Tuesday, March 17, 2015

UTUNZAJI MAZINGIRA NI MUHIMU KUENDELEZA RASILIMALI MAJI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Tabia ya utunzaji wa mazingira imeelezwa kuwa ni muhimu katika kuendeleza rasilimali maji mkoani Iringa.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bw. Adam Swai katika hotuba yake ya uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji katika mkoa wa Iringa yaliyofanyika katika Kata ya Ruaha, Manispaa ya Iringa. 
Bw. Swai amesema “utunzaji wa mazingira ni kitu muhimu katika kuhakikisha uendelevu wa rasilimali maji. Sote tunafahamu kuwa rasilimali maji ni muhimu kwa maisha na maendeleo ya binadamu zikiwepo shughuli za kiuchumi. Bila maji hakuna maendeleo na bila maendeleo hakuna maji,”. 

Akiongelea kusuasua kwa ujenzi wa miradi ya maji, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia kikamilifu ujenzi wa miradi ya maji. Aidha, amewataka kuwapatia kazi makandarasi na wataalamu washauri wenye uwezo na sifa za kufanya kazi zenye ubora. Amewataka kujiridhisha na uwezo wa makandarasi kabla ya kuwapatika kazi juu ya ubora wa utendaji kazi wao ili miradi ikamilike kwa wakati.

Akiongelea juhudi za kuongeza upatikanaji huduma ya maji mijini na vijijini, ameshauri kutumia teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua. Ameongeza utumiaji wa teknolojia ya nguvu ya jua na nguvu ya upepo katika kusukuma maji katika ngazi ya kaya na taasisi kutokana na urahisi wa teknolojia hizo.

Akiongelea hali ya upatikanaji huduma ya maji mkoani Iringa, Mhandisi wa Maji Mkoa wa Iringa, Mhandisi Shaban Jellan amesema kuwa hadi kufikia Disemba, 2014, idadi ya watu waliokuwa wakipata huduma ya maji ndani ya umbali usiozidi mita 400 toka kwenye makazi yao ni 651,917 sawa na 69.3% ya wakazi wote wa Mkoa wa Iringa.

Akiongelea huduma ya maji vijijini, amesema kuwa wakazi wa vijijini wanaopata huduma ya maji ni 452,524 sawa na 66.1% ya wakazi wote waishio vijijini. Ameitaja idadi ya wanaopata huduma ya maji kwa kila Halmashauri kuwa ni 90% sawa na wananchi 14,213 katika Halmashauri ya Manispaa (vijijini-peri-urban), 69% sawa na wananchi 175,282 katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ni 60.8% sawa na wananchi 93,722 na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi 64.8 sawa na wananchi 172,258 wanaopata huduma ya maji. 

Maadhimisho ya wiki ya maji mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu isemayo maji na maendeleo endelevu.
=30=