Wednesday, November 2, 2011

KWANZA JAMII LIPEWE USHIRIKIANO

Serikali Mkoani Iringa imeahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya habari vya Mkoani hapa na nje ya Mkoa ili kuhakikisha uhuru wa upatikanaji habari unashamiri na wananchi wanapata habari zinazohusu maendeleo yao.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma akizundua gazeti la Kwanza Jamii-Iringa  

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma akiongea na mmoja wa wajumbe wa bodi wa gazeti la Kwanza Jamii Maggid Mjengwa

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma wakati akizindua gazeti la Kwanza Jamii-Iringa katika sherehe za uzinduzi zilizofanyika katika uwanja wa shule ya sekondari Mwembetogwa katika Manispaa ya Iringa.

Dk. Ishengoma amesema “ieleweke kuwa serikali imekuwa na ushirikiano mkubwa na mzuri na vyombo vya habari, mara nyingi Mhe. Rais amehimiza ushirikiano huo kwa watendaji wengine, huku akiwataka wananchi kuvitumia vyombo hivyo kwa manufaa ya taifa”.

Aidha, amewataka wananchi wa Mkoa wa Iringa kujitokeza na kutoa ushirikiano wao kwa gazeti hilo kwa manufaa ya maendeleo ya Mkoa wa Iringa. Amewataka kuwa wadau kwa kununua nakala na kutoa matangazo yao ili kulifanya gazeti hilo kuwa endelevu.

Mkuu wa Mkoa amewataka wananchi wa Mkoa wa Iringa, kulitumia gazeti hilo kama jukwaa la kusemea na kuwaunganisha na viongozi wao kwa manufaa ya maendeleo ya wana Iringa.

WALIMU WATOE DARASA LA VVU/UKIMWI

Walimu Mkoani Iringa wameshauriwa kutumia muda wao kuzungumzia masuala ya VVU/UKIMWI na madhala yake katika jamii pindi wanapokuwa wakifundisha katika utaratibu wao wa kawaida ili kuongeza uelewa kwa wanafunzi.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma alipokuwa akiongea na waandishi wa habari wa Mkoa wa Iringa ofisini kwake katika utaratibu wake wa kawaida wa kukutana na waandishi wa habari mara kwa mara na kujadili masuala ya maendeleo na changamoto katika Mkoa.

Dk. Ishengoma amesema “ukimwi ni tatizo sana katika Mkoa wetu wa Iringa hivyo hata kama haupo katika mitala ya elimu lakini ni vizuri kila mwalimu akachukua angalau dakika tano anapoanza au anapomaliza kipindi kuelezea masuala ya UKIMWI”.

Amesema katika kukabiliana na janga hili ni lazima elimu itolewe kwa umakini mkubwa kuanzia darasa la tatu na kuendelea kwa misingi ya kuwaandaa vijana na mapambano hayo.

Akiongelea dawa ya kudumu dhidi ya UKIMWI amesema ipo wazi nayo ni wananchi kubadili tabia sambamba na elimu dhidi ya kujikinga na maambukizi. Amesema kwa wale waaminio basi watumie maandiko matakatifu kama kinga na wale wasioweza kabisa basi zana zitumike, “ila dawa ni wewe mwenyewe kubadili tabia”.

Mkuu wa Mkoa huyo aliwaagiza waandishi wa habari kujikita katika kuandika habari na makala zinazoelezea madhara ya UKIMWI katika jamii ili kuweza kueneza habari hizo na hatimae kuifikishia jamii taarifa sahihi ili kuweza kuinusuru na kuongeza nguvu kazi katika Mkoa na Taifa.  

IRINGA YAPATA MGAO WA VOCHA

Mkoa wa Iringa unatarajia kupata mgao wa jumla ya vocha 693,000 za pembejeo za kilimo kwa mwaka wa fedha 2011/ 2012.

Akiwasilisha mapendekezo ya mgao wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kila Halmashauri kwa msimu wa mwaka 2011/2012 katika kamati ya vocha ya mkoa wa Iringa, Afisa Kilimo Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni ameyataja mapendekezo hayo kwa kila Halmashauri kuwa ni Mufindi (kupandia 44,300, kukuzia 44,300, chotara 44,000, mpunga 300), Makete (kupandia 23,700, kukuzia 23,700, chotara 23,700), Iringa (kupandia 45,000, kukuzia 45,000, chotara 43,500, mpunga 2,500), Njombe Mji (kupandia 21,000, kukuzia 21,000, chotara 21,000), Manispaa (kupandia 4,000, kukuzia 4,000, chotara 4,000), Kilolo (kupandia 26,000, kukuzia 26,000, chotara 25,800, mpunga 200), Njombe (kupandia 42,500, kukuzia 42,500, chotara 42,500) na Ludewa (kupandia 24,500, kukuzia 24,500, chotara 24,000 na mpunga 500).

Akiongelea thamani za vocha moja moja msimu katika msimu wa mwaka 2011/ 2012  Nyoni amesema kuwa vocha za kupandia kilo 50 ni shilingi 28,000, kukuzia kilo 50 ni shilingi 18,500, mahindi chotara kilo 50 ni shilingi 20,000 na mpunga kilo 50 ni shilingi 12,000.

Ili kuhakikisha usimamiaji wa vocha hizo za pembejeo unakuwa madhubuti, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma amewaagiza wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato mzima wa vocha katika wilaya zao. Vilevile, amewaagiza Wakuu hao wa Wilaya kutokuwafumbia macho mawakala wasio na vigezo ili huduma hiyo iweze kufanikiwa na kuwanufaisha wananchi kama yalivyo madhumuni ya Serikali.

Amesema “mfumo huu wa vocha ni mzuri sana ila una mianya ya rushwa hivyo tusichague mawakala matapeli bali  tuchague mawalaka wenye rekodi nzuri na wasio na madeni” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.

KAMATI YA VOCHA NAYO YANYOOSHEWA KIDOLE

Kamati ya vocha ya ruzuku ya pembejeo za kilimo ngazi ya Mkoa wa Iringa imetakiwa kufanya kazi kwa uangalifu mkubwa katika kusimamia menejimenti ya vocha za pembejeo za kilimo ikiwa ni pamoja na mfumo wa uchaguzi wa mawakala unaozingatia vigezo na uwezo.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo ngazi ya mkoa ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma “kamati na kila mmoja ni lazima awe mwangalifu katika kusimamia menejimenti ya ugawaji na usambazaji wa vocha za pembejeo za kilimo ili kuhakikisha zoezi zima linafanikiwa”. Ameongeza kuwa lazima utumike mfumo mzuri na madhubuti wa kuwapata mawakala utakaozingatia vigezo na uwezo wao ili kuondoa ubabaishaji ambao umekuwa ukijitokeza na kusababisha wakulima kutokunufaika na ruzuku hiyo ya serikali wakati mawakala wakiendelea kutajirika kupitia migogo ya wakulima. Amesisitiza kuwa ni vizuri kuwa na mawakala wachache wenye vigezo kuliko kuwa na mawakala wengi wasio na vigezo.     

Akiwakilisha taarifa ya upatikanaji na usambazaji wa vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa mwaka 2010/2011, Afisa Kilimo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni amesema kuwa Mkoa umepokea vocha zenye thamani ya shilingi Bilioni 21.6. Amesema vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo zilizopokelewa na Mkoa ni za kutosha Kaya 336,635 ambazo ni sawa na vocha 1,009,905 kwa ujumla wa nakala moja moja ya vocha.

Akiongelea idadi ya mawakala kwa Mkoa wa Iringa katika kipindi husika, Nyoni amesema kuwa Mkoa ulikuwa na mawakala 514 waliofanya kazi ya kusambaza pembejeo za kilimo. Amesema miongoni mwa mawakala hao mawakala 390 ndio waliofanya kazi ya kusambaza pembejeo katika ngazi ya vijiji na kata kwa utaratibu wa mfumo wa ruzuku ya pembejeo.

Nyoni amesema changamoto kubwa ni malalamiko kutoka kwa wakulima juu ya kuongezeka kwa bei ya mbolea ilikinganishwa na msimu uliopita. Amesema msimu uliopita bei mkulima alichangia shilingi 48,000 hadi 65,000 ikilinganishwa na msimu 2010/2011 aliochangia shilingi 85,000 hadi 90,000 kwa pembejeo za ekari moja yaani mbegu bora, mbolea ya kupandia na kukuzia. 

MA DC WAAGIZWA KUSIMAMIA VOCHA



MKUU wa Mkoa wa Iringa amewaagiza Wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kutokuwafumbia macho mawakala wababaishaji na wanaojinufaisha kupitia migongo ya wakulima ili kuondoa manung’uniko na wakulima kunufaika na mfumo huu wa vocha za ruzuku za serikali.


Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma 
Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa kamati ya vocha za pembejeo ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma katika kikao cha kamati ya vocha za pembejeo mkoa wa Iringa kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.   

Dk. Ishengoma amesema “ili kuhakikisha usimamiaji wa vocha hizo za pembejeo unakuwa madhubuti, ni lazima wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato mzima wa vocha katika wilaya zenu”. Aidha, amewataka Wakuu hao wa Wilaya kutokuwafumbia macho mawakala wasio na vigezo ili huduma hiyo iweze kufanikiwa na kuwanufaisha wananchi kama yalivyo madhumuni ya Serikali.

Amesema “mfumo huu wa vocha ni mzuri sana ila una mianya ya rushwa hivyo tusichague mawakala matapeli bali  tuchague mawalaka wenye rekodi nzuri na wasio na madeni na wasio wababaishaji kwa sababu lengo la serikali ni kumsaidia mkulima kwa kumpunguzia gharama katika pembejeo za kilimo” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.

Aidha, Mkuu wa Mkoa aliagiza kamati ya vocha ya Wilaya na Wataalam wa kilimo kuwaelimisha wakulima juu ya utaratibu wa awali wa kufikisha pembejeo kwa wakulima kulingana na fomu zalizowasilishwa ma Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika.

Akiwasilisha mapendekezo ya mgao wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kila Halmashauri kwa msimu wa mwaka 2011/2012 katika kamati ya vocha ya Mkoa wa Iringa, Afisa Kilimo Mkuu katika Ofisi ya Mkuu Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni ameyataja mapendekezo hayo kwa kila Halmashauri kuwa ni Mufindi (kupandia 44,300, kukuzia 44,300, chotara 44,000, mpunga 300), Makete (kupandia 23,700, kukuzia 23,700, chotara 23,700), Iringa (kupandia 45,000, kukuzia 45,000, chotara 43,500, mpunga 2,500), Njombe Mji (kupandia 21,000, kukuzia 21,000, chotara 21,000), Manispaa (kupandia 4,000, kukuzia 4,000, chotara 4,000), Kilolo (kupandia 26,000, kukuzia 26,000, chotara 25,800, mpunga 200), Njombe (kupandia 42,500, kukuzia 42,500, chotara 42,500) na Ludewa (kupandia 24,500, kukuzia 24,500, chotara 24,000 na mpunga 500).

Akiongelea thamani za vocha moja moja msimu katika msimu wa mwaka 2011/ 2012  Nyoni amesema kuwa vocha za kupandia kilo 50 ni shilingi 28,000, kukuzia kilo 50 ni shilingi 18,500, mahindi chotara kilo 50 ni shilingi 20,000 na mpunga kilo 50 ni shilingi 12,000.

Nyoni amesema kuwa Mkoa unatarajia kupata mgao wa jumla ya vocha 693,000 za pembejeo za kilimo kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

VIJANA PUNGUZENI KASI YA VVU/ UKIMWI


VIJANA mkoani Iringa wametakiwa kuwa wajumbe makini katika kupunguza kasi ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI na kujilinda kwa kutumia mafundisho ya MUNGU kama silaha kubwa katika kujilinda na ugonjwa huo.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma wakati akifunga semina ya siku mbili ya vijana iliyoandaliwa na Kanisa Katoliki Parokia ya Kihesa katika manispaa ya Iringa.

Dk. Ishengoma amesema “mkoa wetu sasa unaongoza kwa maambukizi ya UKIMWI ukiwa na kiasi cha asilimia 15.7 ya maambukizi”. “Naomba kila mmoja wetu awe mjumbe katika kupunguza kasi ya maambukizi haya”. Amesema kwa kufanya hivyo kiasi cha maambukizi kitapungua sana. Aidha, amewasisitiza vijana kujilinda kwa kufuata mafundisho ya Mungu kama silaha kubwa katika kujilinda huko. Akikariri Kitabu cha Waefeso 6:11 “vaeni silaha zote za Mungu mpate kuweza kuzipinga hila za shetani”.

Vilevile, amewaasa vijana wote kujenga tabia ya kushiriki kikamilifu katika michezo mbalimbali kwa malengo ya kuimarisha afya zao, uwezo wa kufikiri na kujipatia ajira.

Amewaomba walimu na viongozi wa dini kuhakikisha vijana wanafanikiwa. Amesema “walimu wa mafundisho ya dini ni nguzo muhimu katika kuhakikisha vijana wanafanikiwa, nawaomba walimu wote na viongozi mbalimbali wa taasisi za dini tutumie nguvu zetu zote kuwapa elimu vijana wetu” alisisitiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Ameshauri kuwa vijana ni taifa linalotegemewa hivyo kwa kutumia karama ya ualimu. Ni vizuri wakatumia tunu hiyo kuufikisha ujumbe wa Mungu kwa vijana na waumini wote. Ameshauri kuendelea kuwafundisha maadili mema ili wafanikiwe katika maisha. Amesema kuwa wapo vijana wakorofi ambao huchangia pia kuharibu nidhamu ya vijana wengine hao wanahitaji mtumie bisara na utu zaidi ili warudi katika nidhamu inayotakiwa.

Akiongelea suala la anami iliyopo nchini, Dk. Ishengoma amesema  “niwakumbushe suala la amani iliyopo nchini kwa sasa”. Watanzania siku zote tunaishi kwa amani na mshikamano mkubwa. Amesema “hivi vyote vimejengwa na waasisi wetu ambao walituunganisha tukawa kitu kimoja”. Amesisitiza kuwa wote kwa pamoja kuimarisha na kudumisha zaidi mshikamano na amani iliyopo ili watanzania waendelee kuishi kwa utulivu na upendo.

Katika mmomonyoko wa maadili, Dk. Ishengoma amesema “katika jamii yetu wote tumeshuhudia mmomonyoko wa maadili, tumeshuhudia vijana wakilewa, wakikosa hekima na busara, dharau, vijana kuvuta na kusafirisha dawa za kulevya”. Amesema mmomonyoko huu unatokana na kutofuata mafundisho ya Mungu. Aidha, aliuomba uongozi wa kanisa kusaidia kwa kadri iwezekanavyo kuwafundisha maadili mema vijana na waumini wao kwa ujumla.

Kanisa Katoliki Parokia ya Kihesa kupitia umoja wa vijana umeandaa semina kwa vijana kwa lengo la kuwaimarisha kimwili na kiroho pamoja na kuwapokea vijana waliohitimu shule ya msingi na kujiunga na umoja huo ili kuweza kuepukana na majanga mbalimbali yanayowakumba vijana kulingana na hali halisi ya utandawazi.