Thursday, August 9, 2012

WILAYA ZATAKIWA KUJIFUNZA KILOLO


Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Gerald Guninita ametoa wito kwa wilaya nyingine kuitembelea wilaya yake kwa lengo la kujifunza mikakati inayowawezesha kulima kwa ubora na uhifadhi wa mazingira.
Kauli hiyo ameitoa alipofanya mahojiano na gazeti hili katika banda la Wilaya ya Kilolo lililopo katika uwanja wa Maonesho wa John Mwakangale Uyole, Jijini Mbeya.

Guninita amesema kuwa wilaya yake imegawanyika katika ukanda wa juu unaohusisha tarafa ya Kilolo wenye miinuko na mabonde jambo linalofanya ugumu katika matumizi ya zana bora za kilimo kama powatila na matrekta.

Amesema ukanda wa chini wenye tarafa za Mazombe na Mahenge una maeneo ambayo ni tambarare pamoja na kuwa na ukame maeneo hayo yanafaa kwa matumizi ya zana bora za kilimo yakiwemo matrekta.

Guninita amesema pamoja na changamoto hiyo ya kijiografia na mabadiliko ya tabia nchi, bado wilaya yake inajivunia utaratibu wa wananchi wake wa kutunza mazingira hasa utunzaji wa vyanzo vya maji. Amesema utunzaji huu wa vyanzo vya maji una mchango mkubwa katika shughuli za kilimo jambo linalowawezesha wakulima wa wilaya hiyo kuweza kulima kwa mwaka mzima. Ameyataja mazao yanayolimwa zaidi kuwa ni maharage, njegere, mahindi, mbogamboga, magimbi, muhogo, na viazi mviringo.

Mkuu wa Wilaya ya Kilolo amesema kuwa wilaya yake imefanikiwa katika uhifadhi wa mazingira kwa uongozi wa wilaya kwa kushirikiana na wadau wengine kuwekeza katika elimu ya uhifadhi wa mazingira. Amesema katika ziara zake za kutembelea wilaya yake baada ya uteuzi wake mapema mwaka huu, katika kata zote 22 alizotembelea amekuwa akisisitiza utunzaji wa mazingira na uhifadhi wa vyanzo vya maji. Aidha, wananchi wamehamasishwa kuacha vitendo vya uchomaji moto miti ya asili na misitu ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

Mkakati mwingine ameutaja kuwa ni wananchi kuhamasishwa katika ulinzi shirikishi unaohusika katika kulinda misiti na hifadhi ya mazingira. Amesema “katika hili la uhifadhi wa mazingira baada ya kutoa elimu na hamasa wale wote watakaobainika watafikishwa katika mkondo wa sheria. Tumekuwa tukisisitiza sana Sheria ya Uhifadhi wa Mazingira ya mwaka 2004, inayotoa adhabu isiyopungua sh. 2,000,000, kifungo cha miaka mitatu au vyote kwa pamoja.

Akiongelea tuzo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya utunzaji wa Mazingira kwa wilaya yake ya kilolo, Guninita amesema “katika kudhihirisha tabia ya uhifadhi wa mazingira kwa wilaya ya Kilolo, wilaya yetu imekuwa mshindi wa kwanza kitaifa. Kata ya bora ni Bomalang’ombe na taasisi bora imetoka katika wilaya yetu nayo ni gereza la Kihesa Mgagao”.

Amesema tuzo hiyo ya Rais, imeendelea kuamsha ari kwa wilaya yake, kuendelea kuhamasisha upandaji miti na uhifadhi wa mazingira. Ameitaja kampuni ya New Forest kuwa nayo inachangia kutoa hamasa kwa wananchi ya kupanda miti kwa wingi na kujiongezea kupato.

Mkuu huyo wa Wilaya amesema kuwa katika kuhakikisha mkulima wa Kilolo anaendelea kuwa na lishe nzuri, wilaya yake imeendelea kuhamasisha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa. Amesema katika kuhakikisha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa unashika kasi, wananchi wamehamasishwa kuzitumia rasilimali walizonazo kufuga kisasa na ufugaji wenye tija. Amesema ufugaji wa kisasa na wenye tija ni ule wa ng’ombe wachache ambao mfugaji anaweza kuwahudumia vizuri na kuepuka mfugaji kuwa mtumwa kwa ngo’mbe wake.

Amesema Halmashauri yake kupitia DADPs imekuwa ikifanya vizuri katika hilo na ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma imeamsha ari zaidi ya ufugaji wa ng’ombe wa maziwa wilayani hapo.
=30=

No comments:

Post a Comment