Thursday, June 9, 2011

VYUO VIONGEZA MAPATO KWA KUANZISHA MIRADI

Vyuo vya Maendeleo ya Jamii vimetakiwa kufikiria mikakati ya kuongeza mapato kwa kupitia miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujielekeza katika mahitaji ya msingi ya jamii inayovizunguka.
Rai hiyo imetolewa na Ummy Ally Mwalimu, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto alipotembelea chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Ruaha kilichopo katika Manispaa ya Iringa.
Mwalimu amesema “lazima mfikirie jinsi ya kuongeza mapato kwa kupitia miradi mbalimbali na mahitaji ya jamii ili muweze kuongeza mapato ya chuo”. Amesema vyuo vikiweka mkakati wa kuongeza mapato vitaweza kutatua matatizo yaliyo ndani ya uwezo wa vyuo husika badala ya kuisubiri Serikali kufanya kila kitu. Aidha, amevishauri vyuo vya maendeleo ya wananchi kuangalia fursa na vikwazo vilivyopo katika jamii na kuandaa programu za kuisaidia jamii. Ametolea mfano kuazisha programu za kuwawezesha kinamama kuondokana na umasikini na kujitegemea na programu za elimu ya ujasiliamali.
Naibu Waziri amehimiza kuendeleza na kudumisha ushirikiano baina Mkoa, Halmashauri na vyuo hivyo ili jamii iweze kunufaika na huduma zitolewazo kwasababu wote wanategemeana.
Awali alitembelea shule ya sekondari wasichana ya Iringa na kuongea na wasichana kwa minajili ya kuhamasisha maendeleo na usawa wa kijinsia na kuwatia moyo wanafunzi hao.
Kaimu Mkuu wa chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha, Gaspar J. Msigala alizitaja baadhi ya changamoto zinazokikabili chuo hicho kuwa ni pamoja na upungufu wa miundombinu ya kitaaluma jambo linalosababisha udahili wa wanafunzi wachache ukilinganisha na uhitaji wa wanafunzi wanaotuma maombi na kuwa na sifa. Aidha, mkakati wa awali uliotumika kukabiliana na changamoto hiyo ni pamoja na kugawa wanafunzi katika awamu mbili za masomo yaani wanaoanzi asubuhi na wengine jioni.
Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto yupo katika ziara ya kikazi ya siku nne Mkoani hapa kutembelea vyuo maendeleo ya jamii na vyuo vya maendeleo ya wananchi kuzifunza fursa na changamoto zilizopo, kuongea na watumishi na kuongeza hamasa ya kimaendeleo.
Chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha kipo kilometa tatu kutoka Iringa mjini na kilianza mwaka 2007 baada ya kubadilishwa toka chuo cha maendeleo ya wananchi.    

No comments:

Post a Comment