Sunday, December 19, 2010

...MADIWANI UNGANISHENI NGUVU KUWALETEA WANANCHI MAENDELEO

Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi wamekumbushwa kuwa wanalo jukumu la msingi la kuunganisha nguvu na kuwaletea maendelea wananchi wao kupitia Ilani ya chama kilichopo madarakani na kuacha siasa za chuki na kupakana matope.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Evarista Kalalu wakati wa kufungua mafunzo ya awali kwa Waheshimiwa Madiwani wa Halmashauri ya Mufindi kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.

Kalalu amesema kuwa jukumu lililo mbele yao ni ni kuitekeleza Ilani ya uchaguzi ya chama kilichopo madarakani ili kuweza kuunganisha nguvu katika kuwaletea maendeleo wananchi waliowachagua. Aidha amesisitiza kuwa kipindi cha kampeni na ushindani wa vyama vya siasa kimemalizika baada ya uchaguzi mkuu, na kuwataka kuacha siasa za kupakana matope, chuki na fitina.

Mkuu huyo wa Wilaya ya Mufindi amewakumbusha Waheshimiwa Madiwani kuzingatia kuwa baada ya miaka mitano ya kuwawakilisha wananchi katika Kata zao watawajibishwa kutokana na kazi moja ya jinsi gani alisshiriki kuwaongoza wananchi wake katika kujiletea maendeleo.

Akielezea umuhimu wa mafunzo hayo amesema kuwa yatasaidia kuondoa migogoro inayotokana na muingiliano wa majukumu katika mipaka ya kiutendaji baina yao na Halmashauri wanayoiongoza. Ameongeza pia kuwa mafunzo hayo yataondoa migogoro baina ya wananchi wanaowakilishwa na Halmashauri husika.

Mafunzo hayo ya Waheshimiwa Madiwani yameandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na kusimamiwa na kuendeshwa na wataalamu wa Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa.