Tuesday, August 21, 2012

OLE WAO WATAKAOVURUGA SENSA IRINGA!


Serikalili Mkoani Iringa imesema kuwa haitamvumilia mtu wala kikundi chochote kitakachojitokeza na kutaka kuvuruga ama kuharibu zoezi la Sensa ya Watu na Makazi linalotarajia kuanza nchini kote Agosti, 26, mwaka huu.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma katika moja ya mikutano yake ya hadhara katika kuhamasisha wananchi kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi uliofanyika katika kijiji cha Ilambilole, katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa.

Dkt. Christine amesema kuwa kila mwananchi anayo haki ya kuhesabiwa, tena kuhesabiwa mara moja. Amesema “asitokee mtu wala kikundi cha watu kuwazuia kuhesabiwa wala kuwatoza hela kwa ajili ya zoezi hili, akitokea mtu wa aina hiyo toeni taarifa kwa Serikali nasi tutamshughulikia mara moja”. Amesema kuwa zoezi hilo lipo kisheria hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kushiriki kwa uhuru na pasipo hofu wala bugdha yoyote. 

Akielezea umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa zoezi hilo lina umuhimu wa kipekee kwa sababu takwimu zitakazokusanywa katika zoezi hilo zitatumika katika kutathmini utekelezaji wa mipango mikubwa ya maendeleo sambamba na utekelezaji wa malengo ya milenia 2015.  

Akiongelea mabadiliko ya Sera mbalimbali za nchi kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi, Mratibu Msaidizi wa Sensa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga amesema kuwa takwimu hizo zitakazokusanywa katika Sensa ndizo zitakuwa msingi wa kubadili Sera mbalimbali zilizopo ili ziendane na hali halisi nchini. Amesema takwimu hizo pia zitasaidia katika kuainisha maeneo ya kuboreshwa kwa kufanya tafiti mbalimbali za kina kwa lengo la kupata suluhisho la matatizo yaliyopo.

Millinga amesema kuwa kuanzia alhamisi tarehe 23 mwezi huu, makarani wa Sensa wataanza kupita katika maeneo mbalimbali mkoani kukusanya taarifa za dodoso la jamii na kuomba wapewe ushirikiano. Akifafanua kuhusu dodoso la jamii, amesema kuwa dodoso hilo litajazwa ndani ya siku tatu kabla ya siku ya Sensa. Mratibu msaidizi wa Sensa Mkoa amesema kuwa dodoso hilo litakusanya taarifa mahususi zinazohusu huduma za jamii kama afya, zahanati, masoko, vituo vya afya, shule vyanzo vya maji, miundombinu na huduma a kifedha. 

Amesema katika dodoso hilo viongozi wa jamii husika ndio watahusika katika kujibu maswali ya dodoso hilo kutokana na uelewa wao mpana wa huduma zitolewazo katika eneo husika. 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa yupo katika ziara ya kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012,  kukagua shughuli mbalimbali na kuhamasisha maedeleo na kuwahamasisha wananchi juu ya mchakato wa mabadiliko ya katiba mpya katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa. Katika siku yake ya kwanza amefanya mikutano minne ya hadhara katika vijiji vya Ilambilole, Uhominyi, Nyang’oro na Ikengeza.
=30=