Friday, December 10, 2010

…UMITASHUMTA NI VIWANGO TU

Wanamichezo na watendaji wametakiwa kuendesha mashindano na kambi ya mkoa wa Iringa kwa viwango vilivyo bora ili mkoa uweze kujivunia hazina ya vipaji iliyopo kwa wananfunzi wa shule za msingi.

Bartholomew Mwellange Mwella, Afisa Tarafa ya Makambako,
akipiga mpira kuashiria ufunguzi rasmi wa UMITASHUMTA Mkoa wa Iringa

Rai hiyo imetolewa na Bartholomew Mwellange Mwella, Afisa Tarafa ya Makambako, kwa niaba ya Katibu Tawala Wilaya ya Njombe, Evergrey Keiya wakati akifungua rasmi mashindano ya michezo ya shule za msingi ngazi ya mkoa wa Iringa uliofanyika katika Mji mdogo wa Makambako.

Mwella amesisitiza kuepuka kasoro zote zilizojitokeza hapo awali na kupelekea mashindano hayo kufutwa mwaka 2001. Aidha alisisitiza kutokuwa na uvumilivu kwa mtendaji yeyote atakayetaka kuharibu mashindano hayo kwa namna moja au nyingine.

Amesisitiza kuwa wakati wa kuchagua timu ya mkoa lazima walimu na wachezaji watakaochaguliwa wawakilishe uhalisia wa mkoa na pasiwepo na masuala ya upendeleo kwa kuangalia udugu, mahusiano mazuri na mtu Fulani, wala Halmashauri anayotoka.

Aidha amewataka washiriki kutumia vizuri fursa waliyoipata kushiriki katika michezo hii kwa kuonesha vipaji vyao na kuuwakilisha vema mkoa katika mashindano ya kitaifa. Afisa Tarafa huyo amesisitiza kucheza kwa amani na utulivu wa hali ya juu mbali na halmashauri wanazotoka kwa kuzingatia wao ni watoto wa mkoa mmoja na ni ndugu.

Akiongeleza sababu za kufutwa kwa mashindano ya UMITASHUMTA mwaka 2001 Mwella amesema kuwepo kwa mapungufu mengi ndiyo sababu ya msingi ya kufutwa kwake. Ameyataja mapungufu hayo kuwa ni pamoja na malezi hafifu hasa kwa wanafunzi wa kike, mapungufu ya idadi ya siku za masomo, tatizo la chakula kwa wanafunzi, watumishi kutopewa stahili zao wanazostahili, udhibiti wa nidhamu kwa wanafunzi na vyombo duni vya usafiri kwa wanafunzi hao.

Nae Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Iringa, Mwalimu Euzebio Mtavangu ameutaja umuhimu wa mashindano hayo kuwa ni kusaidia kuibua vipaji vya wachezaji katika timu za wilaya, Mkoa na Taifa, kuimarisha afya za washiriki, kusaidia kujenga uzalendo wa kulipenda Taifa. Aidha amezitaja faida nyingine kuwa ni sehemu ya muendelezo wa vipaji vya darasani na hivyo kuwafanya wanafunzi wazingatie masomo wakati wote, kusaidia kuimarisha udugu na urafiki miongoni mwa wanamichezo.

Afisa Michezo wa Mkoa wa Iringa, Keneth Komba amesema kuwa lengo la mashindano hayo ya UMITASHUMTA ni kuwajengea umoja wanafunzi wa shule za msingi na kuwafanya wajue kuwa wao ni wamoja. Ameongeza kuwa Mkoa wa Iringa umepata heshima kubwa kuwa miongoni mwa mikoa 10 iliyoteuliwa katika kushiriki katika mashindano hayo. Mikoa hiyo ni Morogoro, Kilimanjaro, Pwani, Singida, Dodoma, Arusha, Tanga, Mbeya, Dar Es Salaam na Iringa yenyewe.

Mashindano ya UMITASHUMTA yatafanyika mjini Kibaha, Mkoani Pwani kuanzia tarehe 13 Disemba, 2010 na yatahusisha michezo ya mpira wa miguu, pete na riadha.           

IRINGA YAONGEZA KIWANGO CHA UFAULU DARASA LA SABA

Mkoa wa Iringa umefanikiwa kuongeza kiwango cha kufaulu kwa wanafunzi waliomaliza darasa la saba mwaka 2010 kutoka asilimia 59.65 ya mwaka 2009 hadi 63.01 mwaka 2010 imefahamishwa.

Hayo yamesemwa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude K Mpaka katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao cha uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2010 kilichofanyika katika kituo cha vijana cha Nazareth Njombe.

Afisa Elimu Mkoa wa Iringa, Mwl Salum Maduhu (kushoto),
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bibi. Gertrude Mpaka (katikati) na
Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Bibi.  Sara Dumda (kulia)

Mpaka amesema “nachukua nafasi hii kuwapongeza Maafisa Elimu wa Wilaya, Waratibu wa Elimu Kata Walimu Wakuu na walimu kwa ujumla kwa kazi nzuri wanayoifanya na kufanya Mkoa wa Iringa kuongeza kiwango cha ufaulu kutoka asilimia 59.65 ya mwaka 2009 hadi asilimia 63.01 mwaka 2010”.

Amezitaja takwimu za watahiniwa wa kuhitimu elimu ya Msingi mwaka 2010 kuwa ni watahiniwa 44,275. Kati yao 20,991 ni wavulana na 23,284 ni wasichana. Aidha jumla ya waliofaulu ni mtihani mwaka 2010 ni 27,899 wavulana wakiwa 13,709 na wasichana ni 14,190, ambao ufaulu huo ni sawa na asilimia 63.01 ya watahiniwa wote.

Katibu Tawala Mkoa ametaja changamoto inayoukabili Mkoa katika Sekta ya elimu kuwa ni wanafunzi wanaosajiliwa kufanya mtihani kutofanya mtihani kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo utoro. Amesema kuwa utoro unachukua karibu asilimia 75.19 ya watahiniwa wote. Idadi ya wanafunzi walioshindwa kufanya mtihani mwaka huu ni 566, ikilinganishwa na 816 walioshindwa kufanya mtihani huo mwaka 2009 na kuagiza litafutiwe ufumbuzi wa kina.

Akiainisha sababu za wasiofanya mtihani Afisa Elimu Mkoa wa Iringa, Salum Maduhu amezitaja kuwa ni utoro wanafunzi (496), vifo (18), ugonjwa (38), mamba (13), sababu nyingine (1).

Kwa upande wa mahudhurio siku ya mitihani yamepanda kutoka 98.43% ya mwaka 2009 hadi 98.74% mwaka 2010. Aidha kiwango cha kumaliza elimu ya msingi kimeshuka kutoka 80.39 (2009) hadi 76.80% (2010) ambayo ni sawa na upungufu wa 3.59%.

Kwa upande wa ufaulu na nafasi kimkoa kwa kila Halmashauri 2010 ni Iringa Manispaa 77.33% (1), Mufindi H/M 71.67% (2), Njombe Mji 71.29% (3), Njombe H/M 66.47% (4), Makete H/M 62.88% (5), Ludewa H/M 58.83% (6), Iringa H/M 42.56% (7) na Kilolo H/M 39.71% (8).

Aidha Afisa elimu Mkoa amezitaja shule 10 zilizofanya vizuri kuwa
ni St.
Benedict (Mji Njombe), Southern Highland (Mufindi), Brooke Bon (Nufindi), Livingstone (Njombe Mji), Ukombozi (Iringa Manispaa), Lupalama A (Iringa H/M), Lihogasa (Njombe Mji), Star (Iringa Manispaa), Lugarawa (Ludewa) na St. Dominic Savio (Iringa Manispaa).

Maduhu pia amewataja wahitimu wawili ambao ni mapacha walioungana kimwili, kutoka shule ya msingi Ikonda, Halmashauri ya Wilaya ya Makete. Wanafunzi hawa wamefaulu na kwa mchanganuo wa alamaufuatao:

JINA
MASOMO
Kis
Eng
M/Jamii
Hisb.
Say
Jumla
Consolatha Mwakikuti
32
34
29
27
29
151
Maria Mwakikuti
32
36
25
27
31
151


Mkoa wa Iringa umekamata nafasi ya tatu kitaifa kwa miaka mine mfululizo tangu mwaka 2007 hati 2010 na unajumla ya shule 853 za msingi.