Tuesday, November 21, 2017

JAMII YATAKIWA KUUNGA MKONO KIKUKI KUPAMBANA NA KIFUA KIKUU IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-IRINGA
Jamii imetakiwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na kikundi cha kudhibiti kifua kikuu mkoa wa Iringa (KIKUKI) ili kiweze kuwaibua wahisiwa wa ugonjwa wa kifua kikuu mkoani hapa.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa KIKUKI, Lucas Mallya alipokuwa akiongelea changamoto zinazokikabili kikundi chao kutekeleza majukumu yake katika kampeni tambuzi za kifua kikuu na magonjwa yasiyoambukiza katika bustani ya Manispaa ya Iringa hivi karibuni.

Mallya alisema “changamoto kubwa katika kikundi chetu ni watu na wadau wa kutuunga mkono katika kazi tunazofanya za kuibua wahisiwa wa ugonjwa wa kifua kikuu, kuwapeleka kufanyiwa uchunguzi na kuanzishiwa dawa”. 

Alisema kuwa kikundi kinahitaji posho na nauli kwa ili wanakikundi waweze kutembelea maeneo tofauti katika kata 18 za Manispaa ya Iringa. Alisema kuwa Kata 18 ni nyingi na kubwa hivyo kuzifikia zote ni kazi inayohitaji moyo wa kujitoa na malipo kidogo.

Changamoto nyingine aliitaja kuwa ni imani potofu waliyonayo wananchi kuwa ugonjwa wa kifua kikuu unatokana na kurogwa, hivyo matibabu yake kufanyika kwa waganga wa kienyeji. 

Ugonjwa wa kifua kikuu unatibika hospitali tena bure. Katika kuthibitisha hili, kikundi chetu kipo hapa kutoa ushuhuda kwa sababu wanakikundi ni watu waliougua ugonjwa wa kifua kikuu na kupona” alisema Mallya.

Nae mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Iringa, Dr. Tecla Orio alisema kuwa kikundi cha KIKUKI kimekuwa kikifanya kazi nzuri kwa kujitolea katika Manispaa ya Iringa. Alitoa wito kwa wadau wa mapambano dhidi ya Kifua Kikuu kujitokeza na kuunga mkono juhudi hizo ili kikundi kiweze kuwafikia na kuwaibua wagonjwa wengi zaidi na kuanzishiwa tiba.
 
Kikundi cha kudhibiti kifua kikuu mkoa wa Iringa, kilianza mwaka 2011 kikiwa na wanakikundi 23. Kikundi kinatumia njia za ngoma, maigizo na kutoa ushuhuda katika kufikia ujumbe kwa wahusika.
=30=