Thursday, June 9, 2011

MKOA WA IRINGA WAIBUKA MSHINDI WA USAFI NA MAZINGIRA

Mkoa wa Iringa umepongezwa kwa kuibuka mshindi wa jumla katika mashindno ya afya na usafi wa mazingira nchini na kupata zawadi ya kombe na kutakiwa mikoa mingine kuiga mfano huo ili mikoa yote iwe na mazingira safi na salama.
Hayo yamesemwa na mgeni rasmi, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , Mhe. Mizengo Pinda katika utoaji zawadi kwa washindi wa shindano la afya na usafi wa mazingira, aliyewakilishwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Kajumulo Tibaijuka  kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani kitaifa yaliyofanyika mjini Songea.
Katika mashindano hayo ya afya na usafi wa mazingira yaliyoratibiwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Halmashauri za Manispaa (Iringa), Mji (Njombe) na Wilaya (Njombe) zimekuwa mshindi wa tatu (Manispaa ya Iringa), wa pili (Mji Njombe), na wa kwanza (Wilaya ya Njombe) katika ngazi ya Halmashauri za Manispaa, Miji na Wilaya.
Kitaifa Halmashauri ya Jiji la Mwanza ndiyo mshindi kati ya majiji matatu yaliyoshindanishwa. Kwa upande wa Halmashauri za Manispaa jumla ya Manispaa 17 zilishindanishwa na Manispaa ya Moshi iliibuka msindi ikifuatiwa na Arusha na Iringa. Upande wa Halmashauri za Miji jumla ya Halmashauri sita zilishindanishwa na Mpanda iliibuka mshindi ikifuatiwa na Njombe. Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ilizishinda Halmashauri za Meru (namba mbili) na Rungwe (namba tatu). 
Mkoa wa Iringa umeibuka mshindi wa jumla wa mashindano ya Afya na Usafi wa Mazingira baada ya Halmashauri zake tatu za Iringa, Mji Njombe na Wilaya ya Njombe kushinda katika nafasi tofauti.
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani huadhimishwa kitaifa kila mwaka tarehe 5 Juni na mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo ‘panda miti na kuitunza: hifadhi mazingira’ mkoani Ruvuma katika Manispaa ya Songea. Maadhimisho haya kimataifa yamefanyika katika miji ya Delhi na Mumbai nchini India.

No comments:

Post a Comment