Tuesday, August 6, 2013

DKT. CHRISTINE ISHENGOMA AITAKA TRA KUKAZA BUTI




Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma ameitaka Mamkala ya Mapato Tanzania kuongeza kasi ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali ili kuongeza wigo wa utoaji huduma nchini.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. christine Ishengoma (Mb.)

Kauli hiyo ameitoa katika majumuisho ya ziara ya Nanenane baada ya kutembelea mabanda ya maonesho likiwemo banda la mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) yaliyopo katika uwanja wa Mwakangale, Uyole Mbeya.


Dkt. Christine amesema kuwa mamlaka ya mapato Tanzania inafanya kazi nzuri, lakini bado inatakiwa kuongeza kasi katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali. Amesema kuwa Serikali bado inapoteza mapato mengi kwa sababu mamlaka hiyo haijakusanya mapato kiasi cha kutosha. Aidha, ameitaka mamlaka hiyo kuziba mianya yote ya upotevu wa mapato ya Serikali ili kuongeza wigo wa serikali katika kutoa huduma kwa wananchi wake.


Amesema kuwa katika kipindi hiki ambapo serikali inaendelea kutekeleza mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN) ni pamoja na kuongeza mapato ya ndani kwa ajili ya kuimarisha utoaji huduma kwa wananchi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu.


Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliyekuwa mgeni rasmi katika siku ya mkoa wa Iringa katika maonesho ya Nanenane, amewataka mamlaka ya mapato kuongeza kasi na mikakati ya kuwahamasisha wananchi kudai risiti wanaponunua bidhaa ili kuziba mwanya wa upotevu wa mapato ya Serikali. Katika kuimarisha elimu na hamasa kwa wananchi juu ya kudai risiti wanaponunua bidhaa, Dkt. Christine ametaka viongozi na wadau wote kushirikiana katika kutoa elimu hiyo. Amesema “jukumu hili si la TRA pekee, bali ni jukumu letu sote. 

Lazima viongozi wote na wadau mbalimbali kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kudai risiti”. Amesema kuwa kwa kufanya hivyo tutapunguza mwanya na hatimae kuondoa kabisa upotevu wa mapato ya serikali kwa njia hiyo.


Akiongelea hali halisi ya maonesho ya Nanenane baada ya kutembelea mabanda,, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu amepongeza jinsi Halmashauri na wadau walivyojipanga katika kuonesha bidhaa zinazozalishwa katika maeneo yao na shughuli mbalimbali zinazofanyika katika maeneo yao. Aidha, ametoa wito kwa washiriki wote kutumia maonesho hayo, si kuona tu, bali pia kujifunza juu ya matumizi ya teknolojia katika kukuza na kuboresha kilimo na mifugo.


Maonesho ya Nanenane mwaka 2013 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “zalisha mazao ya kilimo na mifugo kwa kulenga mahitaji ya soko”.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. chrisrine Ishengoma (mwenye kofia) na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Wamoja Ayubu wakipata maelezo katika Banda la TRA


=30=

No comments:

Post a Comment