Sunday, October 9, 2011

RASILIMALI ZA NCHI ZIWANUFAISHE WANANCHI

Serikali imeshauriwa kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi zinatumika kwa maslahi ya nchi na kuwanufaisha wananchi wenyewe walio wengi.
Ushauri huo umetolewa na Askofu mteule wa Dayosisi ya Kusini- Njombe, Askofu. Isaya Japhet Mengele katika ibada ya kumsimika na kumuingiza kazini msaidizi wa Askofu, Mch. Dk. George Mark Fihavango iliyoongozwa na Mkuu wa KKKT nchini Askofu. Dk. Alex Malasusa iliyofanyika katika kanisa kuu, Dayosisi ya Kusini Njombe.
Askofu. Mengele amesema kuwa rasilimali za nchi zinapogawanywa kwa maslahi ya nchi na wanufaikaji wakawa ni wananchi, nchi hutawaliwa kwa amani na utulivu. Aidha, ameshauri pia migodi itakayoanzishwa katika ukanda wa kusini mwa nchi, uanzishwaji, uratibu na usimamizi wake lazima uwe mzuri ili kuepusha migogoro inayoshuhudiwa katika ukanda wa kaskazini mwa nchi.
Akiongelea uhifadhi wa mazingira, amesema kuwa ni muhimu kwa Serikali na wadau wengine wote wa maendeleo na wenye mapenzi mema na nchi hii kutilia mkazo dhana ya uhifadhi wa mazingira ili kuinusuru nchi na uharibifu unaotokana na uharibifu wa mazingira ili nchi iwe mahali salama kwa ustawi wa binadamu wake.
Askofu mteule Mengele ameipongeza Serikali katika jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo na kusifu Serikali kutojiingiza katika masuala la kidini hali inayochangia ukuaji na ustawi wa uhuru wa kuabudu unaoendana na misingi ya kidemokrasia nchini.
Akimsimika rasmi, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Askofu. Dk. Alex Malasusa amewataka viongozi wa dini kutokutumia nafasi zao kwa maslahi ya kisiasa.
Katika salamu za Mkoa wa Iringa, zilizotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amempongeza Askofu mteule Mengele kwa uteuzi wake. Aidha, amewaomba viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla wao kukaa chini na kutafakari juu ya nchi na kuiombea ili iendelee kuwa na amani, upendo na utulivu.
Vilevile, Dk. Ishengoma imelishukuru kanisa la kiinjili la kilutheri Tanzania kwa michango na ushiriki wake katika kuiletea maendeleo jamii. Ameitaja michango hiyo kuwa ni pamoja na kuijenga jamii katika maadili na kuwafanya wananchi wake kuwa raia wema, mingine ni elimu na afya. 

No comments:

Post a Comment