Sunday, May 31, 2015

RC IRINGA ATAKA HALMASHAURI ZIHAMASISHE MATUMIZI YA EFD



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza amezitaka Halmashauri kuhimiza matumizi ya mashine za kieletroniki za kodi (EFDs) kwa lengo la kuongeza mapato ya serikali.

Masenza amesema hayo alipokuwa akichangia katika taarifa ya Mpango na Bajeti ya Mkoa wa Iringa kwa mwaka 2015/2016 iliyowasilishwa na Kaimu Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Mipango na Uratibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga katika kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo, Manispaa ya Iringa.

Masenza amesema “umefika wakati kwa kila halmashauri kuhimiza na kuhamasisha matumizi ya mashine za kieletroniki za kodi katika kuongeza mapato ya serikali. Mapato ya serikali yanakwamishwa na wafanyabiashara wasio na nia njema ya kulipa kodi halali ya serikali kwa kukwepa kutumia mashine hizi’’. Amesema halmashauri zina wajibu wa kuwahamasisha wafanyabiashara kutumia mashine hizo katika biashara zao.

Amesema kuwa atashangaa kusikia halmashauri inatetea wafanyabiashara kutotumia mashine hizo. Amesema kwa kuwa serikali inatumia kile kinachokusanywa kujiendesha ni jukumu la jamii nzima kuhimiza matumizi ya mashine hizo. 

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu amesema pamoja na kuwa jukumu la kukusanya kodi ni muhimu sana kwa mustakabali wa serikali, kulipa kodi kwa hiari ni kitendo cha kizalendo. Ameitaka jamii kujivunia kulipa kodi kwa hiari hasa wafanyabiashara. Amesema kuwa halmashauri nyingi zinashindwa kujiendesha kutokana na mianya iliyopo katika ukusanyaji wa mapato ya serikali. 

Akiongelea umuhimu wa matumizi ya mashine hizo, Ayubu amesema kuwa mashine hizo zinauwezo mkubwa wa kutunza kumbukumbu za mauzo, manunuzi ya mali ya biashara bila kufutika kwa muda usiopungua miaka mitano na kuondokana na usumbufu wa kuchapisha vitabu vya risiti kwa kipindi chote hicho.
=30=

No comments:

Post a Comment