Saturday, February 22, 2014

TATHMINI YA MAZINGIRA KUFANYIKA TENA KABLA YA STENDI YA IGUMBILO



Serikali imelitaka baraza la usimamizi wa mazingira (NEMC) kufanya upya tathmini ya athari za kimazingira katika eneo la Igumbilo inapotarajiwa kujengwa stendi mpya ya mabasi na halmashauri ya Manispaa ya Iringa.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais- Mazingira, Dkt. Binilith Mahenge alipofanya ziara ya kutembelea eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya mabasi mjini Iringa.


Waziri wa Nchi OMR- Mazingira, Dkt. Binilith Mahenge (wa tatu kushoto)
 
Dkt. Mahenge amelitaka baraza la usimamizi wa mazingira kufanya upya tathmini juu ya athari za kimazingira na kuwasilisha taarifa hiko kwake. Kauli hiyo imekuja kutokana na mvutano wa muda mrefu sasa baina ya Manispaa ya Iringa na wadau wa maji kwamba mradi huo itaharibu chanzo pekee ya chaji katika mji wa Iringa. Aidha, Dkt. Mahenge amesema kuwa katika kipindi chote manispaa ya Iringa isifanye shughuli zozote za maendeleo katika eneo hilo.

Waziri wa Nchi OMR amesema kuwa lengo la kutembelea eneo la Igumbilo ni kujionea hali halisi kufuatia hoja zilizotolewa na wadau mbalimbali hasa wa maji kuhusu ujenzi wa stendi hiyo. Amesema kuwa baada ya tathmini hiyo wataalam watamshauri kitaalam kwa mujibu wa taaluma. Amesema kuwa maamuzi ya kitaaluma hayawezi kufanywa kisiasa.

Naibu Meya wa Manispaa ya Iringa, Gervas Ndaki litaka suala hilo lisichukuliwe kisiasa. Amesmea kuwa wapo baadhi ya wafanyabiashara wanaopinga kwa nguvu dhana ya stendi hiyo kuhamishwa mjini na kujengwa eneo la Igumbilo kutokana na maslahi yao ya kibiashara.

Katika taarifa fupi ya mkoa wa iringa iliyowasilsihwa kwa Waziri wa nchi OMR na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu amesema kuwa mradi wa ujenzi wa stendi, unatokana uhitaji mkubwa wa uboreshaji wa miundombinu ya usafiri katika manispaa ya Iringa na mkoa kwa ujumla. Amesema lengo la ujenzi wa stendi mpya ni kuboresha muindombinu ya stendi ndani ya mji kutokana na misongamano mikubwa katikati ya mji na kukosa nafasi ya kupanua stendi. Amesema kuwa halmashauri hiyo kwa kujenga stendi hiyo inakusudia kuongeza kuboresha vyanzo vya mapato na kukuza shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wake.

Akiongelea sheria iliyoanzisha mamlaka za maji, Ayubu amesema kuwa sheria hiyo inazitaka mamlaka kusambaza kwa wananchi maji yaliyo safi na salama. Amesema kuwa ikitokea mamlaka imewasambazia wananchi maji ambayo hayako katika viwango mamlaka itakuwa inakiuka sheria. Amesema kuwa wananchi wa manispaa ya Iringa watakuwa kwenye mazingira hatarishi kwa kunywa maji yenye takakemikali na kupelekea madhara kiafya.
=30=
  

SEKTA YA KILIMO KUAJIRI ZAIDI




Sekta ya kilimo inachangia asilimia kubwa katika maendeleo ya taifa na kuajiri watu wengi zaidi nchini. 

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika kongamano kati ya serikali na wadau kuhusu siku ya kilimo na usalama wa chakula afrika lililofanyika katika kijiji cha Kaning’ombe wilayani Iringa.

 Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la wadau wa kilimo (ANSAF), Audax Rukonge

 Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma aliyemuwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

 Mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (watatu kushoto) aliyemuwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Dkt. Bilal amesema “kama tujuavyo kilimo ni uti wa mgongo kwa uchumi wa taifa letu. Kilimo hutegemewa na watanzania wengi hasa akina mama, na asilimia 75 ya kipato cha watanzania hutokana na kilimo”. Amesema kuwa kilimo kinasaidia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wan chi (GDP). Akiongelea umasikini, amesema kuwa pamoja na ukweli kwamba umasikini bado upo nchini kilimo ni suluhisho la mabadiliko kwa watanzania wengi. Amesema kwa msingi huo ni vizuri dira na malengo yaelekezwe katika kilimo cha kibiashara.

Makamu wa Rais amesema kuwa elimu ya uzalishaji bora wenye tija kwa wakulima wadogo itolewe ili waondokane na umasikini. Amesema kuwa kufanya hivyo uchumi wan chi utazidi kukua na kuongezeka kwa ustawi wa jamii.

Dkt. Bilal amesema kuwa serikali itaendelea na jitihada za kuendeleza na kuimarisha sekta ya kilimo nchini. Amesema program ya kuendeleza sekta ya kilimo ilizinduliwa rasmi mwaka 2005/2006 ambapo malengo makubwa ya program hiyo ni kuhakikisha kilimo kinakua kwa asilimia 6 kwa mwaka. Amesema hadi sasa lengo halijafikiwa sababu ukuaji bado ni asilimia 4 tu.  Amesema malengo ya hayawezi kufikiwa bila kuunganisha nguvu na jitihada za pamoja. Ameseme kupitia mkakati wa kilimo kwanza, serikali inaendelea kusimamia na kutekeleza malengo iliyojiwekea na kwa kuzishirikisha sekta binafsi ili kuleta mafanikio makubwa kwa pamoja.

Akiongelea makubaliano na ahadi za Maputo mwaka 2003, Mkurugenzi Mtendaji wa Jukwaa la wadau wa kilimo (ANSAF), Audax Rukonge amesema kuwa katika kilele cha mkutano wa umoja wan chi za Afrika, AU mwaka 2003 wakuu wan chi walikubaliana kuwa kila nchi itenge kiasi cha asilimia 10 ya bajeti ya kitaifa iingizwe kwenye kilimo.

Amesema kuwa kiwango hicho kilitarajiwa kutosha kuchangia kuongeza uzalishaji na tija, kukuza sekta ya kilimo kwa asilimia 6 kwa mwaka na kuondoa tatizo la njaa na umasikini. Amesema kuwa miaka kumi baadae ni nchi nane tu za Afrika zimetimiza ahadi hiyo na kilimo katika nchi hizo kimekua kwa asilimia 6 na zaidi.

Amesema kuwa unahitajika mtazamo mpya wa kibiashara dhidi ya kilimo tofauti na kisiasa kwa kuwekeza maeneo ya kimkakati na yenye ufanisi mkubwa.

Kongamano hili ni fursa ya kuhakikisha yanapatikana mafanikio katika kilimo kwa kuzikabili changamoto mbalimbali kwa kuzifanyia kazi ili kupata mazao bora yenye tija. Aidha, ni muendelezo wa Kongamano la Umoja wa Bara la Afrika uliozinduliwa na Rais Yayi Boni wa Benini, Mwaka 2012, katika kuendeleza Kilimo na Usalama wa chakula  ili kupata chakula cha uhakika.
=30=


Thursday, February 13, 2014

SHULE BBINAFSI ZAPONGEZWA KUFANYA VIZURI KITAALUMA




Serikali imezipongeza shule zisizo za serikali kwa kufanya vizuri katika matokeo ya kitaifa kwa mitihani ya kuhitimu darasa la saba, kidato cha nne na sita kanda ya Nyasa.
 Gerald G. Guninita,

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Gerald Guninita katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Kalenga mjini Iringa.

Dkt. Ishengoma amesema “niwapongeze sana kwa namna ya pekee kutokana na ukweli kwamba, ninyi mmekuwa ni mfano bora wa malezi ya mtoto wa kike kwani mara nyingi wanafunzi hufanya vizuri kitaifa katika matokeo ya mitihani ya kuhitimu darasa la saba, kidato cha nne na cha sita. Shule zisizo za serikali zinaongoza katika kufanya vizuri”. Amesema kwa matokeo haya inaonesha wazi mmejipanga vizuri kulisaidia taifa kutoa elimu yenye manufaa na tija kwa watanzania.

Amesema mafanikio hayo yanadhihirisha nia njema waliyonayo wamiliki wa shule binafsi katika kulielimisha na kuliendeleza taifa. Amepongeza juhudi za kukutana na kujadili na kupeana uzoefu na kubadilishana mbinu za ufundishaji katika kutoa elimu bora kwa wanafunzi.

Mkuu wa Mkoa amesema kuwa pamoja na kufanya vizuri kwa shule binafsi, zipo zinazofanya vibaya pia kutokana na wanafunzi wengi kutohudhuria masomo kwa kukosa ada, gharama kubwa ya masomo. Sababu nyingine amezitaja kuwa ni uhaba wa walimu kwa baadhi ya masomo, uongozi mbaya na migogoro katika shule pamoja na mambo mengine.

Akiongelea mikakati ya kuboresha elimu itolewayo nchini, amesema kuwa serikali imeamua kufanyia marekebisho sera ya elimu na mafunzo ya ufundi ya mwaka 1995. Amesema kuwa tayari kuna mambo mengi ambayo yamerekebishwa kwa lengo la kuendana na mahitaji ya utoaji wa elimu bora inayopatikana kwa wote.

Aidha, amewashauri kujenga vyuo vya ualimu na vyuo vingine ili kukidhi hitaji kubwa la walimu katika shule zote za serikali na binafsi na wataalamu wengine.
=30=

PICHA ZA UWASILISHAJI WA TAARIFA YA UTEKELEZAJI ILANI YA CCM -MKOA WA SHINYANGA

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe.Ally N.Rufunga akizungumza na waandishi wa Habari katika ukumbi wa mikutano ofisini kwake wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa miezi sita Julai - Juni 2013 na kuhusu kongamano la uwekezaji kanda ya ziwa linalofanyika Mkoani Mwanza kuanzia leo hadi 16 ,kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa Dkt.Anselm Tarimo.





Wakuu wa Sehemu na Vitengo wa Sekretarieti ya Mkoa wa Shinyanga wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa akitoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM Julai - Desemba 2013 kwa waandishi wa Habari


Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga Dkt.Anselm Tarimo akifafanua jambo kwa waandishi wa habari wakati wa mkutano wa kueleza utekelezaji wa Ilani ya CCM na Kongamano la Uwekezaji kanda ya Ziwa

MKOA WA SHINYANGA KUNUFAIKA NA KONGAMANO LA UWEKEZAJI KANDA YA ZIWA



Na. Magdalena Nkulu
 
Mkoa wa Shinyanga ni kati ya mikoa sita ya kanda ya Ziwa inayoshiriki katika kongamano la uwekezaji kanda ya ziwa litakalofanyika jijini Mwanza kuanzia tarehe 13-16 Februari 2014.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe.Ally N.Rufunga ametoa taarifa hiyo Jumanne ya wiki hii katika mkutano na waandishi wa Habari ofisini kwake.

Mhe.Rufunga amesema, kongamano la uwekezaji kanda ya Ziwa ni mkutano ulioandaliwa kwa ajili ya kutangaza fursa za uwekezaji na kuwashawishi wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika mikoa ya kanda ya Ziwa ambayo ni Mwanza,Shinyanga,Mara,Kagera,Geita na Simiyu.

Mkoa wa Shinyanga unashiriki kwenye kongamano hilo kwa sababu ya kutangaza fursa zilizopo katika mkoa ambazo ni

·        Mazingira mazuri yanayofaa kwa utalii na kilimo
·        Hali ya usalama na amani hivyo hali ya matukio ya uhalifu ni ndogo
·        Nguvu kazi ya kutosha
·        Uwepo wa taasisi mbalimbali za Elimu zinazotoa ujuzi tofauti
·        Miundombinu ya usafiri na usafirishaji kutokana na mkoa kuunganishwa na mikoa mingine ndani na nje ya nchi kama Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, na DRC.

Kutokana na kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo mkoani Shinyanga kupitia kongamano hilo,serikali inatarajia mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii.
 Kupitia shughuli mbalimbali za uwekezaji katika viwanda za uzalishaji bidhaa, biashara, vyuo na taasisi wananchi wa mkoa wa Shinyanga na maeneo ya jirani wategemee kupata ajira, wataboresha na kuongeza thamani ya mazao ya mifugo na kilimo ili kuzalisha malighafi na fursa nyingi zitaongezeka.

Tayari mkoa wa Shinyanga imekwisha anza kunufaika na shughuli za uwekezaji wa viwanda ambavyo baadhi ya wawekezaji hasa wa nje ya nchi wamejenga na wameanza uzalishaji kama kiwanda cha ngozi (Ibadakuli),kiwanda cha kutengeneza nyuzi (Nhelegani),kiwanda cha mafuta ya kupikia (Nhelegani) na kiwanda cha mwekezaji mzawa cha Maji na soda cha “Jambo Group of Companies”.

Kongamano hili ni kutokana na mkakati wa serikali wa kukuza uchumi kupitia sekta ya uwekezaji hivyo ni muhimu kutangaza fursa zilizopo ili kuwavutia zaidi wawekezaji kuja katika mkoa wa Shinyanga.

Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Shinyanga

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI TSHS.BILIONI 16 ZATUMIKA KUTEKELEZA ILANI YA CHAMA CHA MAPINDUZI JULAI – DESEMBA 2013





JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

       Ofisi ya Mkuu wa Mkoa,                            
                     S. L. P. 320,
                       Shinyanga

          10 Februari, 2014

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
TSHS.BILIONI 16 ZATUMIKA KUTEKELEZA ILANI YA CHAMA CHA MAPINDUZI JULAI – DESEMBA 2013

Mkoa wa Shinyanga umetumia jumla ya Shilingi 16,097,445,854 kutekeleza miradi ya maendeleo kwa kipindi cha Mwezi  Julai hadi Desemba Mwaka 2013.

Fedha hizo zimetumika katika sekta mbalimbali kama ilivyoainishwa katika maelekezo ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya uchaguzi mkuu na malengo yaliyopangwa kutekelezwa kwa kipindi hicho.

Utekelezaji wa Ilani umezingatia malengo ya Mpango wa Matokeo Makubwa sasa na malengo ya maendeleo ya milenia hadi ifikapo 2015.

Katika kipindi cha nusu ya mwaka 2013/2014, mafanikio makubwa yamepatikana katika sekta za Elimu,Afya,Maji,Kilimo,Miundombinu, Mapato ya Ndani ,Mifugo n.k. kama ifuatavyo:-

Mapato ya ndani
Hadi kufikia Desemba 2013 mkoa umekusanya mapato ya ndani kiasi cha Sh. 5,983,590,960 sawa na asilimia 47.3 ya Lengo kwani Mkoa umejiwekea Lengo la kukusanya kiasi cha Sh.11,356,021,186 kwa mwaka wa Fedha 2013/14.

Elimu
Kwa kipindi cha miezi sita,upande wa Elimu ya msingi,serikali imefanikiwa kuongeza madawati 1692, kusambaza vitabu 157,051 katika shule zote, kujenga nyumba za walimu 31 kujenga matundu ya vyoo 136 na madarasa 38 kwa Tshs 2,991,101,190 sawa na ongezeko la asilimia 40 ya mwaka jana 2012/2013. 

Aidha, madawati 459 kwa ajili ya madarasa ya awali yametengenezwa na ununuzi bado unaendelea,vilevile jumla ya watoto 3070 wenye ulemavu walimbuliwa na kuandikishwa katika Elimu ya Msingi.

Katika Elimu ya sekondari,Mkoa umetumia jumla ya Tshs. 1,348,013,030 kusambaza madawati, kujenga vyumba14 vya maabara na vifaa vya maabara hizo, kujenga maktaba na kununua vitabu 2975, kujenga nyumba za walimu 4, kujenga madarasa 17 na vyoo matundu 23.

Afya
Katika sekta ya Afya serikali imetumia kiasi cha Tsh.3,464,084,797 katika kuajiri watumishi 145 wa kada mbalimbali,kukarabati vituo vya Afya15,nyumba 11 za watumishi wa sekta ya Afya, ujenzi wa zahanati 40 unaendelea,ununuzi wa vifaa tiba,ujenzi wa hospitali ya wilaya unaoendelea, ununuzi wa gari moja la wagonjwa,usafirishaji wa wagonjwa 520 kwenda hospitali za rufaa, ujenzi wa jengo la OPD  na kufanya matengenezo ya magari yanayotumika kwa ajili ya ufuatiliaji na usimamizi wa huduma za Afya.

Maji
Tshs. 6,064,397,831 zimetumika katika kuboresha sekta ya maji kwa shughuli zifuatazo:- kujenga miradi ya maji ya visima virefu 17 ikiwa ni pamoja na kutandika mabomba na kufunga pampu za mikono kwenye visima virefu, mafunzo mbalimbali yamefanyika na vikundi vya maji 19 vilivyoundwa na kaya 115 kuhusu uvunaji wa maji ya mvua. 

Aidha vituo 42 vya kuchotea maji vimejengwa, mabirika 67 ya kunyweshea ng’ombe yamejengwa, visima vifupi 15 vimechimbwa sambamba na uchambaji wa mitaro ya kulaza mabomba.

Serikali ipo katika mchakato wa kupeleka huduma ya maji katika wilaya ya Kishapu kutoka bomba kuu la maji ya Ziwa Viktoria.Tayari michoro ya kupeleka maji imekamilika na kazi inayoendelea sasa ni kupata mkopo kwenye taasisi za fedha na pia kushirikiana na mgodi wa Almasi wa Mwadui.

Kilimo
Kiasi cha Tshs.1,557,687,000 zimetumika kufanikisha mapinduzi ya kilimo ikilinganishwa na tshs.907,664,635 zilizotumika mwaka 2012/2013 sawa na ongezeko la asilimia 58 ikilinganishwa na kipindi cha Januari hadi Juni 2013.Shughuli zilizofanyika katika kipindi hiki ni pamoja na ufuatiliaji wa mashamba darasa ya wakulima, ujenzi wa vituo vya rasilimali za kilimo, kuanzisha mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora, kuongeza upatikanaji wa pembejeo, kununua vikatuzi nguvu yaani Power Tillers” 6, jumla ya vocha 8441 zimsambazwa, mbegu bora za mtama aina ya Macia zimesambazwa tani 12.7,kata 20 zimehamasishwa kulima mazao yanayostamili ukame,vyama vitatu vya SACCOS vimepewa mafunzo na zana za kilimo na ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji.

Ufugaji
Katika sekta ya ufugaji zimetumika shilingi 148,530,310 kutoa mafunzo ya ugani kwa wafugaji 3431,kujenga malambo matatu,na jumla ya mifugo 33,686 imepatiwa chanjo. Aidha, vikundi 38 vya wafugaji vimeundwa kufikia Desemba 2013.

Wanyamapori na Misitu
Tsh.4,656,000 zimetumika kuunda vikundi 7 vya mtandao wa ushirika wa ufugaji wa nyuki,mikutano ya hamasa juu ya kufuga kwa kutumia mizinga ya nyuki ya kisasa imefanyika katika kata 24, kuandaa na kutoa mizinga ya kisasa 1641 kwa ajili ya kujifunzia, kuendeleza msukumo katika ufugaji wa nyuki na kutoa Elimu kwa wafugaji nyuki.

Mkoa unaendelea na juhudi za kulinda na kuhifadhi mazingira ikiwa ni pamoja na kutunza vyanzo vya maji. Jumla ya miti 126,000 imeoteshwa na kupandwa na watu binafsi na shule za msingi.

Miundombinu
Kwa kipindi cha miezi sita,serikali imetumia shilingi 1,126,973,000 kufanya shughuli za kutoa hatimiliki za kimila na ugawaji wa ardhi.Matengenezo ya kawaida ya barabara katika sehemu korofi jumla ya km 539.52, usanifu wa ujenzi wa kiwango cha lamo wa km 15,uchimbaji wa mitaro ya maji ya mvua yenye ukubwa wa ujazo wa(cubic meter) 6100 matengenezo makalavati jumla ya mistari 21.

Aidha, uwanja wa ndege wa Ibadakuli upo kwenye mchakato wa kuboreshwa kwa kiwango cha lami kwenye njia ya ndege,kujenga ghorofa moja la abiria na maegesho ya magari madogo. Ujenzi huo utagharimu shilingi Bilioni 17 na tayari zabuni ya kumpata Mhandisi mshauri imetangazwa.

Utawala Bora
Ili kudumisha utawala bora wenye kufuata misingi ya haki na usawa, kiasi cha shilingi 197,045,196 zimetumika kuendesha vikao vya kamati za maendeleo ya kata, mabaraza ya wafanyakazi na mabaraza ya madiwani.

Ulinzi na Usalama
Hali ya ulinzi na usalama katika mkoa ni ya kurdhisha tofauti na kipindi cha nyuma kwani matukio makubwa ya uhalifu yamepungua,kwa kipindi cha Julai-Desemba,2013 mauaji ya Albino na yale yanayohusishwa na ushirikina yamepungua kwa asilimia 99 ikilinganishwa na asilimia 95 ya kipindi kilichopita.

Mkoa umewaelekeza Wakurugenzi wa Halmashauri kutenga fedha kwenye bajeti ya 2014/14 kwa ajili ya mgambo na ujenzi wa vituo vya polisi na Mahakama katika maeneo yao ya utawala ili kuimarisha haki, ulinzi na usalama.

Kuendeleza makundi maalum ya Wanawake,Watoto,Vijana na Walemavu

Katika kudumisha shughuli na ustawi wa makundi maalumu, shilingi 102,738,000 zimetumika kuimarisha mifuko ya uwezeshaji wa wanawake na kuhamasisha vyama vya kuweka na kukopa(SACCOS na VICOBA),vikundi 12 vya wanawake vimeelimishwa,vikundi 75 vimesajiliwa na kupewa mafunzo ya kuimarisha mifuko ya mikopo,vikundi 20 vya wanawake wajasiriamali vimewezeshwa kwa mikopo na kurejesha mikopo hiyo. 

Vilevile, Mkoa umesimamia Halmashauri kutoa michango ya asilimia 5 kwenye mfuko wa maendeleo ya wanawake.

Aidha, mkoa umefanya juhudi kubwa katika kuhakikisha kwamba haki za watoto zinasimamiwa ipasavyo kwa kutoa Elimu katika vijiji 32 kwa kushirikiana na mashirika ya Save the Children, AMREF na UMATI / JOICEF.

Vikundi 12 vya vijana wajasiriamali na ushirika wa kuweka na kukopa yaani SACCOS na VIKOBA vimeanzishwa na usimamizi wa matumizi ya fedha za maendeleo ya vijana umeimarishwa ili kuwanufaisha vijana wengi zaidi,na kuhakikisha asilimia 5 ya mfuko wa vijana inatengwa.

Kwa upande wa walemavu jumla ya shilingi 4,120,000 zimetumika kuwaendeleza pamoja na kuwaandikisha watoto wenye ulemavu na wenye uhitaji maalum. Watoto 3,070 wenye mahitaji maalum wametambuliwa na kuandikishwa darasa la kwanza.

Elimu ya ujasiriamali imetolewa kwenye vikundi 6 vya watu wenye ulemavu,pia walemavu wamewezeshwa katika maadhimisho ya sherehe zao za siku ya fimbo nyeupe, siku ya walemavu duniani na siku ya Albino.

Viwanda
Mkoa unaendelea na juhudi za kuendeleza viwanda pamoja na kutangaza fursa za uwekezaji nje na ndani ya nchi yetu.Hadi Desemba 2013 hali halisi ya viwanda ilikuwa kama ifuatavyo:-
§  Kiwanda cha ngozi cha Xinghua Investment Co.Ltd kilikuwa kimekamilika hivyo mwekezaji alikuwa anatarajia kujaribu mitambo mwezi Januari 2014, kabla ya kuanza uzalishaji na mwezi huu Februari kimeanza uzalishaji.
§  Kiwanda cha nyama cha Xinghua Investment kinatarajiwa kukamilika mwezi Juni mwaka huu 2014.
§  Mwekezaji Dahong Cotton Product Limited amekamilisha kiwanda cha kuchambua nyuzi za pamba klichopo Nhelegani.
§  Kiwanda cha kukamua mafuta ya kupikia ya pamba cha Jielong Holding (T)Ltd kilichopo Nhelegani pia kimekamilika.

Serikali ya mkoa wa Shinyanga inazidi kuwahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na viongozi wao kuanzia ngazi za vijiji na mitaa,kata,tarafa na wilaya katika kuibua na kutatua changamoto zinazowakabili kwenye maeneo yao, na changamoto zinazohitaji ushauri wa ngazi ya mkoa zifike na zitaendelea kushugulikiwa.

Imetolewa na
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Shinyanga