Wednesday, May 6, 2015

VIONGOZI WA DINI IRINGA ISAIDIENI SERIKALI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Viongozi wa dini mkoani Iringa wametakiwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali kuhakikisha maisha bora kwa wananchi yanawezekana.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Bibi. Amina Masenza alipokuwa akiongea na viongozi wa dini katika kikao maalumu kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Bibi. Amina Masenza
Bibi. Masenza amesema kuwa viongozi wa dini ni muhimu sana katika kuunga mkono juhudi zinazofanywa na serikali na kufikisha ujumbe kwa watu wengi. Amesema “viongozi wa dini mnao watu wengi nyuma yenu ambao ni waumini na wanawasikiliza hivyo mnawajibu wa kusaidia juhudi zinazofanywa na serikali za kuboresha maisha ya wananchi wake”. 

Akiongelea zoezi linaloendelea la uboreshaji daftari la wapiga kura, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa zoezi la uboreshaji daftari la wapiga kura linaendelea katika mkoa wa Iringa. Amesema kuwa changamoto ni kuwa mashine zinatumia umeme hivyo zinahitaji kuchajiwa na sehemu za vijijini hazina umeme. Amesema kuwa mkoa unakabiliana na changamoto hiyo ili kuhakikisha zoezi zima linakuwa na mafanikio. Amesema changamoto ya matumizi ya kopyuta limechukuliwa kwa uzito unaostahili na watu wenye uelewa wa kompyuta wamechukuliwa katika kufanya zoezi la uboreshaji daftari hilo ili liende vizuri na haraka.

Wakati huohuo, bibi. Masenza amewataka viongozi wa dini kuendelea kuwahamasisha waumini na wananchi kwa ujumla kuipitia na kuifahamu Katiba inayopendekezwa ili mwisho waweze kufanya maamuzi sahihi wananchi wenyewe pasipo kushurutishwa. Amesema kuwa Katiba hiyo imegusa maeneo na makundi yote ya kijamii hivyo ikisomwa kwa umakini itawasaidia wananchi ufanya maamuzi sahihi.

Katika kikao hicho mada juu ya hali ya lishe katika mkoa, hali ya maambukizi ya ukimwi na hali ya elimu ziliwasilishwa na kujadiliwa kwa kina. Viongozi hao wamekubaliana kukutana kila baada ya miezi nne na kujadili mambo muhimu katika mkoa wa Iringa.
=30=

SHULE ZA IGOWOLE NA KAWAWA ZAPONGEZWA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Shule za sekondari za Igowole na Kawawa zimepongezwa kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita mwaka 2014 na kuung’arisha mkoa wa Iringa kitaifa.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya mitihani wa Mkoa wa Iringa, bibi. Wamoja Ayubu alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu mitihani inayoendelea ya kidato cha sita nchini ofisini kwake.

Wamoja amesema “nichukue nafasi hii kipekee kuzipongeza shule za sekondari za Igowole na Kawawa zote zipo katika halmashauri ya wilaya ya Mufindi kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita mwaka 2014, ambapo Igowole iliahika nafasi ya kwanza kitaifa na Kawawa ilishika nafasi ya kumi. Hongereni sana kwa matokeo hayo yaliyoufanya mkoa wetu kung’ara.” “Aidha, nichukue nafasi hii pia kuzipongeza shule zote za mkoa wa Iringa kwa kuwa kwa ujumla wake zilifanya vizuri katika matokeo hayo kati ya shule 22 zilizokuwa na watahiniwa wa kidato cha sita mwaka 2014 shule 18 zilifaulisha kwa asilimia 100 kwa maana hakukuwa na mwanafunzi aliyepata daraja la 0”, aliongeza bibi. Wamoja.

Akiongelea mitihani inayoendelea ya kidato cha sita, Mwenyekiti wa Kamati ya Mitihani wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa mkoa unavyo vituo 23 vya mtihani wa kidato cha sita vyenye jumla watahiniwa 2,162. Amesema kuwa vituo hivyo vitasimamiwa na wasimamizi 73 kati yao wasimamizi wakuu 23 na wasimamizi wasaidizi kutoka nje wapatao 50. 

Kwa mitihani ya ualimu, amesema vipo vituo 4 vyenye jumla ya watahiniwa 324 kati yao 122 ni ngazi ya Cheti na 202 ngazi ya Diploma. Ameongeza kuwa vituo hivyo vitasimamiwa na wasimamizi wakuu wanne na wasimamizi wasaidizi saba kutoka nje.
Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amewataka wasimamizi kutokuwa na tamaa ya fedha itakayowasababishia kujiingiza katika vitendo vya uvujishaji mitihani. Aidha, amewataka kuzingatia ratiba zilizotolewa ili kila mtihani ufanyike kwa wakati uliopangwa na kuwepo katika chumba cha mtihani kipindi chote ili kutotoa mwanya kwa watahiniwa kutazamiana.

Wakati huohuo Mkuu wa Mkoa wa Iringa, bibi. Amina Masenza amewatakia heri watahiniwa wote wa mitihani ya kidato cha sita mkoani Iringa na kuwataka kutokuwa na hofu na kufanya mitihani hiyo kwa kujiamini kwa kuzingatia yale yote waliyojifunza.

Mitihani wa kumaliza kidato cha sita na ualimu imeanza tarehe 04 Mei na itaendelea hadi tarehe 27 nchini kote.
=30=