Friday, March 16, 2012

TANZANIA YABORESHA HUDUMA ZA MAJI

Na.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikiboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ukiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji na kuboresha upatikanaji wa huduma za maji safi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji.

Akiongea wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji kitaifa mkoani Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, aliyemuwakilisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika amesema kuwa “Serikali kupitia Dira ya Maendeleo ya Taifa, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini -MKUKUTA, na mabadiliko mbalimbali ya kisera na kimfumo, imekuwa ikitekeleza mipango mbalimbali ya kuboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii ikiwemo mpango wa kuboresha usimamizi na rasilimali za maji, kuboresha upatikanaji wa huduma za majisafi, usafi wa mazingira na maji kwa ajili ya umwagiliaji”.

Amesema kuwa kwa sasa Serikaili inatekeleza mpango wa pamoja wa matumizi ya rasilimali za maji kupitia ofisi zote tisa za mabonde nchini. Amesema pindi mpango huo utakapokamilika utaainisha njia za matumizi bora ya rasilimali maji.

Amesema “katika kuhakikisha rasilimali ya maji inatumika kwa manufaa ya taifa na usalama wa chakula nchini unakuwepo, ninawaomba viongozi wenzangu, vyombo vinavyosimamia rasilimali maji kama vile Mamlaka za Maji, Ofisi za Maji za Mabonde, Vyombo vya Watumiaji Maji na wananchi kwa ujumla kujiandaa kuzikabili changamoto na vihatarishi nilivyotaja”.

Ameitaka jamii kushirikiana katika kuhifadhi, kutunza na kuendeleza mfumo mzima wa maji kuanzia kwenye vyanzo, uzalishaji na ugawaji kwa kuzingatia ongezeko la matumizi ya maji.

Mkoa wa Iringa ni mwenyeji wa maadhimisho ya 24 ya wiki ya maji kitaifa yanayoongozwa na kauli mbiu isemayo ‘maji kwa usalama wa chakula’, shughuli mbalimbali za sekta ya maji pamoja na maonesho zitafanyika katika uwanja wa Samora na maeneo mengine.
=30=

MAAFISA KILIMO WATAKIWA KUFANYA MABADILIKO

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika amewataka maafisa kilimo na wadau wa sekta hiyo kufanya mabadiliko makubwa katika kukuza sekta hiyo ili iwe ya kisasa na kuifanya iwanufaishe wananchi wengi zaidi.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Prof. Jumanne Maghembe, wakati akifungua mkutano wa maafisa kilimo wa Tanzania bara, uliofanyika katika hoteli ya royal village, katika Manispaa ya Dodoma.

Prof. Maghembe amesema kuwa asilimia 77.5 ya wananchi wanaokadiriwa kufika mil. 40 wanategemea sekta ya kilimo katika kuendeleza maisha yao na kati yao asilimia 22.5 ndiyo wanaofanya kazi katika sekta hiyo.

Amesema pamoja na ukubwa wa asilimia ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo  bado kilimo kinachangia asilimia 34 tu ya fedha za kigeni nchini. Katika mchango wa kilimo katika pato la taifa, kinachangia asilimia 24 pekee. Amesema “bado kazi inatakiwa kufanywa na sisi tuliomo humu ndani, tumeandaliwa vizuri kitaaluma ili tuweze kutekeleza hili, kushindwa tunaliangusha taifa”.    

Prof. Maghembe amesema kuwa kilimo nchini kinakua kwa asilimia 4.2 tofauti na lengo la kitaifa la kilimo kukua kwa angalau asilimia 6 kwa mwaka.

Pamoja na kuhimiza kilimo cha umwagiliaji, Waziri wa kilimo, Chakula na Ushirika amesema “suala si kuongeza maeneo ya kulima, bali ni kuongeza uzalishaji katika maeneo tunayolima”.

Akiongelea vikwazo vinavyoikabili sekta ya kilimo, amesema kuwa masoko yasiyo ya uhakika dunia na kuwataka wadau hao kujipanga katika kukuza kilimo ili kiweze kuzinufaisha nchi zenye upungufu wa chakula na kuzifanya zisifikirie kununua chakula sehemu nyingine zaidi ya Tanzania.

Akichangia katika mkutano huo huku akisikilizwa kwa umakini mkubwa na mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma amesema kuwa nchi haiwezi kuwa na mafanikio katika sekta ya kilimo bila kuendeleza kilimo cha umwagiliaji. Amesema ni vema juhudi zikawekwa katika kufufua kilimo cha umwagiliani pamoja na kuimarisha skimu za umwagiliaji ili kilimo kiweze kushamiri.

Akichangia katika upatikanaji wa soko, Dk. Ishengoma amesema kuwa soko ni changamoto kuwa kwa kufanikisha shughuli za kilimo. Amesema ukitangaza uhakika wa soko la mazao mapema wakulima watalima kwa nguvu kwa sababu watakuwa na uhakika na soko. Akitolea mfano katika mkoa wake wa Iringa, amesema kuwa mkoa huo umehimiza kilimo cha zao la mtama kwa wingi ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa chakula, muitikio umekuwa mzuri baada ya kuwa na uhakika wa soko.

Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni upungufu wa fedha za ufuatiliaji, hatua inayowakwamisha wataalamu wa kilimo katika kutekeleza majukumu yao katika sekta ya kilimo.
=30=