Thursday, August 9, 2012

SERIKALI YABUNI MIKAKATI YA KUKUZA KILIMO



Serikali imeendelea kubuni na kutekeleza mikakati mbalimbli ya kwa lengo la kuhakikisha kuwa taifa linakuwa na chakula cha kutosha kwa wananchi wake na ziada kwa ajili ya watu wengine.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika kilele cha sikukuu ya wakulima na maonesho ya Nanenane mwaka 2012 yaliyofanyika kikanda katika viwanja vya Maonesho ya kilimo vya John Mwakangale Jijini Mbeya.
 Mgeni rasmi katika kilele cha Maonesho ya Nanenane Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Dr. Christine Ishengoma alipotembelea banda ya Halmashauri ya Wilaya ya Iringa

Katika hotuba yake, Dkt. Christine amesema “katika jitihada za taifa letu za kujitosheleza kwa chakula, mikakati mbalimbali imeendelea kubuniwa na kutekelezwa ikiwa ni pamoja na kanda ya Nyanda za Juu Kusini kupewa jukumu la kuzalisha mazao ya chakula kwa wingi na kuwa ghala la chakula la Taifa kutokana na fursa nzuri za uzalishaji zilizopo hatika mikoa hii”.

Amesema ili jukumu hili la kitaifa lifanikiwe ni lazima wakulima wazalishaji wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kutumia vizuri fursa zilizopo, kuzalisha kwa tija kwa kutumia kanuni bora za kilimo zitakazowawezesha kupata ziada ya chakula ya kuuza kwa mikoa mingine isiyokuwa na firsa nzuri za uzalishaji.

Akiongelea viwanzo tija vya uzalishaji wa mazao ya chakula, Dkt. Christine amesema “..viwango vya tija katika uzalishaji wa mazao ya chakula kwa eneo bado viko chini. Takwimu zinaonesha kuwa, katika Nyanda za Juu Kusini uzalishaji wa mahindi kwa mfano, ni kati ya tani 2-3 kwa hekta moja wakati ambapo utafiti unaonesha kwamba hekta moja inaweza kuzalisha hadi tani 7”.Aidha, ametoa wito kwa viongozi na wakulima kuyatumia maonesho hayo kama jukwaa la kuwajengea uwezo wazalishaji wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kuongeza tija na kufikia uwezo wa juu katika uzalishaji kadri inavyowezekana.

Akiongelea ufugaji, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, amesema kuwa kanda hiyo ina fursa ya ufugaji kutokana na uwepo wa ardhi, mvua za kutosha, miundombinu ya machinjio ya kisasa na rasilimali kubwa ya mifugo. Amesema mifugo imekuwa ikichangia katika uzalishaji wa mazao ya kilimo kwa njia ya nguvu kazi na samadi. Amesema “katika kanda hii, asilimia 70 ya wakulima hutumia wanyamakazi katika shughuli za kilimo. Hii ni hatua kubwa inayostahili kupongezwa kwani matumizi ya nguvukazi ya wanyama ni moja kati ya teknolojia rahisi, sahihi na endelevu kwa wakulima wetu”.

Ikumbukwe kuwa sekta ya kilimo nchini inatoa ajira kwa karibia asilia 80. Vilevile, wakazi karibu asilimia 90 wa kanda ya Nyanda za Juu Kusini wanategemea kilimo kama shughuli kuu ya kiuchumi kwa mazao ya chakula na biashara.

=30=

No comments:

Post a Comment