Monday, April 15, 2013

AGA KHAN YATOA HUDUMA KWA KAMBI


Kituo cha Afya cha Aga Khan Iringa kwa kushirikiana na Serikali kimetoa huduma za afya ya mama mjamzito na mtoto katika wilaya ya Mufindi na kufanikiwa kuwahudumia wananchi wengi kwa wakati mmoja.

Katika mahojiano na Mratibu wa Mradi wa Tuunganishe Mikono Pamoja nchini, Narmin Adatia katika kituo cha afya cha Ihongole amesema “lengo la kuweka kambi katika kituo cha afya cha Ihongole ni kuhakikisha tunawafikia wananchi wengi zaidi kwa wakati mmoja na kuhakikisha wananchi wananufaika na huduma ya afya ya mama mjamzito na mtoto”. Amesema tumeamua kuweka mguvu zaidi kwa wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano kwa sababu kundi hilo linahitaji huduma bora na salama zinazopatikana kwa urahisi na ukaribu katika maeneo yao. Amesema kufanya hivyo kunasaidia kufikia malengo ya Milenia katika kupunguza vifo vya wanawake wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Akiongelea ushirikiano baina ya Serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na sekta binafsi, Narmin amesifu ushirikiano huo unaogusa ngazi zote za Serikali. Ameishukuru Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi kupitia Ofisi ya Mganga Mkuu wa wilaya kwa kuwachagulia eneo kwa ajili ya kuweka kambi wilayani hapo ili kuwafikia wananchi wengi zaidi wilayani Mufindi katika kituo cha Afya cha Ihongole.

Nae Diwani wa Kata ya Boma, Raphael Makomba amesema kuwa hilo ni jambo jema lililolenga kuwahudumia wananchi wengi zaidi kwa wakati mmoja. Amepongeza jitihada za kituo cha afya cha Aga Khan kupitia mradi wake wa Tuunganishe Mikono Pamoja kwa kushirikiana na Serikali ya Wilaya ya Mufindi kuamua kupeleka huduma hiyo katika Kata ya Boma. Ametumia fursa hiyo kuomba huduma hiyo iwe endelevu ili kuendelea kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa wakati mmoja.

Morris Mwingila, mama mjamzito aliyekwenda katika kambi hiyo
kwa ajili ya kupata huduma ya afya amesifia huduma hiyo na kusema kuwa watoa huduma walikuwa wamejipanga kikamilifu kuwahudumia wananchi kwa haraka na ubora. “Nilitarajia kuwa watu tutakaa muda mrefu katika mistari tukisubiri huduma lakini imekuwa tofauti, watoa huduma wamekuwa wakitoa huduma kwa haraka sana” alisisitiza Morris.

Huduma ya Afya kwa Mama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano imetolewa bure na kituo cha Aga Khan Iringa katika kituo cha afya cha Ihongole kwa kushirikiana na Wilaya ya Mufindi ikiwa ni muendelezo wa huduma hizo chini ya mradi wa Tuunganishe Mikono Pamoja. Huduma zilizotolewa ni pamoja na uchunguzi wa saratani ya shingo ya kizazi, unasihi, uzazi wa mpango, upimaji wa CD4 na magonjwa mengine mengi.
=30=