Saturday, February 28, 2015

IRINGA YAONGEZA PATO LA MWANANCHI HADI TSHS. 1,660,532

Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkoa wa Iringa umepiga hatua katika kuongeza pato la mwananchi kufikia shilingi 1,660,532 mwaka 2013.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wakati akifanya majumuisho ya ziara yake ya siku sita Mkoani Iringa katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.
Mheshimiwa Pinda amesema kuwa pato la mwananchi wa Mkoa wa Iringa linakua vizuri, mwaka 2006 pato la mwananchi mmoja mmoja lililuwa shilingi 589,607 na limeongezeka hadi kufikia shilingi 1,660,532 mwaka 2013. “Nawapongeza wana Iringa kwa kuwa juhudi na uchapakazi ambao umeufanya Mkoa kufikia hatua hiyo na kuwa wa pili baada ya Dar es Salaam.” Alisema Mheshimiwa Pinda. Amesema kuwa pato hilo ni sawa na shilingi 138,377 kwa mwezi au shilingi 4,612 kwa siku.
Amesema kuwa viashiria vya kukua kwa uchumu ni pamoja na ujenzi wa nyumba za kisasa zenye umeme, elimu bora, afya bora na vifaa vya mawasiliano. Amesema kulingana na taarifa ya shirika la fedha Duniani, Tanzania imetoka miongoni mwa nchi 10 masikini Duniani na kwamba Tanzania ni miongoni mwa nchi 20 zenye uchumi unaokua kwa kasi kubwa.
Waziri Pinda ameutaka Mkoa wa Iringa wenye fursa kubwa ya ardhi nzuri kwa kilimo cha mazao ya chakula na biashara na hali ya hewa nzuri kutumia vizuri fursa hiyo. Amesema kuwa kuna fursa nyingine za kuwepo kwa kilimo cha umwagiliaji katika ukanda wa chini. Ameyasema hayo wakati Mkoa wa Iringa ukiwa na zaidi ya asilimia 80 ya wakazi wanaotegemea kilimo. Mheshimiwa Pinda amesema kuwa uzalishaji wa mazao ni mzuri na kuhakikisha kipo chakula cha nafaka ziada ya tani 1,032,613. Katika mwaka ulioishia 2013/2014, mavuno yalifikia tani 1,379,602 za mazao ya chakula na tani 77,622 za mazao ya biashara.
=30=



No comments:

Post a Comment