Friday, November 18, 2016

WATAALAM IRINGA WATAKIWA KUBUNI JINSI YA KUWASAIDIA WANUFAIKA WA TASAF


Na. Mwandishi Maalumu, Iringa
Wataalam mkoani hapa wametakiwa kujikita katika kutafuta mbinu za kuwasaidia wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya masikini Tasaf III ili wajikwamue katika lindi la umasikini.

Agizo hilo lilitolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akifungua kikao kazi cha wataalam wa wilaya na mkoa wa Iringa cha kupanga mikakati ya jinsi ya kuzisaidia kaya masikini zinazonufaika na ruzuku ya Tasaf kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Bonde la Rufiji mjini Iringa.

Ayubu alisema “lengo la kikao kazi hiki ni kuwashirikisha ninyi wataalam wa sekta za afya, elimu, kilimo, mifugo, maendeleo ya jamii na ushirika ambazo kwa kiasi kikubwa zimeguswa na walengwa wa mpango huu wa Tasaf. Mnafahamu kuwa walengwa wengi wa Tasaf wapo vijijini na wameanzisha miradi midogomidogo ya ufugaji wa kuku, bata, simbilisi, nguruwe, mbuzi na kondoo. 

Aidha, wengine wanaboresha makazi yao, wote hawa wanahitaji msaada na ushauri wa kitaalam na ufuatiliaji wa karibu”. Aliongeza kuwa wataalam wa serikali wanawajibu wa kuwasaidia na kuwaelekeza wanufaika hao kuweza kufikia malengo yao. Aliwataka kuona kuwa kuwasaidia wanufaika hao ni jukumu lao na kuwataka kuweka katika mpango kazi wao na ratiba ya kazi ya kila mwezi.

Akiongelea wanufaika wanaopata ruzuku yenye masharti ya elimu na afya, Katibu Tawala Mkoa aliwataka kuwasimamia walengwa ili watimize masharti hayo. “Mfano, upande wa afya mlengwa atapata ruzuku kama ametimiza sharti la kupeleka mtoto kliniki aliye chini ya umri wa miaka mitano. Kwa upande wa elimu mlengwa atapata ruzuku kama atahakikisha mtoto wake anahudhuria shuleni siyo chini ya asilimia 80 ya mahudhurio yanayohitajika” alisisitiza Ayubu. Ni jukumu la kikao kazi hiki kujadili na kupanga namna bora ya kufanya ufuatiliaji wa karibu na kutoa ushauri kwa walengwa ili malengo ya serikali ya kupunguza umasikini yaweze kutimia. 

Awali Mratibu wa Tasaf Mkoa wa Iringa, William Kingazi alimtaarifu Katibu Tawala Mkoa kuwa mkoa wa Iringa ulipata fedha kupitia mpango wa Tasaf III kwa ajili ya kuziwezesha kaya masikini sana ili ziweze kujikimu. Mpango huo ulianza mwezi Januari, 2015 ambapo kaya 26,321 zilitambuliwa kuwa masikini sana. Hadi kufikia mwezi Septemba, 2016 mkoa ulipokea shilingi 6,525,080,001.
=30=

HOSPITALI YA RUFAA IRINGA YAVUKA LENGO UPIMAJI SUKARI


Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa IRINGA
Kliniki maalumu ya kupima ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu mkoani Iringa imevuka lengo kwa kufanikiwa kupima wananchi zaidi ya 2,000.

Kauli hiyo ilitolewa na Mganga mkuu wa mkoa wa Iringa Dkt Robert Salim alipokuwa akiongea na waandishi wa habari katika hitimisho la siku tano za kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya bustani ya Manispaa mjini Iringa.

Dkt. Salim alisema “kliniki ya kupima ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu imefanikiwa kwa kiasi kikubwa. Tumefanikiwa kuwapima wananchi 2,007 na kuvuka lengo letu la kuwapima wananchi 2,000, hivyo lengo limefikiwa kwa asilimia 100.35”. Alisema kuwa mafanikio haya yanatokana na utayari wa wananchi wa mkoa wa Iringa kujitokeza kupima afya zao pindi fursa zinapojitokeza za upimaji zinapojitokeza.

Mganga mkuu wa mkoa aliwataka waratibu wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza katika halmashauri kuanzisha kliniki za magonjwa yasiyo ya kuambukiza katika halmashauri zao na kutoa huduma za mkoba. Aidha, liwataka kufikiria kuanzisha utaratibu wa kuwapima watumishi katika taasisi mbalimbali ili kuwapa fursa ya kunufaika na huduma za afya kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
Dkt Salim aliwatka wananchi wa mkoa wa Iringa kujikita katika kufanya mazoezi kama kutembea na kukimbia ili kujikinga na kisukari. Rai nyingine alitoa kuwa wananchi kuacha tabia ya kula vyakula vyenye mafuta, kupunguza unywaji wa pombe kupita kiasi na uvutaji wa sigara.
Akiongelea ufanisi wa kliniki hiyo, Dtk Tatu Mbotoni wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa alisema kuwa kliniki hiyo ilifanikiwa kutokana na timu yake ya wataalam kujipanga vizuri kuwahudumia wananchi wote waliojitokeza kwa muda. “Tulipanga timu ya wataalam wa kutosha kutoka hospitali ya rufaa ya mkoa na hospitali ya manispaa Frelimo.

Lengo la kuandaa wataalam wengi ni kuhakikisha kila mwananchi anayehudhuria anahudumiwa haraka sana ili aweze kuendelea na mjukumu yake tukizingatia matakwa ya serikali ya awamu ya tano ya hapa kazi tu’’ alisema Dkt Mbotoni.

Nae Elimina Sanga aliyefika katika kliniki hiyo, alisema ameridhishwa na huduma alizopata na kuomba kliniki hiyo iwe endelevu badala ya kusubiri kwenye maadhimisho ya siku ya kisukari duniani.
=30=  
 

MAKAMPUNI YA ULINZI YATAKIWA KUTUMIA WASTAAFU WA MAJESHI YA ULINZI


Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Makampuni ya ulinzi mkoani Iringa yametakiwa kuwatumia askari wastaafu kutoka majeshi ya ulinzi kwa mujibu wa sheria ili kunufaika na ujuzi walionao na kuimarisha usalama wa nchi.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa chama cha makampuni binafsi ya ulinzi mkoa wa Iringa (TSIA) kilichofanyika katika bwalo la Polisi mjini Iringa jana.

Masenza alisema “wito  wangu  kwenu  ni  kwamba  hakikisheni wasimamizi wa makampuni ya ulinzi wanakuwa wastaafu kutoka majeshi ya ulinzi kwa mujibu wa sheria. Wastaafu hawa wanauzoefu na ujuzi katika kusimamia masuala yote ya kiulinzi na usalama”. Aliongeza kuwa wastaafu hao wanauwezo wa kudhibiti nidhamu na kufundisha maadili mema kwa walinzi. 

Alisema kuwa walinzi wengi katika makampuni hayo wanakabiliwa na tatizo la nidhamu na maadili hivyo kuwatumia askari wastaafu kutawasaidia kuimarisha nidhamu na maadili kwa walinzi wa makampuni hayo.

Mkuu wa mkoa wa Iringa alipongeza juhudi zinazofanywa na makampuni ya ulinzi mkoani hapa. Alisema “mimi binafsi nichukue nafasi hii kutambua juhudi mbalimbali zinazofanywa na makampuni ya ulinzi katika kuimarisha hali ya amani miongoni mwa jamii na taasisi mbalimbali. Makampuni ya ulinzi yana mchango mkubwa katika kulinda mali za raia wa Tanzania. Pasingekuwepo makampuni haya vyombo vyetu vya ulinzi haviwezi kulinda peke yao kwa kuwa watanzania ni wengi na askari ni wachache lakini pia mali za watanzania ni nyingi na ukizingatia wahalifu wanaongezeka na kubuni mbinu mpya kila kukicha”

Mkuu wa mkoa wa Iringa ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya usalama ya mkoa aliagiza makampuni yote ya ulinzi mkoani Iringa kuhakikisha walinzi wake wote wanapitia mafunzo ya JKT au mgambo. “Walinzi wanapaswa kupitia mafunzo ya JKT au mgambo. Mafunzo haya huwajengea uwezo wa kupambana na majambazi, kuzuia matendo ya kihalifu na kulitumikia Taifa kizalendo” alisisiza mkuu wa mkoa. 

Awali afisa upelelezi mkoa wa Iringa, Deusdedit Kasindo waliwakumbusha wamiliki wa makampuni ya ulinzi kuwa ni wabia wa jeshi la Polisi kwa sababu wanafanya kazi zinazofanana za kulinda raia na mali zao. Alisisitiza kuwa viongozi wa makampuni hayo wanatakiwa kuwa na taaluma ya ulinzi na walinzi wao wanatakiwa kuwa na taaluma ya ulinzi.
Kasindo aliwakumbusha wamiliki wa makampuni ya ulinzi kuwa wanatakiwa kuwa na silaha mbili angalau tofauti na maeneo mengi ambayo walinzi wanakuwa na silaha moja jambo ambalo ni rahisi kuvamiwa. Aliwakumbusha kuwa kuazima silaha ni kosa kisheria. Aidha, aliwataka wamiliki wa makumpuni hayo kuhakikisha walinzi wao wanajua kutumia silaha kikamilifu.
=30=

MGAMBO IRINGA WATAKIWA KUWA WAZALENDO


Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mshauri wa Mgambo Mkoa wa Iringa ametakiwa kusimamia zoezi la medani la komaza 2016 ili kuchochea kuwaandaa vizuri vijana kuwa wazalendo kwa nchi yao.

Agizo hilo lilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua zoezi la medani komaza 2016 lililofanyika Manispaa ya Iringa.

Masenza alisema “askari hufanya mambo mengi hususani misako na doria, kupambana na majambazi, kuzuia dawa za kulevya na wahamiaji haramu na kuilinda nchi”. Aliongeza “juhudi hizo zinathibitisha kwamba jeshi la mgambo linaumuhimu mkubwa kwa maendeleo ya Taifa letu, hivyo zoezi la medani komaza 2016 liwe kichocheo kikubwa cha kuwaandaa vijana wetu kuwa askari wazuri, wazalendo, waadilifu, watenda haki, jasiri na wenye dhamira ya uaskari”.

Aliwataka wanamgambo hao kuhakikisha mafunzo watakayopewa yanatekelezwa kwa vitendo. Aliongeza kuwa askari wanaoandaliwa wawe mfano wa kuigwa katika jamii inayowazunguka. Alisema kuwa wanamgambo wengine wakipata mafunzo, huonesha ubabe kwa jamii bila sababu ya msingi. “Sisi tusifanye hivyo, mafunzo haya yatupe nidhamu ya kuwaheshimu wananchi wanaotuzunguka na kuwasaidia” alisisitiza Masenza.

Mkuu wa mkoa alipongeza juhudi za mshauri wa mgambo mkoa wa Iringa za kuwaandaa vijana wanaoshiriki mafunzo ya mgambo kuwa wakakamavu kiaskari ambao wako tayari kuilinda nchi yao na kupambana na uhalifu wa aina yoyote katika mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla.