Monday, March 26, 2018

Viongozi Iringa kupunguza Maambukizi ya Kifua Kikuu-RC Masenza



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Viongozi mkoani Iringa wametakiwa kujipanga kuhakikisha maambukizi ya kifua kikuu yanapungua ili wananchi waweze kutekeleza shughuli za maendeleo.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza aliyekuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya kifua kikuu duniani yaliyofanyika ngazi ya mkoa katika mji wa Ilula wilayani Kilolo hivi karibuni.
 
Masenza alisema kuwa viongozi katika ngazi zao wanajukumu la kuhakikisha maambukizi ya kifua kikuu yanapungua katika jamii inayowazunguka ili jamii hiyo iweze kufanya kazi za kuzalisha mali. “Kwa hiyo katika vikao vyote vitakavyofanyika katika maeneo yetu ya kazi, katika ngazi zote kifua kikuu iwe ni agenda ili kuweza kupanga mikakati ya uboreshaji wa huduma za kifua kikuu” alisema Masenza. 

Aidha, alizitaka Halmashauri katika mkoa wa Iringa kupanga na kufanya shughuli za uchunguzi wa dalili za kifua kikuu katika makundi hatarishi. Aliyataja makundi hayo kuwa ni shule, magareza na maeneo yenye mikusanyiko mikubwa ya watu.

Mkuu wa mkoa alisema kuwa katika kuadhimisha juma la siku ya kifua kikuu duniani, katika eneo la Ilula Sokini, huduma mbalimbali zilikuwa zikitolewa kwa wananchi bila malipo. Huduma hizo alizitaja kuwa ni uchunguzi wa dalili za kifua kikuu na matibabu, upimaji wa maambukizi ya VVU, uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi, uchangiaji na utoaji wa damu, huduma ya uzazi wa mpango, elimu kuhusu lishe, na elimu kuhusu kifua kikuu.

Maadhimisho ya siku ya kifua kikuu duniani yamefanyika ngazi ya mkoa katika mji wa Ilula yakiongozwa na kaulimbiu isemayo ‘viongozi tuwe mstari wa mbele kuongoza mapambano ya kutokomeza kifua kikuu’.
=30=

SERIKALI KUENDELEZA BIASHARA NDOGO- RC MASENZA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Serikali imeandaa mkakati wa kuendeleza biashara ndogo kwa lengo la kufikia uchumi unaotegemea viwanda ifikapo mwaka 2025.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua maonesho ya wajasiriamali wadogo na wa kati katika uwanja wa mashujaa mjini Mafinga jana.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza akikagua bidhaa katika Maonesho ya wajasiriamali mjini Mafinga

Masenza alisema kuwa katika nchini nyingi duniani, asilimia kubwa ya pato la watu binafsi linatokana na biashara ndogo na za kati. 

Hivyo kuendeleza sekta hii ni mkakati wa kutimiza  malengo ya dira ya maendeleo ya kuwa na uchumi imara unaotegemea  uzalishaji katika viwanda  ifikapo 2025” alisema Masenza. Aidha, aliwataka SIDO kuandaa mkakati wa kuwasaidia wajasiriamali waweze kupata masoko ya kudumu ndani na nje ya nchi.

Akiongelea changamoto ya uingizaji bidhaa kutoka nje, mkuu wa mkoa alisema kuwa uzalishaji wa bidhaa nyingi ndiyo suluhisho la kujitegemea kwa mkoa wa Iringa. Alisema kuwa uzalishaji huo utapunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi na kuongeza matumizi ya malighafi zinazozalishwa ndani kutumika katika viwanda vya ndani. 

Utaratibu huu utasaidia kulinda viwanda vyetu wenyewe bila kutegemea masoko ya nje tu kwa baadhi ya malighafi zetu” alisema mkuu wa mkoa.

Katika kipindi hiki chenye changamoto za kiuchumi duniani tujitahidi kuzalisha bidhaa kwa wingi na zenye ubora wa hali ya juu ili kuongeza ajira na pato la Taifa. Wananchi wote, wafanyabiashara na viongozi mliobahatika kutembelea maonesho haya, hii ni fursa nzuri ya kuweka miadi na kununua au kuchangia mawazo yenu katika kuboresha bidhaa zetu za hapa nchini, ili kusaidia kujenge msingi imara wa viwanda na uchumi wetu” alisisitiza mkuu wa mkoa.

Maonesho ya wajasiriamali kwa mkoa wa Iringa ni ya kwanza ya aina yake yaliyoandaliwa na T-LED, SIDO, TCCIA, TWCC  kwa kushirikiana na Halmashauri ya mji wa Mafinga.
=30=


MATUKIO KATIKA PICHA MAONESHO YA WAJASIRIAMALI MAFINGA