Thursday, June 9, 2011

BAJETI YAUJENZI WA VIWANJA VYA MICHEZO IRINGA

Halmashauri za Mkoa wa Iringa zimeshauriwa kutenga bajeti ya kutosha ya kuhudumia michezo hasa ujenzi wa viwanja vya michezo ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa viwanja hivyo.
Ushauri huo umetolewa na George Lukindo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Njombe, wakati akifungua rasmi mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa Sekondari Tanzania (UMISSETA) ngazi ya Mkoa yatakayopelekea kuundwa kwa timu ya UMISSETA ya Mkoa wa Iringa.
Lukindo amesema “upungufu wa viwanja vya michezo ni tatizo katika Mkoa wa Iringa kutokana na jiografia ya Mkoa wenyewe kutokuwa na maeneo mengi tambalale hivyo nazishauri Halmashauri za Mkoa huu zipange bajeti ya kutosha kwa shule kadhaa ili kujenga viwanja vya michezo”. Amesema huwezi kuongelea kuinua sekta ya michezo katika ngazi yoyote kama hutakuwa na viwanja vya kutosha na vilivyo katika ubora unaostahili kwa michezo husika.
Akiongelea ufinyu wa bajeti ya michezo ya UMISSETA, Lukindo amezishauri Halmashauri kuangalia uwezekano wa kuongeza fedha za ziada ili kufidia upungufu unaojitokeza.
Akisisitiza suala la nidhamu amesema mchezaji asiye na nidhamu UMISSETA si mahali pake. Amesema “mchezaji asiye na nidhamu hata kama atakuwa ni mzuri kiasi gani asiingizwe katika timu ya Mkoa”.
Wakati akimkaribisha mgeni rasmi kufungua mashindano ya UMISSETA, Mwenyekiti wa UMISSETA Mkoa wa Iringa ambae pia ni Afisa Elimu Mkoa, Joseph Mnyikambi amesema kuwa michezo ni upendo, furaha na msikamano na kusisitiza kuwa katika kipindi chote cha mashindano hayo suala la nidhamu lipewe umuhimu wa pekee. Vilevile, amewaasa wanamichezo kuwa wanapokuwa uwanjani lazima watarajie na kukubali kushinda, kutoka sare au kushindwa.
Katika risala iliyoandaliwa na UMISSETA Mkoa na kusomwa na Upendo Mdzovela iliainisha changamoto zinazoikabili michezo ya UMISSETA kuwa ni pamoja ufinyu wa bajeti inayotengwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi. Aidha, changamoto nyingine ni upungufu wa walimu wenye taaluma ya michezo na vifaa vya michezo na upungufu wa viwanja vya michezo.
Mechi za ufunguzi zilizofana sana kwa kuzishindanisha timu za mpira wa miguu ya Halmashauri ya Mji Njombe wasiosikia (viziwi) na timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa ambapo Ludewa waliibuka kidedea kwa ushindi wa 1-0. Katika mechi nyingine ya mpira wa pete timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa iliibwaga timu ya Wasiosikia ya Halmashauri ya Mji Njombe kwa mabao 7-3.

No comments:

Post a Comment