Wednesday, November 28, 2012

CHANJO YA MPYA KUZINDULIWA JAN, 2013




Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma ametoa wito kwa wananchi kuondokana na hofu pale chanjo ya mpya za magonjwa ya kuhara na nimonia zitakapoanzishwa mkoani Iringa.

Rai hiyo ameitoa alipokuwa akifungua kikao cha kamati ya huduma ya afya ya msingi Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.


Dkt. Christine amesema kuwa mara nyingi chanjo mpya zinapoanzishwa wananchi wanakuwa na hofu na minong’ono mbalimbali. Amesema “napenda kuwahakikishia wananchi kuwa chanjo hizi ni salama na zimefanyiwa utafiti wa kina, hivyo ni salama kwa matumizi ya binabamu”. Aidha, ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuwapeleka watoto wao kupatiwa chanjo hizo ili kuweza kupunguza na hatimae kuondoa kabisa vifo vya watoto wadogo.

Akiwasilisha mada juu ya kuanzishwa kwa chanjo mpya za “Rotavirus na Pneumococcal” Mratibu wa huduma za chanjo Mkoa wa Iringa, Naftal Mwalongo amesema kuwa chanjo ni moja kati ya afua madhubuti na nafuu za kuzuia magonjwa na vifo. Amesema chanjo inazuia magonjwa, ulemavu na inaokoa mamilioni ya watoto kila mwaka.

Akiongelea nafasi ya chanjo katika utekelezaji wa malengo ya milenia, Mwalongo amesema “chanjo ni afua muhimu kufikia lengo namba nne la milenia la kupunguza vifo vya watoto  chini ya mwaka mmoja ifikapo 2015”.

Mwalongo amesema kuwa hali ya ugonjwa wa kuharisha kwa Mkoa wa Iringa mwaka 2010-2011, idadi ya wagonjwa wa kuharisha chini ya miaka mitano kwa mwaka 2010 ilikuwa ni 35,424 sawa na asilimia 12 kati ya wagonjwa waliopata matibabu ya nje na mwaka 2011 idadi ya wagonjwa wa kiharisha chini ya miaka mitano ilikuwa 34,941 sawa na asilimia 11 kwa wagonjwa waliopata matibabu ya nje.

Amesema kuwa chanzo cha ugonjwa wa kuharisha ni kula au kunywa maji yaliyochafuliwa na kinyesi chenye virusi. Aidha, amesema kuwa muda wa uambukizo hadi dalili kujitokeza ni kati ya saa 24 hadi 48. Amesema kundi linaloathirika zaidi ni watoto chini ya umri wa miaka miwili.

Mratibu wa huduma za chanjo Mkoa wa Iringa, amezitaja dalili za ugonjwa wa kuhara kuwa ni kuharisha, kutapika, kupungukiwa maji na chumvi mwilini na mara chache huambatana na homa.

Amesema kinga yake ni pamoja na kunyonyesha mtoto maziwa ya mama pekee na kuimarisha usafi wa mazingira. Kinga nyingine ameitaja kuwa ni kuimarisha usafi wa mtu binafsi kwa kunawa mikono kwa sabuni na nyongeza ya virutubishovya Zinc huchangia katika kupunguza kuenea kwa Rotavirus, pamoja na kupatiwa chanjo ya Rotavirus.

Kikao hicho kilichojumuisha maafisa waandamizi, viongozi wa dini, waandishi wa habari na watu maarufu, wataalamu toka sekta ya afya kilikuwa na lengo la kutoa uelewa wa pamoja kwa ajili ya kuwaelimisha wananchi juu ya chanjo hizo zitakazoanza mapema mwezi Januari, 2013.
=30=