Friday, November 30, 2012

WAHASIBU WATAKIWA KUBADILIKA


Wahasibu nchini wametakiwa kubadilika na kuendana na mabadiliko ya kimfumo hasa imapoanzishwa kwa ajili ya kuboresha ufanisi wa kazi na kupunguza upotevu wa fedha za Serikali.

Waziri wa Fedha, Dkt. William Mgimwa
 
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Fedha, Dkt. William Mgimwa alipokuwa akiongea na maafisa wa Serikali Mkoani Iringa muda mfupi kabla ya kuhudhuria Mahafari ya Chuo kikuu cha Ruaha Iringa (RUCO).

Akifafanua kuhusu changamoto za mfumo wa Epicor 9.05 katika utekelezaji wa kazi za kihasibu na malipo, Dkt. Mgimwa ambae pia ni mbunge wa jimbo la Kalenga amesema kuwa lengo la Serikali kuanzisha mfumo huo ni kuhakikisha ufanisi katika matumizi ya fedha za serikali na kuondoa mianya ya upotevu wa fedha hizo. Amesema “tumekuwa na kipindi kifupi sana cha kuwawezesha wahasibu wetu juu ya kuutumia mfumo wa Epicor 9.05”. Akiufafanua mfumo huo, amesema kuwa mfumo huo ulianzia Marekani mwaka 1996 na kuanzishwa nchini kutokana na uwezoz wake wa kuchukua maagizo ya kimalipo kwa wingi, ukubwa, wepesi na haraka na sifa yake nyingine ni kukidhi viwango vya kihasibu vya kimataifa. Amesema kuwa mfumo huo pia unauwezo mkubwa wa kuhifadhi taarifa nyingi kwa wakati. 

Amesema kuwa ili kuweza kuenda vizuri na mfumo huo ni lazima wahasibu wakubali kubadilika na kuwa wepesi zaidi kuyakubali mabadiliko hayo.

Akiongelea uidhinishwaji wa fedha za miradi ya maendeleo ambao umekuwa ukilaumiwa sana kuwa umekuwa ukichelewa sana, Waziri wa Fedha amesema kuwa mchanganuo wa matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo ni muhimu sana na ndio unaozingatiwa kabla ya kuidhinishwa malipo wengine ya miradi ya maendeleo. Amesema kuwa thamani ya fedha ni jambo linalopewa uzito katika miradi yote ya maendeleo ili fedha ya serikali inayotolewa iendane na mradi uliokusudiwa. Amesema kuwa changamoto iliyopo katika kodi ya Serikali ikihusishwa na miradi ya maendeleo, amesema “tunaruhusiwa kutoa asilimia tano tu iliyopatikana na kupeleka katika miradi ya maendeleo na asilimia nyingine inabaki kwa ajili ya kulipa mishahara na shughuli nyingine za uendeshaji wa Serikali” amesisitiza Dkt. Mgimwa.  

Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Nuhu Mwasumilwe ameelezea changamoto inayoukabili Mkoa wa Iringa kuwa ni ukomo wa bajeti hasa katika miradi ya maendeleo. Amesema kuwa katika miradi ya maendeleo fedha hizo zimepungua kutoka shilingi bilioni 1 hadi milioni 274. Ametolea mfano miradi inayoendelea kuwa ndiyo inayoathirika zaidi, kama ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iringa mwaka 2012/2013 imetengewa shilingi milioni 51 tu kati ya milioni 700 zinazohitajika.

Aidha, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa ameiomba Hazina kuwa inatoa kipaumbele kwa miradi ya maendeleo inayoendelea. Akiongelea fedha za matumizi ya kawaida amesema kuwa kupungua kwa fedha hizo kumekuwa kukisababisha kutokueleweka katika maeneo mengine ikiwa ni pamoja na Ofisi za Wakuu wa Wilaya. Amesema mfano mwaka 2011/ 2012 fedha za matumizi mengine Mkoa ulipangiwa shilingi bilioni 2.7 ingawa hazikutolewa zote. Aidha, mwaka 2012/2013 Mkoa umepangiwa shilingi bilioni 1.9.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amempongeza Waziri wa Fedha kwa kuteuliwa kwake katika nafasi hiyo na kuomba ushirikiano wa viongozi na wadau wote katika kuwaletea wananchi maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
=30=

Wednesday, November 28, 2012

CHANJO YA MPYA KUZINDULIWA JAN, 2013




Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma ametoa wito kwa wananchi kuondokana na hofu pale chanjo ya mpya za magonjwa ya kuhara na nimonia zitakapoanzishwa mkoani Iringa.

Rai hiyo ameitoa alipokuwa akifungua kikao cha kamati ya huduma ya afya ya msingi Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.


Dkt. Christine amesema kuwa mara nyingi chanjo mpya zinapoanzishwa wananchi wanakuwa na hofu na minong’ono mbalimbali. Amesema “napenda kuwahakikishia wananchi kuwa chanjo hizi ni salama na zimefanyiwa utafiti wa kina, hivyo ni salama kwa matumizi ya binabamu”. Aidha, ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuwapeleka watoto wao kupatiwa chanjo hizo ili kuweza kupunguza na hatimae kuondoa kabisa vifo vya watoto wadogo.

Akiwasilisha mada juu ya kuanzishwa kwa chanjo mpya za “Rotavirus na Pneumococcal” Mratibu wa huduma za chanjo Mkoa wa Iringa, Naftal Mwalongo amesema kuwa chanjo ni moja kati ya afua madhubuti na nafuu za kuzuia magonjwa na vifo. Amesema chanjo inazuia magonjwa, ulemavu na inaokoa mamilioni ya watoto kila mwaka.

Akiongelea nafasi ya chanjo katika utekelezaji wa malengo ya milenia, Mwalongo amesema “chanjo ni afua muhimu kufikia lengo namba nne la milenia la kupunguza vifo vya watoto  chini ya mwaka mmoja ifikapo 2015”.

Mwalongo amesema kuwa hali ya ugonjwa wa kuharisha kwa Mkoa wa Iringa mwaka 2010-2011, idadi ya wagonjwa wa kuharisha chini ya miaka mitano kwa mwaka 2010 ilikuwa ni 35,424 sawa na asilimia 12 kati ya wagonjwa waliopata matibabu ya nje na mwaka 2011 idadi ya wagonjwa wa kiharisha chini ya miaka mitano ilikuwa 34,941 sawa na asilimia 11 kwa wagonjwa waliopata matibabu ya nje.

Amesema kuwa chanzo cha ugonjwa wa kuharisha ni kula au kunywa maji yaliyochafuliwa na kinyesi chenye virusi. Aidha, amesema kuwa muda wa uambukizo hadi dalili kujitokeza ni kati ya saa 24 hadi 48. Amesema kundi linaloathirika zaidi ni watoto chini ya umri wa miaka miwili.

Mratibu wa huduma za chanjo Mkoa wa Iringa, amezitaja dalili za ugonjwa wa kuhara kuwa ni kuharisha, kutapika, kupungukiwa maji na chumvi mwilini na mara chache huambatana na homa.

Amesema kinga yake ni pamoja na kunyonyesha mtoto maziwa ya mama pekee na kuimarisha usafi wa mazingira. Kinga nyingine ameitaja kuwa ni kuimarisha usafi wa mtu binafsi kwa kunawa mikono kwa sabuni na nyongeza ya virutubishovya Zinc huchangia katika kupunguza kuenea kwa Rotavirus, pamoja na kupatiwa chanjo ya Rotavirus.

Kikao hicho kilichojumuisha maafisa waandamizi, viongozi wa dini, waandishi wa habari na watu maarufu, wataalamu toka sekta ya afya kilikuwa na lengo la kutoa uelewa wa pamoja kwa ajili ya kuwaelimisha wananchi juu ya chanjo hizo zitakazoanza mapema mwezi Januari, 2013.
=30=

Monday, November 26, 2012

UKATILI WA KIJINSIA...WANAUME WAWAJIBIKE



Unyanyasaji wa kijinsia ni changamoto kubwa nchini kutokana na baadhi ya dhana na mila na desturi hasa zinazowapa wanaume mamlaka na kuwanyima wanawake haki zao.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika hotuba yake wakati wa uzinguzi wa kampeni ya siku 16 za kupinga unyanyasaji wa kijinsia maadhimisho yaliyofanyika katika uwanja wa Mwembetogwa Manispaa ya Iringa.

Dkt. Christine amesema “unyanyasaji wa kijinsia unaweza kutokea kwa jinsi yeyote ile, mwanamke, mwanaume au watoto. Ila huwapata sana kina mama na vijana hasa watoto wa kike. Unyanyasaji wa kijinsia ni changamoto kubwa ulimwenguni kote, nchini Tanzania, kadhalika katika mikoa yetu ya Iringa, Rukwa, Mbeya, Ruvuma, Njombe, Mtwara na Lindi”. Amesema kuwa baadhi ya dhana kama umasikini, mila na desturi hasa zinazowapa wanaume mamlaka na kuwanyima wanawake haki zao ni moja klati ya viini vinavyopelekea unyanyasaji wa kijinsia nchini. Amesema kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Tanzania Demographic Health Survey mwaka 2010, Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini inakuwango cha wastani wa vitendo unyanyasaji wa kijinsia. Amesema “Iringa 54%, Ruvuma 55%, Mbeya 55%, Mtwara 26%, Lindi 22% na Rukwa 56%” amesema kuwa kwa mikoa ya Iringa, Ruvuma, Mbeya na Rukwa wastani wa kiwango ni mkubwa ukilinganisha na na kiwango cha wastani wa kitaifa ambao ni asilimia 44.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa katika kupambana na hali hiyo, Serikali kupitia Mpango wa kupambana na Umasikini na Kukuza Uchumi Tanzania (MKUKUTA), mabadiliko ya Sera na Sheria mbalimbali ikiwemo Sheria ya Makosa ya Kujamiiana, imefanya juhudi kubwa kukabiliana na tatizo la ukatili wa kijinsia. Aidha, amesema kuwa Mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na wadau utaendelea kuwajengea uwezo watendaji wa Serikali katika ngazi mbalimbali ili waweze kutatua na kuzifanyia kazi kesi zinazohusi ukatili wa kijinsia.

Miongoni mwa jitihada hizo, Mkuu wa Mkoa amezitaja kuwa ni pamoja na kuanzishwa kwa madawati ya jinsia na watoto katika vituo vya polisi na kusisitiza kuwa wananchi wahamasishwe kwenda kutoa taarifa, kuhakikishiwa usalama wao na kuamini kuwa madawati yale yako kwa ajili yao. Amesema katika kuliwekea mkazo tatizo hilo, Mkoa umeziagiza Halmashauri kuendelea kutenga bajeti katika mipango yao kwa ajili ya kutoa mafunzo kuhusu unyanyasaji wa kijinsia, haki za binadamu, sheria na madhara yatokanayo na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Dkt. Christine amesema “yatupasa tukumbuke kuwa ukatili wa kijinsia sio suala la wanawake ama watoto pekee. Ni muhimu sana kwa wakati huu; hasa kwa kina baba kuwa chachu ya mabadiliko kwa kupinga vitendo vya ukatili na hata kukemea tabia hizo”. Amesema ni vema viongozi na jamii ikatumia ushawishi wake kuamsha majadiliano juu ya vitendo hivyo vya ukatili wa kijinsia, kuvipinga kwa nguvu zote na kuwa mfano bora wa kuigwa ili kuimarisha ustawi wa nchi ya Tanzania.
=30=

MUFINDI WAJIDHATITI KUFIKISHA PEMBEJEO VIJIJINI




Wilaya ya Mufindi imehakikisha usambazaji wa pembejeo unafanikiwa kwa kuhakikisha mbadala wa mawakala waliopungukiwa na uwezo wa kusambaza pembejeo za kukuzia baada ya kutoa taarifa kwa uongozi wa wilaya na wakala mwingine kuendeleza usambazaji huo haraka ili kutokuwachelewesha wakulima.

Hayo yamesemwa na Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wa Wilaya ya Mufindi, Edna Kaduma wakati akiwasilisha taarifa ya usambazaji wa pembejeo kwa wilaya ya Mufindi mwaka 2011/2012 na 2012/2013 katika kikao cha kamati ya vocha ya mkoa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Edna amesema kuwa miongoni mwa changamoto ilikuwa ni mawakala kupungukiwa uwezo wa kusambaza pembejeo hasa wakati ilipoanza kutumika mbolea ya kukuzia. Amesema kuwa mawakala hao walitoa taarifa kwa uongozi wa Wilaya na haraka walipatikana mawakala wengine kwa lengo la kuendeleza huduma hiyo pasipo kuwachelewesha wakulima kutumia mbolea hiyo ya kukuzia. Amesema katika kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa, kamati ya vocha Wilaya ya Mufindi ilifanya mikutano mitatu na mawakala wote kwa lengo la kutathmini uwezo wa kila mmoja na kukubaliana maeneo ya kuhudumia kulingana na uwezo wa kila wakala aidha, wale wenye uwezo mkubwa walikubali kutoa huduma kwa maeneo yaliyokosa mawakala.   

Amesema ili kuweka uwazi katika mchakato huo, kamati ya vocha ya wilaya ilifanya mikutano ya hadhara na wananchi kwa kila kata na pamoja na kukutana na kamati za vocha za vijiji kwa ajili ya kutoa maelekezo ya utaratibu wa mpito wa usambazaji wa pembejeo kwa kutumia vocha. Amesema miongoni mwa changamoto ni kupanda kwa bei za pembejeo baadhi ya wakulima wameshindwa kutumia pembejeo bora. Amesema miongoni mwa changamoto pia ni kupungua kwa wanufaika kutokana na kupungua kwa idadi ya vocha na kuchelewa kuwa vocha za ruzuku kusababisha baadhi ya vijiji kutotumia vocha za mbegu bora.

Edna amesema kuwa ili kuhakikisha usambazaji unafika katika maeneo yote suala la mawasiliano lilipewa uzito unaostahili. Amesema mawasiliano na ufuatiliaji wa mara kwa mara ulifanyika kati ya wilaya na vijiji ili kuhakikisha maeneo yote usambazaji unakwenda vizuri na pembejeo zinauzwa kwa bei iliyokubalika katika vikao.

Akiongelea maadalizi ya pembejeo kwa msimu wa mwaka 2012/2013, Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wilaya ya Mufindi amesema kuwa mahitaji ya mbolea kwa wilaya ya Mufindi, jumla ya tani 13,720 na mahitaji ya mbegu ni jumla ya tani 887. Amesema “msimu huu wilaya imepokea mgao wa vocha seti 22,188 ikiwa ni pungufu kwa asilimia 50 ikilinganishwa na mgao wa msimu uliopita.
=30= 

Wednesday, November 21, 2012

KAMPUNI ZAIDI YA 10 KUSAMBAZA MBOLEA IRINGA




Kampuni za mbolea zaidi ya 10 zimejitokeza kuhudumia wakulima katika Wilaya ya Iringa kwa ajili ya kusambaza vocha za pembejeo za kilimo kwa mwaka 2012/2013 na 2013/2014.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa utoaji wa pembejeo zenye ruzuku kwa msimu wa kilimo wa mwaka 2011/2012 na maandalizi ya kilimo msimu wa mwaka 2012/2013 katika kikao cha kamati ya pembejeo cha mkoa wa Iringa, Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wa Wilaya ya Iringa, Lucy Nyalu amesema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa imepokea utaratibu mpya kutoka Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika wa usambazaji wa pembejeo zenye ruzuku ya Serikali kwa wakulima wa mahindi na mpunga kwa msimu wa kilimo wa mwaka 2012/2013.

Amesema kuwa utaratibu wa kutumia vocha utaendelea ila mawakala watakaosambaza pembejeo hizo kwa wakulima wanufaika na kampuni ya pembejeo ndiyo itasambaza pembejeo hizo badala ya kamati ya pembejeo ya wilaya kama ilivyokuwa awali.
Amesema lengo la kampuni za pembejeo kupewa jukumu la kuteua mawakala ni kuhakikisha pembejeo zenye ubora zinawafikia wakulima kwa wakati muafaka. Amesema kuwa kazi ya kamati ya pembejeo ya wilaya itakuwa ni kusimamia na kufuatilia utaratibu mzima wa pembejeo katika mchakato wote.

Lucy amesema jumla ya kampuni 13 za mbolea na mbegu zimejitokeza kuhudumia wakulima wa Wilaya ya Iringa. Amesema makampuni hayo yameteua mawakala wawakilishi saba na mawakala wasaidizi 46. Akiongelea uhamasishaji wa matumizi ya mbolea ya minjingu mazao pamoja na utaratibu wa usambazaji wa vocha za pembejeo za kilimo kwa wakulima kwa kipindi cha mwaka 2012/2013 na 2013/2014 umefanyika katika vijiji vya Nyabula, Lupembelwasenga, Usengelindeti, Makombe, Kihanga, Ng’enza, Magulilwa na Tagamenda. Uhamasishaji huo unaendelea sambamba na usambazaji wa vocha za pembejeo.

Wakati huohuo, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa imepokea mgao wa pembejeo zenye ruzuku kwa mwaka 2012/2013 zenye thamani ya shilingi 1,828,654,000. Akielezea aina ya pembejeo hizo, Afisa Kilimo, mifugo na ushirika amesema kuwa mbolea ya kupandia vocha (22,000), mbolea ya kukuzia (22,000), mbegu ya mahindi (chotara) (5,409),mbegu ya mahindi mchanganyiko (9,309), mbegu ya mpunga (7,282).

Lucy ameyataja mafanikio yaliyotokana na mfumo wa vocha kuwa ni upatikanaji wa pembejeo katika ngazi ya kijiji umefikiwa ambapo wakulima wanaweza kununua pembejeo katika maeneo ya vijiji vyao. Mafanikio mengine ameyataja kuwa ni ongezeko la uzalishaji kutoka gumia 3-5 za mahindi hadi kufikia wastani wa gunia 12-22 kwa ekari, kwa zao la mpunga ongezeko kutoka gunia 8-10 hadi kufikia wastani wa gunia 16-25.  Aidha, idadi ya wakulima wanaolima kitaalamu imeongezeka na matumizi ya pembejeo kwa wakulima yameongezeka.

Akifungua kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amekiaarifu kikao hicho kuwa msimu wa kilimo umefika na kuwa mvua zimeanza kunyesha katika baadhi ya maeneo ya Wilaya ya Mufindi na wakulima wameanza kupanda. Aidha, aliwataka wataalamu wa kilimo kuwa karibu na wakulima katika kuwafundisha na kuwaelekeza mbinu bora za kilimo. 

=30= 

JAPAN KUSHIRIKIANA NA TANZANIA KATIKA AFYA



Serikali ya Japan imeahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina yake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sekta mbalimbali hasa sekta ya afya na kilimo.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma akimkabidhi kitabu cha profile ya Mkoa wa Iringa Balozi wa Japan nchini Tanzania

Ahadi hiyo imetolewa na Balozi wa Japan nchini Tanzania Masaki Okada alipotembelea ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa katika ziara iliyolenga kusaini mkataba wa ukarabati wa hospitali ya Tosamaganga iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Iringa.

Balozi Okada amesema kuwa Serikali yake itaendeleza ushirikiano na Tanzania katika kuhakikisha uchumi unakuwa kwa kasi zaidi kwa kukuza biashara baina ya nchi mbili hizo. Amesema kwa kuwa zaidi ya asilimia 80 ya watanzania wanategemea kilimo, ni lazima kipato chao kiongezeke ili waweze kunufaika na kilimo hicho kama shughuli yao kuu ya kiuchumi. Amesema kuwa Serikali yake inao mpango wa kuisaidia sekta ya kilimo nchili ili kuhakikisha kilimo cha mpunga kinaongezeka mara dufu kwa kuwa nchi ya Japan inasifika kwa uzalishaji wa mpunga duniani.

Aidha, amezipongeza juhudi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuwaletea maendeleo wananchi wake na kuahidi kuziunga mkono juhudi hizo kwa karibu.

Awali katika salamu za Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amesifu juhudi za Serikali ya Japan katika kusaidia maendeleo kwa mkoa wa Iringa na kusema ni juhudi za kupongezwa sana. Amesema kupitia misaada ya Japan, Halmashauri ya Wilaya ya Iringa imeweza kupata ufadhili katika utekelezaji wa miradi ya afya, elimu, kilimo, maji na umwagiliaji.

Akiongelea maambukizi ya virusi vya ukimwi na ukimwi, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa kwa kujibu wa utafiti wa mwaka 2008, mkoa wa Iringa ulikuwa na takribani asilimia 16 ya maambukizi, kiwango ambacho ni karibu mara tatu ya kiwango cha maambukizi kitaifa. Amesema kuwa hali hiyo haikubaliki na zinaihitajika juhudi za pamoja kati ya Tanzania na Japan katika kuendeleza mapambano hayo. Aidha, amezipongeza juhudi za Serikali ya Japan za kuisaidia Tanzania katika sekta ya afya na ustawi wa jamii kupitia miradi mbalimbali kwa lengo la kuboresha afya ya mama na familia katika  mkoa wa Iringa.

Balozi wa Japan nchini Tanzania yupo mkoani Iringa kwa ajili ya utiaji saini mkataba wa ukarabati wa hospitali ya Tosamaganga unaogharimu dola za kimarekani 123,339 kwa lengo la kuongeza ubora wa huduma za afya na kupunguza vifo vya wanawake na watoto mkoani Iringa.
=30=


Monday, November 19, 2012



TAMKO LA ASKOFU METHODIUS KILAINI

Askofu Methodius Kilaini

Kwa masikitiko makubwa nimesoma katika gazeti la Mwananchi kwamba nimeiponda safu ya uongozi na sekretariati ya CCM. Mimi sijaongea na gazeti lolote juu ya uongozi wa CCM na wala sina nia au sababu ya kuuponda uongozi huo. 

 Ni vibaya kwa gazeti lo lote lile kutumia jina la mtu kwa kueneza maoni yake. Kama ni waugwana natumaini watasahihisha waliyoyaandika. Nasikitika sana kwa kunikwazwa na hilo. 
 

Askofu Method Kilaini
Bukoba Catholic Diocese


Sunday, November 18, 2012

JESHI LA POLISI LAFANYA KAZI NZURI IRINGA


Serikali imelipongeza jeshi la polisi mkoani hapa kwa kazi nzuri linayofanya katika kuhakikisha ulinzi wa wananchi na mali zao unalindwa na wananchi wanaendelea kuishi na kufanya kazi kwa amani na utulivu.
Waziri wa Nchi, OWM- Sera, Uratibu na Bunge William Lukuvi (katikati) akimjulia hali Padri Angelo Burgeo hatika hospitali ya mkoa wa Iringa

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu mwenye dhamana ya Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvu alipokuwa akiongea na waandishi wa habari katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa alipofanya ziara ya kiserikali pamoja na mambo mengine kuwajulia hali na kuwapa pole mapadri Angelo Burgio (60) kutoka Italia na msaidizi wake Herman Myala wa kanisa katoliki, parokia ya Isimani, jimbo la Iringa waliojeruhiwa vibaya na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi.

Lukuvi amesema “napenda kulipongeza jeshi la polisi chini ya kamanda wa mkoa wa Iringa, Michael Kamhanda kwa jitihada zao za kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa katika hali ya usalama wao na mali zao”. Aidha, amezipongeza jitihada za jeshi hilo za kuhakikisha watuhumiwa wa uhalifu uliofanyika katika parokia ya Isimani wanakamatwa na kufikishwa katika mkondo wa sheria. Amesema kuwa ndani ya siku mbili jeshi hilo limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa wanane jambo linalodhihirisha utendaji makini wa jeshi hilo.

Kutokana na kazi hiyo nzuri, Waziri huyo amevitaka vyombo vya habari mkoani hapa kuhakikisha vinatangaza utendaji na ufanisi wa jeshi hilo ili wananchi waweze kufahamu utendaji huo na kuondokana na hofu inayoweza kujitokeza na kuendelea na utendaji kazi wao wa kila siku. Amewahakikishia wananchi kuwa serikali yao ipo makini kuhakikisha usalama wao.

Amesema kuwa ipo dhana iliyojengeka ndani ya jamii hasa wanapowaona wazungu wanadhani kuwa ni watu wenye fedha nyingi hivyo kushawishika kufanya uhalifu.

Wakati huohuo, Waziri Lukuvi amesema kuwa tukio hilo la ujambazi wa kutumia silaha ni uhalifu wa kawaida kama unavyofanyika uhalifu mwingine wa aina hiyo nchini hivyo usihusishwe na hisia nyinyine kwa namna yoyote ile.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Kamishna Mwandamizi Msaidizi Michael Kamhanda, amesema kuwa wananchi wa Isimani wametoa ushirikiano mkubwa kwa jeshi hilo katika tukio hilo na kuhakikisha watuhumiwa wa uhalifu huo wanakamatwa mapema na kufikishwa katika mikono ya sheria. Amesema kuwa watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani hivi karibuni baada ya upelelezi kukamilika. Amesema kuwa jeshi la polisi limeanzisha program maalumu kwa mkoa mzima ya kuwaelimisha wananchi na taasisi juu ya ulinzi shirikishi na mbinu za kujilinda wenyewe.   
Waziri wa Nchi, OWM- Sera, Uratibu na Bunge William Lukuvi (kulia) akimpongeza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa Kamishana Mwandamizi Msaidizi, Michael Kamuhanda (kushoto) (katikati) ni Afisa Muuguzi Muuguzi msaidizi mkuu Lustica Tun’gombe. 

Akiongelea maendeleo ya mapandri hao, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Iringa, Dk. Faustine Gwanchele amesema kuwa mapadri hao wanaendelea vizuri kwa ujumla.
=30=

MASHINE YA ULTRASOUND YAFUNGWA AGA KHAN



Hospitali ya Aga Khan Iringa imefunga mashine mpya ya kisasa ya Ultrasound iitwayo Sonoace R5 iliyotengenezwa na kampuni ya Samsung Medison kwa lengo la kutoa huduma bora za Ultrasound mkoani Iringa na maeneo ya jirani.


Mtaalamu wa kuendesha mashine ya Ultrasound katika Hospitali ya Aga Khan Iringa John Mwega akifanya uchunguzi muda mfupi baada ya kufungwa kwa mashine ya kisasa ya Ultrasound  Sonoace R5 jana.


Mashine ya kisasa ya Ultrasound Sonoace R5

Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti la Uhuru, Mratibu wa huduma za matibabu (PMC) kwa hospitali za Aga Khan, Saidu Beyai amesema kuwa hospitali ya Aga Khan imeamua kufunga mashine hiyo kwa lengo la kuboresha huduma za uchunguzi kwa wagonjwa wanaohitaji uchunguzi huo kwa njia ya Ultrasound. Amesema kuwa mashine hiyo pia itaboresha uchunguzi wa ubora wa huduma hiyo na matokeo yake kwa wanawake wajawazito kwa haraka na ubora unaokubalika.

Nae mtaalamu wa uendeshaji wa mashine hiyo, John Mwega amesema kuwa mashien hiyo italeta mapinduzi ya kimatibabu katika uchunguzi na matibabu kwa sababu mashine hiyo inazo probu tatu tofauti na ile ya awali iliyokuwa ndogo na kuwa na probu moja jambo lilikuwa likizuia uchunguzi wa baadhi ya magonjwa katika mwili wa binadamu. Amesema kuwa tofauti na ile mashine ya awali, mashine hii mpya itakuwa ikiwezesha uchunguzi wa matatizo ya ndani zaidi ya wanawake tofauti na mashine ya awali iliyokuwa inatumika zaidi nje (juu ya tumbo la mwanamke).

Mwega amesema kuwa mashine hii kubwa zaidi itasaidia hata matatizo ya mishipa ya damu kuweza kuangaliwa vizuri tofauti na awali sambamba na ubora wa picha zitakazopigwa.
Akielezea umuhimu wa mashine hiyo katika kumsaidia daktari kumhudumia mgonjwa wake vizuri, mtaalamu huyo wa uendeshaji mashine amesema “unapoweza kutambua ugongwa mapema unaweza kumhudumia mgonjwa wako mapena na kwa haraka hivyo kuweza kuhudumia wagonjwa wengi kwa haraka tofauti na ilivyokuwa awali”. Amesema mashine hiyo mpya inaweza kufanya uchunguzi kwa ogani za mwili kwa wanaume na wanawake.

Amesema kuwa mashine hiyo ni mzuri zaidi kwa sababu inao uwezo mkubwa wa kuhifadhi picha na taarifa za mgonjwa jambo linaloweza kumsaidia daktari kuweza kufanya ulinganifu na kushauriana na madaktari wengine katika kupata ufanisi wa tiba. Aidha, ametoa wito kwa wananchi kuweza kufika katika hospitali hiyo kwa ajili ya huduma hizo bora na za kisasa za Ultrasound.

Ikumbukwe kuwa hospitali ya Aga Khan imekuwa ikipokea kati ya wagonjwa 10-25 kwa siku kwa huduma za Ultrasound.
=30=

Picha IMG 7863 mashine ya Ultrasound  Sonoace R5 jana ikioa majibu ya kipimo.

Saturday, November 17, 2012

RC AKEMEA UKWEPAJI KODI


Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewataka wananchi kuachana na tabia ya kukwepa kulipa kodi na kuwa wazalendo kwa mkoa wao na Taifa lao kwa ujumla wakati akikemea tabia ya wafanyabiashara wanaokwepa kutumia mashine za kieletroni za kutolea risiti.


Mkuu wa Mkoa amesema hayo katika hotuba yake kwenye maadhimisho ya siku ya mlipakodi iliyofanyika katika ukumbi wa chuo kikuu huria tawi la Iringa iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Dkt. Leticia Warioba.

Dkt. Warioba amesema “bado wapo walipakodi ambao sio wazalendo.Walipakodi ambao mpaka sasa wanakwepa kodi. Tabia hii ya kukwepa kodi siyo ya kizalendo na ningependa kuwaasa muiache mara moja”. Amesema kuwa ukadiliaji na ukusanyaji wa kodi vinafanyika kwa mujibu wa sheria za kodi na ni muhimu kwa kila mlipa kodi kuheshimu sheria na taratibu nchi ilizojiwekea.

Amesema tabia ya kukwepa kodi imekuwa ikiwafanya wafanyabiashara kupitisha bidhaa vichochoroni badala ya kupitisha bidhaa hizo kwenye ofisi za forodha zilizopo mipakani. Amesema kuwa utaratibu huo unafanyika kinyume na sheria za nchi na kutaka tabia hiyo iachwe mara moja.

Akiongelea matumizi ya mashine ya kieletroniki za kutolea risiti, Dkt. Leticia amesema “matumizi ya mashine hizo ni changamoto katika utendaji kazi wa Mamlaka ya Mapato nchini, ningependa kuwafahamisha kuwa, matumizi ya mashine hizi ni agizo la Serikali na lengo lake ni kuhakikisha kodi ya ongezeko la thamani inakusanywa ipasanyo”.

Amewataka wale wote waliosajiliwa na kodi ya ongezeko la thamani kutumia mashine za kieletroniki za kutolea risiti kwa kila mauzo wanayofanya. Amesema kuwa mashine hizo zinatumika kwa mujibu wa sheria ya bunge hivyo utekelezaji wake ni lazima.

Wakati huohuo, Mamlaka ya Mapato Mkoa wa Iringa imefanikiwa kuvuka lengo kwa kukusanya zaidi ya asilimia 100 ya lengo iliyowekewa la idara ya ushuru wa forodha na kodi za ndani. Katika maelezo ya Meneja wa mamlaka ya mapata Mkoa wa Iringa, Rozalia Mwenda amesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2011/2012 Mkoa wa Iringa ulipangiwa kukusanya jumla ya shilingi  23,761,800,000/= lengo la idara ya ushuru wa forodha likiwa shilingi 110,100,000/= na lengo la idara ya kodi za ndani likiwa shilingi 23,651,700,000/=. Amesema kwa kipindi hicho Mkoa ulikusanya shilingi 24,730,752,185 sawa na asilimia 105 ya utendaji.

Akiongelea ubora wa huduma kwa wateja, Rozalia amesema “mamlaka ya mapato makao makuu, mikoani hadi wilayani, inatekeleza sera ya ubora ambayo inaelekeza utendaji kazi wenye lengo la kutoa huduma bora inayokidhi na hata kupita matarajio ya mteja”. Amesema “baada ya kufanyika  kwa ukaguzi wa ubora wa huduma zetu na kampuni ya wakaguzi wa nje, mamlaka ilitunukiwa cheti cha kimataifa cha ubora wa viwango cha ISO 9001:2008”. Amesema kuwa mamlaka yake imepanga kutathmini mara kwa mara viwango vya huduma tunazotoa kwa walipa kodi ili kuhakikisha kuwa mahitaji ya walipakodi yanazingatiwa katika mipango ya mamlaka ya kimkakati.

Amesema kuwa mamlaka yake inaendeleza ushirikiano baina yake na mlipakodi kwa lengo la kudumisha ushirikiano wa kulipa kodi kwa mujibu wa sheria kwa kutoa huduma bora. Amesisitiza kuwa urafiki baina mamlaka na mlipakodi sharti uongeze tija katika kukusanya mapato ya Serikali kwa lengo la kutokumuumiza mlipa kodi na wala Serikali.

Meneja wa mamlaka ya mapato mkoa wa Iringa ameahidi kuongeza juhudi katika utendaji kazi, amesema “mimi na wafanyakazi  wa mamlaka ya mapato Mkoa wa Iringa tunaahidi kuongeza, juhudi, maarifa na uadilifu katika kuhakikisha tunavuka malengo tuliyopangiwa kama tulivyokwishaonesha kipindi kilichopita. Kwa mshikamano na mikakati tuliyonayo, tunaamini malengo ya mwaka 2012/2013 ambayo ni shilingi 33.4 bilioni yanafikiwa”.

Wiki ya maadhimisho ya 6 ya sherehe ya mlipakodi kitaifa ilianza tarehe 01-07 Novemba, 20122 ikiongozwa na kaulimbiu isemayo “ulipaji kodi wa hiari Kwa Taifa lenye mafanikio” ikiwa na lengo kuu la kuboresha huduma kwa mlipakodi.
=30=



MKOA WA IRINGA WAZIDI KUFANIKIWA KATIKA SEKTA YA KILIMO
Mkoa wa Iringa umeendelea kupata mafanikio makubwa katika Sekta ya Uchumi na Uzalishaji mali kwa kuongeza matumizi ya zana za kilimo hadi kufikia asilimia 15 kwa wakazi wa Mkoa huo.

 Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Scolastica Mlawi akifafanua jambo.

Mafanikio hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Scolastica Mlawi wakati akifungua kikao cha siku mbili cha kupitia taarifa za uekelezaji wa kazi za Sehemu ya uchumi na sekta za uzalishaji na kuainisha vipaumbele kwa mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Scolastica amesema “mafanikio kwa upande wa sekta ya kilimo ni pamoja na ongezeko la matumizi ya zana za kilimo ambapo kwa sasa asilimia 15 ya wakazi wa mkoa huu wanatumia matrekta makubwa na madogo katika Kilimo”. Amesema asilimia 20 ya wakazi wanatumia wanyamakazi na asilimia 65 wanatumia jembe la mkono ikilinganishwa na asilimia 75 ya wakulima waliokuwa wanatumia jembe la mkono mwaka 2005.

Kaimu Katibu Tawala Mkoa amesema kuwa pato la mkoa wa Iringa limeongezeka toka Sh. 867,482 mwaka 2005 hadi kufikia Sh. 1,985,708 mwaka 2011, wakati pato la mkazi mwaka 2005 lilikuwa Sh. 558,444 na limeongezeka hadi kufikia Sh. 1,125,503 mwaka 2011.
Akiongelea maandalizi ya kilimo msimu huu, amesema kuwa msimu wa kilimo umeanza na wakulima wameonesha jitihada kubwa katika kulima na kupanda mazao mbalimbali ya chakula na biashara.

Amesema “msimu huu tunajipanga zaidi katika kuhimiza mazao yanayostahimili ukame kama vile alizeti, mtama, muhogo na viazi vitamu. Kwa pamoja tuhimize kilimo cha mazao haya katika maeneo yote yenye ukame (upungufu wa mvua) katika wilaya zote hasa wilaya ya Iringa (Tarafa ya Idodi, Isimani na Pawaga), wilaya ya Kilolo (Tarafa ya Mahenge na Mazombe) wilaya ya Mufindi (Tarafa ya Sadani na Malangali)”.

Akiongelea ufanisi wa kilimo Scolastica amesema “ili kilimo chetu kiweze kufanikiwa vizuri tunahitaji kuwaelimisha wakulima wetu mbinu bora za kilimo ikiwemo matumizi bora na sahihi ya pembejeo za Kilimo”.

Awali Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Sekta ya Uchumi na Uzalishaji, Adam Swai alisema kuwa lengo la kikao hicho ni kutoa taarifa za utekelezaji wa kazi kutoka katika Halmashauri za wilaya ili kujadili tathamini, matokeo na kubadilishana uzoefu wa shughuli na kutoa ushauri wa pamoja katika  kuboresha utekelezaji wa shughuli na kupata takwimu halisia katika sekta ya uchumi. Aidha, amesema kuwa kikao hicho kitasaidia katika kuandaa taarifa ya Mkoa itakayoonyesha vipaumbele vichache ambavyo vitaleta matokeo na mafanikio.
=30=

Sunday, November 11, 2012

MATUKIO YA KUKABIDHI KIKOMBE CHA MSHINDI WA PILI WANAWAKE KUVUTA KAMBA A

 Kombe la mshindi wa pili kuvuta kamba wanawake

 Nahodha wa timu Agnes Mlula akimkabidhi kombe mgeni rasmi Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka

 Kaimu Mwenyekiti mstaafu wa Klabu ya Shimiwi Ras Iringa Gillian Bukori akimkabidhi cheti cha ushiriki wa Mkoa mgeni rasmi Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Gertrude Mpaka.





 Baadhi wa wachezaji wa timu hiyo ya kuvuta kamba wanawake




  




 Picha ya pajama baina ya wachezaji, viongozi wa Mkoa na mgeni rasmi.

Wakati wa Burudani