Sunday, November 18, 2012

JESHI LA POLISI LAFANYA KAZI NZURI IRINGA


Serikali imelipongeza jeshi la polisi mkoani hapa kwa kazi nzuri linayofanya katika kuhakikisha ulinzi wa wananchi na mali zao unalindwa na wananchi wanaendelea kuishi na kufanya kazi kwa amani na utulivu.
Waziri wa Nchi, OWM- Sera, Uratibu na Bunge William Lukuvi (katikati) akimjulia hali Padri Angelo Burgeo hatika hospitali ya mkoa wa Iringa

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu mwenye dhamana ya Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvu alipokuwa akiongea na waandishi wa habari katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa alipofanya ziara ya kiserikali pamoja na mambo mengine kuwajulia hali na kuwapa pole mapadri Angelo Burgio (60) kutoka Italia na msaidizi wake Herman Myala wa kanisa katoliki, parokia ya Isimani, jimbo la Iringa waliojeruhiwa vibaya na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi.

Lukuvi amesema “napenda kulipongeza jeshi la polisi chini ya kamanda wa mkoa wa Iringa, Michael Kamhanda kwa jitihada zao za kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa katika hali ya usalama wao na mali zao”. Aidha, amezipongeza jitihada za jeshi hilo za kuhakikisha watuhumiwa wa uhalifu uliofanyika katika parokia ya Isimani wanakamatwa na kufikishwa katika mkondo wa sheria. Amesema kuwa ndani ya siku mbili jeshi hilo limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa wanane jambo linalodhihirisha utendaji makini wa jeshi hilo.

Kutokana na kazi hiyo nzuri, Waziri huyo amevitaka vyombo vya habari mkoani hapa kuhakikisha vinatangaza utendaji na ufanisi wa jeshi hilo ili wananchi waweze kufahamu utendaji huo na kuondokana na hofu inayoweza kujitokeza na kuendelea na utendaji kazi wao wa kila siku. Amewahakikishia wananchi kuwa serikali yao ipo makini kuhakikisha usalama wao.

Amesema kuwa ipo dhana iliyojengeka ndani ya jamii hasa wanapowaona wazungu wanadhani kuwa ni watu wenye fedha nyingi hivyo kushawishika kufanya uhalifu.

Wakati huohuo, Waziri Lukuvi amesema kuwa tukio hilo la ujambazi wa kutumia silaha ni uhalifu wa kawaida kama unavyofanyika uhalifu mwingine wa aina hiyo nchini hivyo usihusishwe na hisia nyinyine kwa namna yoyote ile.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Kamishna Mwandamizi Msaidizi Michael Kamhanda, amesema kuwa wananchi wa Isimani wametoa ushirikiano mkubwa kwa jeshi hilo katika tukio hilo na kuhakikisha watuhumiwa wa uhalifu huo wanakamatwa mapema na kufikishwa katika mikono ya sheria. Amesema kuwa watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani hivi karibuni baada ya upelelezi kukamilika. Amesema kuwa jeshi la polisi limeanzisha program maalumu kwa mkoa mzima ya kuwaelimisha wananchi na taasisi juu ya ulinzi shirikishi na mbinu za kujilinda wenyewe.   
Waziri wa Nchi, OWM- Sera, Uratibu na Bunge William Lukuvi (kulia) akimpongeza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa Kamishana Mwandamizi Msaidizi, Michael Kamuhanda (kushoto) (katikati) ni Afisa Muuguzi Muuguzi msaidizi mkuu Lustica Tun’gombe. 

Akiongelea maendeleo ya mapandri hao, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Iringa, Dk. Faustine Gwanchele amesema kuwa mapadri hao wanaendelea vizuri kwa ujumla.
=30=

MASHINE YA ULTRASOUND YAFUNGWA AGA KHAN



Hospitali ya Aga Khan Iringa imefunga mashine mpya ya kisasa ya Ultrasound iitwayo Sonoace R5 iliyotengenezwa na kampuni ya Samsung Medison kwa lengo la kutoa huduma bora za Ultrasound mkoani Iringa na maeneo ya jirani.


Mtaalamu wa kuendesha mashine ya Ultrasound katika Hospitali ya Aga Khan Iringa John Mwega akifanya uchunguzi muda mfupi baada ya kufungwa kwa mashine ya kisasa ya Ultrasound  Sonoace R5 jana.


Mashine ya kisasa ya Ultrasound Sonoace R5

Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti la Uhuru, Mratibu wa huduma za matibabu (PMC) kwa hospitali za Aga Khan, Saidu Beyai amesema kuwa hospitali ya Aga Khan imeamua kufunga mashine hiyo kwa lengo la kuboresha huduma za uchunguzi kwa wagonjwa wanaohitaji uchunguzi huo kwa njia ya Ultrasound. Amesema kuwa mashine hiyo pia itaboresha uchunguzi wa ubora wa huduma hiyo na matokeo yake kwa wanawake wajawazito kwa haraka na ubora unaokubalika.

Nae mtaalamu wa uendeshaji wa mashine hiyo, John Mwega amesema kuwa mashien hiyo italeta mapinduzi ya kimatibabu katika uchunguzi na matibabu kwa sababu mashine hiyo inazo probu tatu tofauti na ile ya awali iliyokuwa ndogo na kuwa na probu moja jambo lilikuwa likizuia uchunguzi wa baadhi ya magonjwa katika mwili wa binadamu. Amesema kuwa tofauti na ile mashine ya awali, mashine hii mpya itakuwa ikiwezesha uchunguzi wa matatizo ya ndani zaidi ya wanawake tofauti na mashine ya awali iliyokuwa inatumika zaidi nje (juu ya tumbo la mwanamke).

Mwega amesema kuwa mashine hii kubwa zaidi itasaidia hata matatizo ya mishipa ya damu kuweza kuangaliwa vizuri tofauti na awali sambamba na ubora wa picha zitakazopigwa.
Akielezea umuhimu wa mashine hiyo katika kumsaidia daktari kumhudumia mgonjwa wake vizuri, mtaalamu huyo wa uendeshaji mashine amesema “unapoweza kutambua ugongwa mapema unaweza kumhudumia mgonjwa wako mapena na kwa haraka hivyo kuweza kuhudumia wagonjwa wengi kwa haraka tofauti na ilivyokuwa awali”. Amesema mashine hiyo mpya inaweza kufanya uchunguzi kwa ogani za mwili kwa wanaume na wanawake.

Amesema kuwa mashine hiyo ni mzuri zaidi kwa sababu inao uwezo mkubwa wa kuhifadhi picha na taarifa za mgonjwa jambo linaloweza kumsaidia daktari kuweza kufanya ulinganifu na kushauriana na madaktari wengine katika kupata ufanisi wa tiba. Aidha, ametoa wito kwa wananchi kuweza kufika katika hospitali hiyo kwa ajili ya huduma hizo bora na za kisasa za Ultrasound.

Ikumbukwe kuwa hospitali ya Aga Khan imekuwa ikipokea kati ya wagonjwa 10-25 kwa siku kwa huduma za Ultrasound.
=30=

Picha IMG 7863 mashine ya Ultrasound  Sonoace R5 jana ikioa majibu ya kipimo.