Friday, October 7, 2011

TUMIENI SKIMU YA MWAGILIAJI -RUAHA MBUYUNI



Wananchi wa Kata ya Ruaha Mbuyuni wametakiwa kuitumia skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni kwa shughuli za kilimo ili kujiletea maendeleo ya kiuchumi.

Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati alipofanya ziara ya kukagua shughuli za kilimo katika skimu hiyo ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni iliyopo katika kata ya Ruaha Mbuyuni.

Dkt. Ishengoma amesema “Ruaha Mbuyuni mnalo bonde zuri sana ila halitumiki ipasavyo kwa shughuli za kilimo cha umwagiliaji, lazima hali za wanaruaha mbuyuni zibadilike kutokana nakuinuka baada ya serikali yenu kuwatengenezea mrefeji na banio la maji”. Amesema baada ya kulitembelea bonde hilo na skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni ni dhahili kuwa shuguli za kilimo bado kipo chini sana na kushauri hamasa itolewe kwa wananchi kuitumia skimu hiyo kwa kilimo cha kisasa ili waweze kuvuna zaidi ya mara moja.

Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji wa kijiji cha Ruaha Mbuyuni Afisa Mtendaji wa kijiji hicho, Nassoro Almasi amesema kuwa mwezi Aprili mwaka 2008 mto Lukosi ulihama katika mkondo wake wa asili na kuacha miundombinu ya umwagiliaji ikiwemo banio kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua zilizonyesha ukanda wa juu wa Wilaya ya Kilolo. 

Amesema kuwa madhara ya mvua hizo yalisababisha ekari 500 za mazao ya chakula ambayo ni mahindi, mpunga, maharage, vitunguu, nyanya na mbogamboga kuathirika kwa ukame na kusimamisha shughuli za kilimo.

Skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni ilianza miaka ya sabini baada ya wakulima wenyewe kuchepusha maji kwa kutumia mawe, magogo, matete na majani ili kumwagilia mashamba yao. 


KILOLO DHIDI YA UKAME


Wilaya ya Kilolo imeshauriwa kulima mazao yanayovumilia ukame ili kukabiliana na ukame unaoendelea kuinyemelea wilaya hiyo.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akiongea na wafanyakazi wa Serikali kuu na Halmashauri Wilayani Kilolo alipofanya ziara ya kujitambulisha na kuzifahamu changamoto zinazoikabili Wilaya hiyo.

Dkt. Ishengoma amesema “lazima tutafute mazao yanayostahimili ukame, lazima twende katika kilimo cha mtama”.  Amesema “lazima tumfikirie mwananchi wa Kilolo atapataje chakula cha kutosha, bahati mbaya huwa sipendi sana tabia ya kuomba omba chakula cha msaada sababu si staha kwa mtu mzima”.

Aidha, ameishauri Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kuangalia uwezekano wa kununua mbegu bora za mtama na kuweka utaratibu mzuri ambao watautumia kwa wakulima ili uweze kuwanufaisha. Amesema kwa mujibu wa vituo vya utafiti mbegu bora ya mtama si nyingi sana kwa sababu sehemu nyingi za nchi zimekumbwa na ukame na kusababisha maeneo mengi kulazimika kununua mbegu ya mtama.

Ameushauri uongozi wa Wilaya ya Kilolo kuwashawishi wananchi kununua mbegu bora za mtama na kuzipanda kwa vitendo. 

Mkuu huyo wa Mkoa amesema “tumepata njaa kwa sababu hatutumii kilimo cha umwagiliaji”. Amesisitiza matumizi mazuri ya skimu za umwagiliaji ili kujihakikishia chakula cha kutosha. Kilimo cha umwagiliaji kinamuwezesha mkulima kulima mara mbili hadi tatu kwa mwaka na kujihakikishia uhakika wa chakula.
Akiongelea usindikaji wa mazao amesema kuwa usindikaji huo unaongeza thamani ya mazao husika. 

Amewataka maafisa Mipango kushirikiana na kuandika maandiko ya miradi midogo midogo ili kuweza kuyaongezea mazao thamani. Amesema “ni lazima tuweke mikakati ya kuwainua wananchi, si lazima mpaka wananchi waibue wenyewe sisi wataalamu tunaweza kuwajibika kwa niaba ya wananchi”.