Tuesday, September 17, 2013

SIETCO YAONGEZEWA MIEZI 6 KUKAMILISHA UJENZI WA BARABARA YA IRINGA- MIGORI




Serikali imemuongezea muda wa miezi sita mkandarasi anayejenga barabara ya Iringa-Migori ili aweze kukamilisha ujenzi huo na kukabidhi barabara hiyo serikalini. 
 
Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli (kushoto) na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (kulia) 
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli alipokuwa akifanya majumuisho ya ziara yake ya kukagua mradi wa barabara ya Iringa-Dodoma katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dk. Magufuli amesema kuwa Mkandarasi China Sichuan International Cooperation Company Limited (SIETCO) anayejenga barabara ya Iringa-Dodoma sehemu ya kwanza Iringa- Migori (km. 95.2) yupo nyuma, hivyo serikali imemuongezea miezi sita. 

Amesema kuwa baada ya kuongeza miezi hiyo mkandarasi huyo atatakiwa kukabidhi barabara hiyo kwa serikali mwezi Septemba, 2014. Akiongelea sababu zilizomfanya mkandarasi huyo awe nyuma, Dk. Magufuli amesema kuwa eneo la Nyang’oro lilikuwa na milima mikali na kuhitajika nguvu zaidi katika kuikata kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Amesema baada ya kipindi hicho mkandarasi lazima akabidhi barabara na hakuna muda wa ziada utakaoongezwa.

Kutokana na umuhimu wa kimkakati wa barabara ya Iringa- Dodoma yenye urefu wa km 260 utakapokamilika, Waziri wa Ujenzi ameshauri uandaliwe mpango wa kutengeneza barabara za michepuo. Amesema kuwa umuhimu wa barabara hizo za michepuo ambazo zitakuwa haziingii katikati ya mji zitaondoa msongamano wa magari katikati ya mji. Aidha, ameshauri itengenezwe stendi kubwa ya magari nje ya mji ili kupunguza msongamano wa magari mjini.

Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma ameishukuru serikali ya awamu ya nne chini ya uongozi wa Rais, Dk. Jakaya Kikwete kwa kuweka nguvu katika ujenzi wa miundombinu ya barabara nchini hasa mkoani Iringa. Amesema kuwa Mkoa wa Iringa utaendela kusimamia barabara zote ili ziweze kudumu kwa muda mrefu. Amesema kuwa serikali kupitia wizara ya Ujenzi inafanya kazi nzuri na wale wasiyoiona basi hawana macho alisisitiza Dk. Christine.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (kulia) akitoa shukrani. Kushoto ni Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa alitumia majumuisho hayo kumuomba Waziri wa Ujenzi kuiangalia kwa jicho la pekee barabara kuu ya TANZAM sehemu ya mlima Kitonga ipanuliwe ili kuondoa ajali za mara kwa mara na hadha kwa watumiaji wa barabara hiyo. Waziri Dk. Magufuli alilipokea ombi hilo na kuahidi kulitafitia ufumbuzi.

Mkataba wa ujenzi wa mradi wa barabara ya Iringa-Migori (km. 95.2) ulisainiwa tarehe 13 Januari, 2011 kati ya Tanroads na Mkandarasi China Sichuan International Cooperation Company Limited (SIETCO) kwa gharama ya shilingi 84.216 bilioni kwa utekelezaji wa miezi 35.
=30=


No comments:

Post a Comment