Saturday, November 17, 2012

RC AKEMEA UKWEPAJI KODI


Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewataka wananchi kuachana na tabia ya kukwepa kulipa kodi na kuwa wazalendo kwa mkoa wao na Taifa lao kwa ujumla wakati akikemea tabia ya wafanyabiashara wanaokwepa kutumia mashine za kieletroni za kutolea risiti.


Mkuu wa Mkoa amesema hayo katika hotuba yake kwenye maadhimisho ya siku ya mlipakodi iliyofanyika katika ukumbi wa chuo kikuu huria tawi la Iringa iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Dkt. Leticia Warioba.

Dkt. Warioba amesema “bado wapo walipakodi ambao sio wazalendo.Walipakodi ambao mpaka sasa wanakwepa kodi. Tabia hii ya kukwepa kodi siyo ya kizalendo na ningependa kuwaasa muiache mara moja”. Amesema kuwa ukadiliaji na ukusanyaji wa kodi vinafanyika kwa mujibu wa sheria za kodi na ni muhimu kwa kila mlipa kodi kuheshimu sheria na taratibu nchi ilizojiwekea.

Amesema tabia ya kukwepa kodi imekuwa ikiwafanya wafanyabiashara kupitisha bidhaa vichochoroni badala ya kupitisha bidhaa hizo kwenye ofisi za forodha zilizopo mipakani. Amesema kuwa utaratibu huo unafanyika kinyume na sheria za nchi na kutaka tabia hiyo iachwe mara moja.

Akiongelea matumizi ya mashine ya kieletroniki za kutolea risiti, Dkt. Leticia amesema “matumizi ya mashine hizo ni changamoto katika utendaji kazi wa Mamlaka ya Mapato nchini, ningependa kuwafahamisha kuwa, matumizi ya mashine hizi ni agizo la Serikali na lengo lake ni kuhakikisha kodi ya ongezeko la thamani inakusanywa ipasanyo”.

Amewataka wale wote waliosajiliwa na kodi ya ongezeko la thamani kutumia mashine za kieletroniki za kutolea risiti kwa kila mauzo wanayofanya. Amesema kuwa mashine hizo zinatumika kwa mujibu wa sheria ya bunge hivyo utekelezaji wake ni lazima.

Wakati huohuo, Mamlaka ya Mapato Mkoa wa Iringa imefanikiwa kuvuka lengo kwa kukusanya zaidi ya asilimia 100 ya lengo iliyowekewa la idara ya ushuru wa forodha na kodi za ndani. Katika maelezo ya Meneja wa mamlaka ya mapata Mkoa wa Iringa, Rozalia Mwenda amesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2011/2012 Mkoa wa Iringa ulipangiwa kukusanya jumla ya shilingi  23,761,800,000/= lengo la idara ya ushuru wa forodha likiwa shilingi 110,100,000/= na lengo la idara ya kodi za ndani likiwa shilingi 23,651,700,000/=. Amesema kwa kipindi hicho Mkoa ulikusanya shilingi 24,730,752,185 sawa na asilimia 105 ya utendaji.

Akiongelea ubora wa huduma kwa wateja, Rozalia amesema “mamlaka ya mapato makao makuu, mikoani hadi wilayani, inatekeleza sera ya ubora ambayo inaelekeza utendaji kazi wenye lengo la kutoa huduma bora inayokidhi na hata kupita matarajio ya mteja”. Amesema “baada ya kufanyika  kwa ukaguzi wa ubora wa huduma zetu na kampuni ya wakaguzi wa nje, mamlaka ilitunukiwa cheti cha kimataifa cha ubora wa viwango cha ISO 9001:2008”. Amesema kuwa mamlaka yake imepanga kutathmini mara kwa mara viwango vya huduma tunazotoa kwa walipa kodi ili kuhakikisha kuwa mahitaji ya walipakodi yanazingatiwa katika mipango ya mamlaka ya kimkakati.

Amesema kuwa mamlaka yake inaendeleza ushirikiano baina yake na mlipakodi kwa lengo la kudumisha ushirikiano wa kulipa kodi kwa mujibu wa sheria kwa kutoa huduma bora. Amesisitiza kuwa urafiki baina mamlaka na mlipakodi sharti uongeze tija katika kukusanya mapato ya Serikali kwa lengo la kutokumuumiza mlipa kodi na wala Serikali.

Meneja wa mamlaka ya mapato mkoa wa Iringa ameahidi kuongeza juhudi katika utendaji kazi, amesema “mimi na wafanyakazi  wa mamlaka ya mapato Mkoa wa Iringa tunaahidi kuongeza, juhudi, maarifa na uadilifu katika kuhakikisha tunavuka malengo tuliyopangiwa kama tulivyokwishaonesha kipindi kilichopita. Kwa mshikamano na mikakati tuliyonayo, tunaamini malengo ya mwaka 2012/2013 ambayo ni shilingi 33.4 bilioni yanafikiwa”.

Wiki ya maadhimisho ya 6 ya sherehe ya mlipakodi kitaifa ilianza tarehe 01-07 Novemba, 20122 ikiongozwa na kaulimbiu isemayo “ulipaji kodi wa hiari Kwa Taifa lenye mafanikio” ikiwa na lengo kuu la kuboresha huduma kwa mlipakodi.
=30=



MKOA WA IRINGA WAZIDI KUFANIKIWA KATIKA SEKTA YA KILIMO
Mkoa wa Iringa umeendelea kupata mafanikio makubwa katika Sekta ya Uchumi na Uzalishaji mali kwa kuongeza matumizi ya zana za kilimo hadi kufikia asilimia 15 kwa wakazi wa Mkoa huo.

 Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa Scolastica Mlawi akifafanua jambo.

Mafanikio hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Scolastica Mlawi wakati akifungua kikao cha siku mbili cha kupitia taarifa za uekelezaji wa kazi za Sehemu ya uchumi na sekta za uzalishaji na kuainisha vipaumbele kwa mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Scolastica amesema “mafanikio kwa upande wa sekta ya kilimo ni pamoja na ongezeko la matumizi ya zana za kilimo ambapo kwa sasa asilimia 15 ya wakazi wa mkoa huu wanatumia matrekta makubwa na madogo katika Kilimo”. Amesema asilimia 20 ya wakazi wanatumia wanyamakazi na asilimia 65 wanatumia jembe la mkono ikilinganishwa na asilimia 75 ya wakulima waliokuwa wanatumia jembe la mkono mwaka 2005.

Kaimu Katibu Tawala Mkoa amesema kuwa pato la mkoa wa Iringa limeongezeka toka Sh. 867,482 mwaka 2005 hadi kufikia Sh. 1,985,708 mwaka 2011, wakati pato la mkazi mwaka 2005 lilikuwa Sh. 558,444 na limeongezeka hadi kufikia Sh. 1,125,503 mwaka 2011.
Akiongelea maandalizi ya kilimo msimu huu, amesema kuwa msimu wa kilimo umeanza na wakulima wameonesha jitihada kubwa katika kulima na kupanda mazao mbalimbali ya chakula na biashara.

Amesema “msimu huu tunajipanga zaidi katika kuhimiza mazao yanayostahimili ukame kama vile alizeti, mtama, muhogo na viazi vitamu. Kwa pamoja tuhimize kilimo cha mazao haya katika maeneo yote yenye ukame (upungufu wa mvua) katika wilaya zote hasa wilaya ya Iringa (Tarafa ya Idodi, Isimani na Pawaga), wilaya ya Kilolo (Tarafa ya Mahenge na Mazombe) wilaya ya Mufindi (Tarafa ya Sadani na Malangali)”.

Akiongelea ufanisi wa kilimo Scolastica amesema “ili kilimo chetu kiweze kufanikiwa vizuri tunahitaji kuwaelimisha wakulima wetu mbinu bora za kilimo ikiwemo matumizi bora na sahihi ya pembejeo za Kilimo”.

Awali Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Sekta ya Uchumi na Uzalishaji, Adam Swai alisema kuwa lengo la kikao hicho ni kutoa taarifa za utekelezaji wa kazi kutoka katika Halmashauri za wilaya ili kujadili tathamini, matokeo na kubadilishana uzoefu wa shughuli na kutoa ushauri wa pamoja katika  kuboresha utekelezaji wa shughuli na kupata takwimu halisia katika sekta ya uchumi. Aidha, amesema kuwa kikao hicho kitasaidia katika kuandaa taarifa ya Mkoa itakayoonyesha vipaumbele vichache ambavyo vitaleta matokeo na mafanikio.
=30=