Thursday, August 9, 2012

MPAKA AWATAKA MPANDA KUPANDA MITI




 Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka ameshauri upandaji wa miti kwa wingi sana ili kuepukana na tatizo la wilaya hiyo kugeuka jangwa kutokana na matumizi makubwa ya kuni katika kukausha zao la tumbaku linaloendelea kushamiri katika wilaya ya Mpanda mkoa mpya wa Katavi.

Ushauri huo ameutoa alipotembelea banda la wilaya ya Mpanda katika uwanja wa maonesho ya Nanenane wa John Mwakangale- Uyole Mbeya.

Gertrude amesema kuwa kutokana na matumizi makubwa ya kuni zinazotumika katika kukaushia zao la tumbaku, ni vizuri wilaya hiyo ikajipanga katika kupanda miti kwa wingi ili kuziba pengo la miti inayokatwa kwa ajili ya matumizi ya kuni katika kukaushia tumbaku. Amesema kuwa ni vema mkakati huo ukaanza mapema wakati njia mbadala ya nishati ya ukaushaji wa tumbaku ikiangaliwa ili kutokuteketeza misitu na mazao yake.

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka alipotembelea banda la Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda 

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, amesema njia za kisayansi zinahitajika katika kukausha majani ya tumbaku pasipo kuharibu mazingira. Aidha, ametoa wito wananchi kufikiria njia ya kiteknolojia itakayotumika katika ukaushaji wa majani hayo. Amesema kwamujibu wa kaulimbiu ya maonesho ya Nanenane mwaka 2012 isemayo “Kilimo kwanza, zalisha kisayansi na kiteknolojia kukidhi mahitaji ya ongezeko la idadi ya watu” vivyo hivyo wilaya ya Mpanda ifikirie hamasa ya maendeleo ya kiteknolojia katika kulifanya zao la tumbaku kuwa na tija zaidi katika ustawi wa wananchi na mazingira kwa ujumla wake.

Gertrude amesema kuwa ili kwenda sambamba na kauli mbiu hiyo, ni vizuri wilaya hiyo ikatoa hamasa zaidi katika utengenezaji wa zana zitakazosaidia katika kukipeleka mbele kilimo. Amesema kuwa wapo vijana wengi wanaoibuka na ubunifu wao kwa kutumia teknolojia rahisi wanaohitaji kupewa msukumo na kuendelezwa ili kuweza kuleta mapinduzi katika kilimo na ufugaji.

Akiongelea changamoto inayowakabili wanawake wajasiriamali katika upatikanaji wa masoko, Katibu Tawala Mkoa wa Iringa ametoa wito kwa wanawake wajasiriamali kuungama pamoja na kuunganisha nguvu zao katika shughuli zao za ujasiliamali. Amesema masoko ni changamoto inayowakabili wakina mama wengi wajasiriamali, na kushauri pindi wanapokuwa katika vikundi ni rahisi kwao kuweza kupatiwa mafunzo ya mbinu za upatikanaji wa masoko ya ndani na nje ya nchi.

Amesema umefika wakati kwa wanawake wa Nyanda za Juu kusini kuungana na kutumia fursa iliyopo sasa ya soko pana la Afrika ya Mashariki.
=30=

No comments:

Post a Comment