Thursday, November 23, 2017

WAKULIMA IRINGA WATAKIWA KUTUMIA VIZURI MVUA ZA MWANZO KUPANDIA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-IRINGA
Wakulima mkoani Iringa washauriwa kuzitumia vizuri mvua zilizoanza kunyesha kupanda kwa kutumia mbegu bora na kuzingatia mistari.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, mheshimiwa Amina Masenza alipokuwa akiongea katika kipindi cha moja kwa moja cha Sunrise power kinachorushwa na kituo cha redio Nuru cha mjini Iringa jana.

Mheshimiwa Masenza alisema kuwa mvua zilizoanza kunyesha zitumike vizuri kwa kupandia. Aliwataka wakulima kuchagua mbegu bora zilizoidhinishwa na wataalam ili waweze kupata mazao bora. Aidha, alishauri kufuata ushauri wa wataalam wa akilimo ili kupata tija kupitia kilimo.

Mkoa wa Iringa ni miongoni mwa mikoa iliyo mstari wa mbele katika kilimo cha mazao ya chakula katika mikoa ya nyanda za juu kusini mwa Tanzania.
=30=

VYAMA VYA SIASA VYAASWA KUFANYA KAMPENI KISTAARABU



Na. Dennis Gondwe, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-IRINGA
Vyama vya siasa mkoani Iringa vimetakiwa kufanya kampeni za kistaarabu na kuachana na vitendo vya vurugu kwa sababu serikalai ipo macho muda wote.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, mheshimiwa Amina Masenza alipokuwa akiongea katika kipindi cha Sunrise power kinachorushwa na kituo cha redio Nuru cha mjini Iringa jana.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza (picha na maktaba)
Mheshimiwa Masenza ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Iringa alivitaka vyama vya siasa kuendesha kampeni za kistaarabu katika maeneo utakapofanyika uchaguzi mdogo wa madiwani. 

Napenda mkubuke kuwa baada ya uchaguzi maisha yanaendelea kama kawaida. Kila chama lazima kipige kampeni kwa uhuru na ustaarabu bila kusababisha viashiria vya vurugu” alisema mheshimiwa Masenza. 

Aliongeza kuwa mtu yeyote atakayefanya vurugu afahamu kuwa serikali ipo macho itamshughulikia kwa mujibu wa sheria za nchi.

Uchaguzi mdogo wa madiwani unatarajiwa kufanyika tarehe 26/11/2017 katika Kata za Kitwiru na Kimala katika halmashauri za Manispaa na Kilolo mtawalia katika mkoa wa Iringa.
=30=

JAMII YATAKIWA KUUNGA MKONO KIKUKI KUPAMBANA NA KIFUA KIKUU IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-IRINGA
Jamii imetakiwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na kikundi cha kudhibiti kifua kikuu mkoa wa Iringa (KIKUKI) ili kiweze kuwaibua wahisiwa wa ugonjwa wa kifua kikuu mkoani hapa.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu wa KIKUKI, Lucas Mallya alipokuwa akiongelea changamoto zinazokikabili kikundi chao kutekeleza majukumu yake katika kampeni tambuzi za kifua kikuu na magonjwa yasiyoambukiza katika bustani ya Manispaa ya Iringa hivi karibuni.
 
KIKUKI
Mallya alisema “changamoto kubwa katika kikundi chetu ni watu na wadau wa kutuunga mkono katika kazi tunazofanya za kuibua wahisiwa wa ugonjwa wa kifua kikuu, kuwapeleka kufanyiwa uchunguzi na kuanzishiwa dawa”. 

Alisema kuwa kikundi kinahitaji posho na nauli kwa ili wanakikundi waweze kutembelea maeneo tofauti katika kata 18 za Manispaa ya Iringa. Alisema kuwa Kata 18 ni nyingi na kubwa hivyo kuzifikia zote ni kazi inayohitaji moyo wa kujitoa na malipo kidogo.

Changamoto nyingine aliitaja kuwa ni imani potofu waliyonayo wananchi kuwa ugonjwa wa kifua kikuu unatokana na kurogwa, hivyo matibabu yake kufanyika kwa waganga wa kienyeji. 

Ugonjwa wa kifua kikuu unatibika hospitali tena bure. Katika kuthibitisha hili, kikundi chetu kipo hapa kutoa ushuhuda kwa sababu wanakikundi ni watu waliougua ugonjwa wa kifua kikuu na kupona” alisema Mallya.

Nae mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Iringa, Dr. Tecla Orio alisema kuwa kikundi cha KIKUKI kimekuwa kikifanya kazi nzuri kwa kujitolea katika Manispaa ya Iringa. Alitoa wito kwa wadau wa mapambano dhidi ya Kifua Kikuu kujitokeza na kuunga mkono juhudi hizo ili kikundi kiweze kuwafikia na kuwaibua wagonjwa wengi zaidi na kuanzishiwa tiba.

Kikundi cha kudhibiti kifua kikuu mkoa wa Iringa, kilianza mwaka 2011 kikiwa na wanakikundi 23. Kikundi kinatumia njia za ngoma, maigizo na kutoa ushuhuda katika kufikia ujumbe kwa wahusika.
=30= 

IRINGA WATAKIWA KUACHA UNYANYAPAA WAGONJWA WA TB



Na. Dennis Gondwe, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-IRINGA
Jamii imetakiwa kuacha unyanyapaa kwa wagonjwa wa kifua kikuu kwa sababu nao ni sehemu ya jamii badala yake kuwapa ushirikianao wa hali ya juu.

Kauli hiyo ilitolewa na mratibu wa kifua kikuu na ukoma mkoa wa Iringa, Dr. Tecla Orio alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na madhara ya unyanyapaa kwa wagonjwa wa kifua kikuu katika bustani ya Manispaa ya Iringa hivi karibuni.
 
Dr Tecla Orio

KIKUKI

Dr. Orio alisema kuwa wagonjwa wa kifua kikuu wamekuwa wakipata unyanyapaa toka kwa jamii na kuwaathiri kisaikolojia.  Aliongeza jamii imekuwa ikiwaangalia na kuwasemea maneno mabaya wagonjwa wa kifua kikuu na familia zao. 

Wagonjwa hawa na familia zao wamekuwa wakitengwa katika shughuli za kijamii na kuwafanya waendelee kujiona wanyonge katika jamii” alisema Dr. Orio. Kutokana na hali hiyo ya unyanyapaa, wagonjwa wa kifua kikuu wanakuwa katika hali ya huzuni, upweke, wasiwasi na kutokujiamini na kukata tamaa. 

Hali ya unyanyapaa imewafanya wagonjwa kuchelewa kupata vipimo na matibabu na kuendelea kueneza ugonjwa huo kwa watu wengine. Lakini unyanyapaa huo umekuwa pia na athari kwa kuwafanya wagonjwa kujificha kuzuia wasitoe taarifa kuhusu hali zao” alisisitiza Dr. Orio.

Akiongelea sababu za unyanyapaa, mratibu wa kifua kikuu na ukoma mkoa wa Iringa, alizitaja kuwa ni ukosefu wa elimu kuhusu ugonjwa wa kifua kikuu hasa njia zinazosababisha maambukizi. 

Uhusiano wa ugonjwa wa kifua kikuu na virusi vya ukimwi, ugunduzi na matibabu yake. Wagonjwa wa kifua kikuu kuonekana hawakuwa makini katika kujikinga” alisema Dr Orio. Sababu nyingine aliitaja kuwa ni ukosefu wa vifaa vya kujikinga kwa wahudumu wa afya walio katika hatari ya kuambukizwa.

Mratibu huyo aliitaka jamii kuwapa ushirikiano wagonjwa wa kifua kikuu na kuwatia moyo ili wakamilishe matibabu yao na kuendelea na utekelezaji wa majukumu yao. Aidha, aliikumbusha jamii kuwa mgonjwa wa kifua kikuu akishaanza matibabu hawezi kuambukiza watu wengine.

Katibu wa kikundi cha kudhibiti kifua kikuu mkoa wa Iringa (KIKUKI), Lucas Mallya alisema kuwa ugonjwa wa kifua kikuu ni kama ugonjwa mwingine unaotibiwa katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Mgonjwa wa kifua kikuu anapoanza dawa hupona kabisa na hupewa elimu ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo. Bahati nzuri matibabu ya kifua kikuu ni bure kabisa” alisema Mallya.

Matibabu ya ugonjwa wa kifua kikuu huchukua miezi sita hadi nane na hutolewa bure katika vituo vya kutolea huduma vya serikali na binafsi.
=30=