoa nafasi kwa wadau kujadili mafanikio yaliyopatikana na matatizo yaliyopo katika kuendeleza usafi wa mazingira ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vyoo bora na kuyatafutia ufumbuzi. Kwa pamoja, kama taifa, tunapata fursa ya kufanya tathmini ya tulikotoka, tulipo sasa na kuainisha malengo na mipango yetu kwa siku zijazo.

Kauli Mbiu ya Maadhimisho

Ndugu Wananchi; Kauli mbiu ya Maadhimisho ya mwaka huu ina ujumbe mzito sana: Kipindupindu  Hakikubaliki, Zuia Maambukizi Mapya, Zingatia Usafi wa Mazingira”. Ni ukweli ulio wazi kuwa bila kuchukua jitihada za makusudi za kuboresha usafi wa mazingira yetu janga hili la kipindupindu litaendelea kuwepo na watu wataoendelea kupoteza maisha na kupunguza nguvu kazi.

Kwa kutambua ukweli huo kuhusu usafi wa mazingira, katika siku ya leo na katika wiki yote hii tafakuri zetu tuzielekeze kwenye kutafuta mikakati na mbinu za kuhakikisha kuwa tunaboresha usafi wa mazingira katika maeneo yetu. Naomba tutambue kuwa mkakati wowote kwa ajili hiyo hauna budi ujielekeze katika kufanya mambo yafuatayo:
1.  Kujenga vyoo bora na kuvitumia
2.  Kunawa mikono kwa maji safi na sabuni katika nyakati tano muhimu,
3.  Kusafisha maeneo yanayotuzunguka,
4.  Kuboresha usafi binafsi na kuaacha tabia ya kutupa taka ovyo.


Ndugu Wananchi;
Huduma duni za usafi wa mazingira zinachangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa milipuko ya magonjwa ya kuhara ikiwemo kipindupindu na kusababisha vifo ambavyo vingeweza kuzuilika. Katika mlipuko wa Kipindupindu unaoendelea nchini takriban watu 106 wameshapoteza maisha.   Idadi hii ni kubwa na pengo kubwa kwa familia zao na Taifa kwa ujumla.
Aidha, Kwa mujibu wa Shirika la UNICEF na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Ugonjwa wa kuhara bado ni miongoni mwa magonjwa makuu matano yanayochangia katika vifo kwa watoto wadogo wenye umri chini ya miaka mitano nchini Tanzania. Takwimu zinaonyesha kwamba moja ya tatu ya vifo vya watoto vinavyotokea ndani ya mwezi wa kwanza wa maisha ya watoto vinatokana na maambukizi au magonjwa ya kuhara yanayosababishwa na:
·        Ukosefu wa maji safi na salama,
·        Mazingira machafu na kutozingatia tabia za usafi.
·        Madhara mengine yatokanayo na ukosefu wa maji safi na salama,
·        Mazingira machafu na kutozingatia tabia za usafi ni kudumaa (mtoto kuwa na kimo kifupi kisichoendana na umri na kuathiri ukuaji)
Takwimu zinaonesha kuwa asilimia 53 ya watoto chini ya miaka mitano mkoani Iringa wamedumaa.
Kunawa mikono kwa sabuni ni mojawapo ya njia rahisi na yenye gharama nafuu kuzuia maambukizi. Njia hii hupunguza uwezekano wa kupata maambukizi kwa 50% na matumizi ya choo bora hupunguza kwa 32%. Takwimu za utafiti uliofanywa na shirika la UNICEF katika mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya zinaonyesha kuwa kaya zenye vyoo bora ni 23%, kaya ambazo zina vyombo vya kunawia mikono na sabuni ni 9%, uoshaji wa mikono baada ya kumhudumia mtoto ni 56%, uoshaji wa mikono kabla ya kuandaa chakula ni 2% na uoshaji wa mikono kabla ya kumlisha mtoto ni 18%.
Ndugu Wananchi;
Uboreshaji wa usafi wa mazingira na kuzingatia kanuni zake ndio ngao pekee ya kujikinga na janga hili kubwa la ugonjwa wa kipindupindu. 

Hatua Zilizochukuliwa na Serikali kukabiliana na changamoto

Ndugu Wananchi;

Baadhi ya jitihada zinazofanywa na Serikali kukabili changamoto za usafi wa mazingira nchini ni:

(i) Utekelezaji wa Kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa Mazingira ambayo inalenga kuongeza idadi ya watu wenye vyoo bora na kuboresha usafi wa mazingira katika maeneo ya mikusanyiko, maeneo ya barabara kuu na kwenye Taasisi. Kwa mkoa wa Iringa kupitia Kampeni hii jumla ya mafundi 156 kutoka vijiji 156 wamefundishwa jinsi ya kujenga vyoo bora kwa gharama nafuu. Nawaomba tuwatumie mafundi hawa ili tuweze kujenga vyoo bora vijijini kwetu.

Nimesikia kuwa Mkoa wa Iringa tayari kuna kata 33 zinatekeleza Kampeni hii, naomba Wakurugenzi wa Halmashauri wapanue utekelezaji huu katika kata nyengine kwa kutumia vyanzo vya ndani vya mapato. Aidha, utekelezaji wa Kampeni hii kwa mkoa wetu hauridhishi kulingana na malengo kama tulivyosikia katika Taarifa ya Mganga Mkuu wa Mkoa. Hivyo nawaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kila Halmashauri inafikia malengo kwa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa Kampeni hii na kuwachukulia hatua watendaji wasio wajibika.  Katika utekelezaji wa Kampeni hii ili mwisho wa siku kila wananchi awe na Choo bora.


(ii) Kusimamia sheria zilizopo za usafi wa mazingira na kuwachukulia hatua wale wote wanaoenda kinyume na sheria hizi zikiwemo sheria ndogo za Halmashauri na vijiji.

Hivyo nachukua nafasi hii kuaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia kikamilifu Sheria hizo ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua wale wote watakaokiuka na kuifanya Kampeni hii isifanikiwe.


Ndugu  Wananchi;
Usafi wa Mazingira ni jukumu letu sote , na ni jukumu endelevu rai yangu kwenu ni kuendelea kufanya usafi katika maeneo yote yanayotuzunguka na kuhamasisha ujenzi na matumizi ya vyoo bora ya vyoo kwa afya ya kaya na Taifa kwa ujumla.  Lazima tuzingatie Kanuni zote za Usafi kama tunavyoelekezwa na wataalamu wa Afya. 

Baada ya kusema haya natamka kuwa uzinduzi wa maadhimisho siku ya kunawa Mikono Duniani, Siku ya Choo Duniani, na wiki ya Usafi wa Mazingira Tanzania imezinduliwa rasmi,

Aksanteni kwa kunisikiliza.



HAPA KAZI TU!!