Tuesday, April 17, 2012

SHERIA YA BIMA YA AFYA KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI

Serikali ya Tanzania iliamua kupitisha Sheria ya kuanzishwa kwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwa kila mtu kwa kuchangia kidogo ili kumuwezesha mwanachi kutibiwa hata kama hana fedha pindi anapougua.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma, katika hotuba yake ya ufunguzi wa kongamano la wadau wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wa Mikoa ya Iringa na Njombe uliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Highland, Manispaa ya Iringa.

Dr. Ishengoma amesema “lengo kuu wa kupitishwa kwa Sheria hii ilikuwa ni kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa kila mtu kwa kuchangia kiwango kidogo kabla ya kuugua, ili anapougua aweze kutibiwa hata kama hatakuwa na fedha za kulipia wakati huo”. Amesema kutokana na gharama za matibabu kuwa juu jambo linalomuwia ugumu mwananchi wa kumudu, ndio msingi ulioifanya Serikali kuanzisha utaratibu wa mwananchi kulipia gharama za matibabu kabla ya kuugua kwa utaratibu wa Bima. Amesema ili utaratibu huu uwe mahususi Serikali ilitunga Sheria inayoanzisha Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii.

Mkuu wa Mkoa amesema kuwa afya bora ni jambo muhimu sana kwa wananchi na ndio chachu ya wananchi kujiletea maendeleo kutokana na uzalishaji sababu kama wananchi hawatakuwa na afya nzuri na imara uzalishaji utashuka na jamii kuendelea kuwa masikini. Amesema kuwa familia inayosumbuliwa na maradhi muda mwingi haiwezi kuzalisha mali.Amesema suluhisho lake ni familia kuwa na uhakika wa matibabu pindi wakiugua, ni vema kuhimiza wananchi kujiunga na Mifuko ya afya ya Jamii katika Halmashauri.

Dr. Ishengoma alionesha kusikitishwa sana na takwimu zinazoonesha kuwa kati ya mwezi Desemba, 2009 na Desemba, 2011 jumla ya shilingi bilioni 3.5 zililipwa na serikali kwa Halmashauri nchini kama tele kwa tele. Kati ya fedha hizo mikoa ya Iringa na Njombe haijaambulia chochote.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Aseri Msangi amewataka viongozi wa bima ya afya katika ngazi za mikoa kuwasilisha taarifa zao katika ofisi ya waku wa wilaya na mikoa ili ziwawezeshe kupanga ratiba za ufuatiliaji na kuhamasisha uhamasishaji kwa wananchi ili mfuko huo wa afya ya jamii iweze kuwa na manufaa na endelevu. Aesema pia changamoto ya mawasiliano na uelewa mdogo pia inahitaji kuangaliwa kwa jicho la karibu na wadau wa bima ya afya kwa lengo la kupanua uelewa wao na wananchi kwa ujumla.

Kaimu Mkurugenziwa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Immaculate Senje, amesema kuwa ili mfuko wa Afya ya Jamii uweze kuwanufaisha wananchi wengi, suala la uhamasishaji jamii linahitaji kupatiwa uzito unaostahili. Amesema kuwa wananchi wapo tayari hasa pale wanapohamasishwa na viongozi na kupatiwa taarifa sahihi hasa manufaa yanayotokana na kujiunga na mfuko huo.


Thursday, April 12, 2012

MALEZI YA WATOTO YAHIMIZWA IRINGA

Na. Dennis Gondwe, IRINGA
Serikali Mkoani Iringa imesema kuwa itaendelea kushirikiana na taasisi binafsi katika kuhakikisha kuwa malezi mazuri yanatolewa kwa watoto na kuwasaidia watoto walio katika mazingira hatarishi ili nao waweze kufurahia matunda ya uhuru kama watoto wengine kwa kuwa na maadili mema.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma katika hotuba yake iliyosomwa na Mwl. Joseph Mnyikambi, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Huduma za Jamii iliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa katika hafla ya ugawaji wa zawadi kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wa Manispaa ya Iringa chini ya shirika lisilo la kiserikali la Operation Christmas Child lenye makao yake Makuu nchini Marekani iliyofanyika katika ukumbi wa IDYDC Manispaa ya Iringa.

Mwl. Mnyikambi amesema kuwa “nimefahamishwa kuwa taasisi hii ya OCC pia inatoa mafunzo yanayolenga maadili. Nawapongeza sana kwa sababu jamii yenye maadili mema ndiyo jamii inayofanikiwa katika maisha”.

Amesema kuwa “ili jamii ifanikiwe katika maisha basi msingi wake lazima jamii hiyo iwekeze katika malezi na makuzi ya watoto katika maadili”. Ametoa wito kwa jamii kulipa kipaumbele suala la maadili kwa watoto na vijana ili kujenga taifa imara na makini.

Amesema kuwa suala la maadili ni suala la upendo katika jamii na kusisitiza kuwa kinyume chake ni mmomonyoko wa maadili katika taifa zima. Amesema kuwa jamii kwa sasa inashuhudia watoto wakitumia dawa za kulevya, ulevi wa kupindukia, lugha za matusi na watoto wa kiume kusuka nywele jambo linalowafananisha na watoto wa kike na kufanya vitendo visivyo vya kibinadamu kama ubakaji wa watoto wadogo.

Katika risala yao iliyosomwa na Mratibu wa Operation Christmas Child Askofu Dk. Boaz Sollo ameishukuru serikali kwa kusamehe kodi na kuiomba kupitia mamlaka ya bandari kuweka mfumo rahisi zaidi wa kutoa vitu bandarini ili kupunguza au kuondoa gharama zinazotokana na uhifadhi wa mizigo hiyo bandarini.

Aidha, ameishauri serikali kuwa macho zaidi na yeyote anayejaribu kuhatarisha amani kwa kutumia dini au siasa ili nchi iiendelee kuwa na amani na utulivu. Amesema kuwa mwaka huu kwa Mkoa wa Iringa umepokea jumla ya mabox 3500 ya zawadi kwa ajili ya watoto 3500.

=30=