Tuesday, September 25, 2012

IRINGA TUMIENI FURSA YA UTALII




Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amewataka wananchi wa mkoa huo kutumia fursa ya maadhimisho ya siku ya utalii duniani yanayofanyika kimkoa katika manispaa ya Iringa kutembelea maonesho hayo na kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo ili kuweza kupata elimu na taarifa z utalii.

Wito huo ameutoa katika hotuba yake ya ufunguzi wa maadhimisho ya siku ya utalii duniani yanayofanyika kimkoa katika uwanja wa Samora, Manispaa ya Iringa.   
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (wa kwanza kulia) akiwa katika moja ya mapango ya kihistoria katika kuhamasisha utalii wa ndani.

Dkt. Christine amesema “natoa wito kwa wananchi wote kutumia fursa hii kutembelea maonesho na kushiriki  katika shughuli mbalimbali za maadhimisho haya”.

Amesema maonesho hayo yatatoa fursa ya kufahamiana na kupanua wigo wa kufanya biashara za utalii. Amesema kuwa maadhimisho yatahusisha maonesho ya bidhaa na shughuli mbalimbali za kitalii, michezo, kutembelea vivutio vya kitalii vilivyopo mkoani Iringa na kutoa elimu kuhusu uendeshaji wa biashara za utalii.

Akielezea madhumuni ya maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa madhumuni ya maadhimisho hayo ni Kutoa umuhimu wa sekta ya utalii kwa maendeleo ya mwanadamu katika nyanja mbalimbali. Amezitaja nyanza hizo kuwa ni pamoja na utamaduni, uchumi, mazingira pamoja na nyingine.

Dkt. Christine amesema kuwa matokeo ya maadhimisho hayo hayawezi kuonekana kwa muda mfupi kwa sababu ni suala linalohitaji hamasa ya muda mrefu. Ameelezea matumaini yake kuwa Mkoa wa Iringa utazidi kuendeleza kwa kasi iliyopo, ukuaji wa utalii na hatimae wananchi kunufaika na utalii huo.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa mkoa wake umejaaliwa kuwa na vivutio Vinci vya utalii ambavyo bado havijafahamika sana kwa wananchi na wadau wengine. Amevitaja vivutio vilivyopo kuwa ni pamoja na mila na desturi za watu wa ukanda huo, maeneo ya hifadhi za mimea na wanyama, mandhari nzuri na za kuvutia, maeneo ya kilimo, maporomoko ya maji na maeneo ya kihistoria.

Nae mwenyekiti wa Kamati ya kuendeleza utalii kwa mkoa wa Iringa ambae pia ni katibu Tawala msaidizi, Sehemu ya Uchumi na Sekta za Uzalishaji, Adam Swai amesema kuwa malengo mahususi ya kufanya maadhimisho katika manispaa ya Iringa ni kuhamasisha wadau mbalimbali kutambua umuhimu wa sekta ya utalii katika kujiletea maendeleo. Ameyataja maadhimisho hayo kuwa ni chachu ya kuendeleza sekta ya utalii katika ukanda wa Kusini ili wananchi waweze kufaidika na utalii huo.

Ikumbukwe kuwa Mkoa wa Iringa ulitangazwa na serikali kuwa kutovu cha kuendeleza utalii kwa Ukanda wa kusini mwaka 2009. aidha, maadhimisho hayo yatafanyika kwa siku tatu, kuanzia tarehe 25 hadi 27 Septemba 2012.
=30=