Monday, October 24, 2011

RC AAGIZA MATUMIZI MAZURI YA FEDHA ZA SERIKALI

MKUU wa Mkoa wa Iringa ameagiza matumizi mazuri ya fedha za serikali kadri zilivyopangwa ili ziweze kuwanufaisha wananchi walio wengi katika jitihada za kuondoa umasikini na kuinua maisha ya kila siku.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) katika kikao cha robo ya kwanza cha kudhibiti Mapato na Matumizi ya serikali katika ofisi yake kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ofisi yake. 

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. christine Ishengoma (Mb.)

Dk. Ishengoma aliyekuwa mwenyekiti wa kikao hicho amesema “lazima fedha za serikali zitumike vizuri kadri zilivyopangwa hasa upande wa miradi ya maendeleo ili ziwanufaishe wananchi wengi”.
Amesisitiza kufuatwa kanuni na taratibu za kihasibu ikiwa ni pamoja na ulipwaji wa madai mbalimbali kwa muda ili kuongeza ufanisi wa kazi na hatimae mkoa kupata hati safi ya kiukaguzi.

Aidha, Mkuu wa Mkoa ameagiza kufanyiwa kazi mapungufu yote yaliyobainishwa katika ripoti ya Mkaguzi na Mthibiti mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha 2009/ 2010 mapema na kuwasilisha taarifa hiyo sehemu husika na kuhakikisha mapungufu hayo hayajitokezi kwa mara nyingine. 

Akiwasilisha taarifa ya Mkaguzi wa Nje kuhusu mapungufu yaliyojitokeza katika ripoti ya Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 kwa mkoa wa Iringa, Mkaguzi Mkazi, Ismail Mbiru amesema kuwa ripoti hiyo imebaini mapungufu kadhaa yaliyoainishwa kwa kila Halmashauri kwa ajili ya kuyatolea majibu sahihi ili kuleta ufanisi katika kusimamia mapato ya Halmashauri.
Mbiru ameyataja mapungufu hayo kuwa ni pamoja na kuwasilisha taarifa zenye mapungufu makubwa, taarifa zenye nyaraka pungufu, taarifa za halmashauri ambazo fedha za mfuko wa maendeleo ya jimbo hazijatumika na kuwasilisha taarifa zenye hati zenye shaka.

Mapungufu mengine ameyataja kuwa ni kuwasilisha taarifa yenye wadaiwa wasiolipa na wasiolipwa, kuwasilisha taarifa zenye mishahara isiyolipwa na haikurejeshwa Hazina na kuwasilisha taarifa ya vitabu vya maduhuli ambayo hayajarejeshwa na mawakala wa kukusanya mapato.

No comments:

Post a Comment