Saturday, December 16, 2017

KAMATI ZA UENDESHAJI MITIHANI MKOANI IRINGA ZAPONGEZWA KUDHIBITI UDANGANYIFU



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Kamati za uendeshaji wa mitihani ngazi za Wilaya na Mkoa zimepongezwa kwa usimamizi madhubuti wa mtihani wa kumaliza elimu ya msingi na kudhibiti udanganyifu.

Pongezi hizo zilitolewa na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi wa wanafunzi wanaotarajia kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2018 Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akifungua kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa jana.
 
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu
Ayubu alisema kuwa mwaka 2017 Mkoa wa Iringa haukukumbwa na tuhuma za udanganyifu. “Kipekee nazipongeza kwa dhati kamati za uendeshaji wa mitihani za Wilaya na ya Mkoa kwa usimamizi mzuri. Nitoe wito kuwa usimamizi huu uendelee  kwa mitihani ya kitaifa ya ngazi zote ili kuepukana na suala la udanganyifu ambalo kwa kiasi kikubwa madhara yake ni makubwa kwa mwanafunzi mwenyewe, mwalimu aliyehusika na udanganyifu na Taifa kwa ujumla” alisema Ayubu.

Akiongelea idadi ya wanafunzi waliofanya mtihani, alisema kuwa
watahiniwa 24,784 (wavulana 11,421 na wasichana 13,363) sawa na 99.5% walifanya mtihani. Aliongeza watahiniwa 20,606 (wavulana 9513 na wasichana 11,093) sawa na asilimia 83.14 wamefaulu mtihani huo. Alisema wanafunzi walioshindwa kufaulu mtihani huo ni 4,178 ikiwa wavulana 1,908 na wasichana 2,270 sawa na asilimia 16.86

“Kiwango cha ufaulu kimeongezeka kwa asilimia 0.27 ikilinganishwa na matokeo ya mwaka jana ambapo ufaulu ulikuwa ni 82.87%. Ninapenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza wadau wote wa elimu katika Mkoa wetu ambao mchango wao ni mkubwa kwa ongezeko hili la ufaulu na kuufanya Mkoa wetu kuwa wa Nne (4) kitaifa kati ya mikoa 26 ya Tanzania bara alisema Ayubu.

Mwaka 2017 Mkoa wa Iringa ulikuwa na watahiniwa 24,905 waliosajiliwa kufanya mtihani, wakiwemo wavulana 11,490 na wasichana 13,415 katika shule 481.
=30=

No comments:

Post a Comment