Thursday, February 17, 2011


...utafutaji kazi wachangia athari za afya kijamii

Uhamaji kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa minajili ya kutafuta kazi kwa ajili ya kujikimu ni miongoni mwa sababu za kijamii na kiuchumi zinazoathiri afya ya jamii nchini.

Hayo yameemwa na Samweli Nyagawa, Afisa Ustawi wa Jamii mkoa wa Iringa wakati akitoa mada juu ya Sababu za kiuchumi na kijamii zinazoathiri afya ya jamii, katika Taasisi ya Afya ya Msingi (PHCI)- Iringa.

Nyagawa amesema kuwa uhamaji kwa malengo ya kutafuta kazi umekuwa ukiwatenganisha wanaume na wake zao na kuvunjika kwa mtandao wa asili wa familia. Uhamaji huo unatokana na kukua kwa miji hali inayoambatana na upungufu au ukosefu mkubwa wa ajira ameongeza.

Uwezo finyu wa wanawake wa kiuchumi pia unachangia kuathirika kwa afya ya jamii. Kutokuwa na uwezo wa kiuchumi kwa wanawake kunawaondolea uwezo wa machanguo baina ya mahitaji yao na kujikuta wameingia katika mkumbo unaohatarisha afya zao.

Afisa Ustawi wa Jamii huyo ameelezea pia ukeketaji wanawake na kiwango kidogo cha utahiri kwa wanaume nazo ni sababu zinazochangia athari za kiafya kwa jamii. Amesema kuwa ukeketaji hufanyika katika mazingira yasiyosalama na kusababisha unyanyasaji kwa wanawake.

Aidha, amezitaja sababu nyingine kuwa ni pamoja urithi wa wajane, usafishaji wajane na ulevi wa kupindukia kuwa sababu zote hizo zinachangia athari za kiafya katika jamii hasa maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi

No comments:

Post a Comment