Tuesday, October 4, 2011

RC RUVUMA AONGEA NA WAANDISHI WA HABARI

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mhe Said Thabit Mwambungu amesema kuwa Serikali inathamini mchango mkubwa unaotolewa na waandishi wa habari katika ujumbe wa serikali kwa wananchi ili kusukuma gurudumu la maendeleo. 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Said Mwambungu akiongea na waandishi wa habari Ofisi kwake

Mhe. Mwambungu amesema hayo alipokuwa akiongea na waandishi wa habari wa Manispaa ya Songea Ofisini kwake hivi karibuni 
Aidha, Mkuu wa Mkoa huyo amewataka waandishi hao wa habari kuendelea kuhabarisha Umma wakizingatia maadili ya habari kwani kwa kukiuka maadili wanaweza kuipotosha jamii na kusababisha hatari katika jamii.
Kwa upande wake Katibu wa Ruvuma Press Club Bw. Andrew Chatwanga  amempongeza  Mkuu wa Mkoa kwa uamuzi wake wa kuongea na wanahabari hao ikiwa ni siku chache tu baada ya kuripoti mkoani kuanza kazi ya kuongoza shughuli za Serikali mkoani hapo.
Bw. Chatwanga alitumia fursa hiyo kumwomba Mkuu wa Mkoa kuchukua hatua za kipekee ili kuifanya Manispaa ya Songea inaboreka kwa usafi wa mazingira kama alivyofanya kwa Manispaa ya Morogoro. Kwa sasa Manispaa ya Songea usafi wa mazingira hauridhishi.

Habari hii ni kwa hisani ya Revocatus A. Kasimba, Afisa Habari, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa

LUDEWA NI PEMBEZONI NA WAPI?? AHOJI RC

Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma ametofautiana na uongozi wa Wilaya ya Ludewa katika dhana inayoendelea kuwa Wilaya ya Ludewa ipo pembezoni.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa amehoji alipokuwa akizungunza na watumishi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa alipofanya ziara ya kujitambusha na kuzifahamu changamoto zinazoikabili Wilaya ya Ludewa.
Dkt. Ishengoma amesema “kuanzia sasa Ludewa hatupo pembezoni”. Aidha, amehoji kuwa Ludewa ipo pombezoni na wapi? Ameendelea kuhoji kuwa “kama Ludewa ipo pembezoni je, mwanzoni ni wapi”.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.) akiongea na watumishi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa
Amesema kuwa maendeleo ndiyo dira inayoipeleka Wilaya pembezoni au mwanzoni. Amesema kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Wilaya na hali halisi aliyokutana nayo njiani inaonesha kuwa Wilaya hiyo inayo maendeleo yanayoonekana na kupimika.
Amewataka viongozi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuachana na dhana hiyo kwani inawafanya kujiona kuwa ni wanyonge na hivyo kujiweka pembeni na dhana ya maendeleo na uwajibikaji kikamilifu.
Aidha, amewataka wanaludewa kuchangamkia fursa iliyopo ya ujenzi wa viwanda na machimbo Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma ili kujumuika katika mchakato wa kujiletea maendeleo.
Akiongelea kero inayowakabili wananchi wa Wilaya hiyo ambayo ni barabara, amesema kuwa barabara za Wilaya hiyo zitajengwa kwa sababu zimeainishwa katika ilani ya uchaguzi ya chama tawala.
Dkt. Ishengoma ametoa ombi kwa watumishi wote wa Umma kuendelea kuipenda serikali yao kwa sababu inawajali na kutekeleza mahitaji yao ikiwa ni pamoja na kuwaletea maendeleo. Vilevile, amewataka kuwajibika kwa serikali yao kwa kuchapa kazi kwa bidii.
Akiongelea miradi ya maendeleo, amewataka watumishi na viongozi wanaosimamia miradi ya maendeleo kwa kutekeleza wajibu huo kulingana na thamani halisi ya fedha za Umma zinazotolewa.
Awali akiwasilisha taarifa ya Wilaya ya Ludewa, Mkuu wa Wilaya hiyo Bibi. Georgina Bundala amesema kuwa Wilaya yake inajishughulisha na shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kilimo (90%), biashara (3%), uvuvi, sekta binafsi (4%) na ajira rasmi (3%).  Amesema kuwa Wilaya yake ina fursa nyingi zinazohitaji kuendelezwa ili ziweze kuchangia katika pato la Wilaya na uchumi wa mwananchi. Amezitaja fursa hizo kuwa ni utajiri mkubwa wa madini ya chuma, makaa ya mawe, dharabu, chokaa na vito mbalimbali vya thamani.
Bibi. Bundala amesema kuwa kwa takwimu za mwaka 2008 wastani wa pato la mwananchi Wilayani Ludewa lilikuwa ni shilingi 125,000 kwa mwaka. Amesisitiza kuwa pato hilo ni dogo sana kukidhi mahitaji muhumu ya kibinadamu. Amesema kuwa mkakati wa Wilaya yake ni kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara ili kuongeza pato la mwananchi kuendana na viwango vya kimataifa.
Amesema kuwa Wilaya yake inaendelea kuhamasisha jamii kuweza kukuza kilimo cha kahawa, pareto, chai, korosho, alizeti, ufuta, karanga na kupanua kilimo cha umwagiliaji.
=30=

'LUDEWA ONGEZENI KASI KATIKA MAENDELEO ASEMA RC'

Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameitaka Wilaya ya Ludewa kuongeza kasi katika kujiletea maendeleo kutokana na kuwa na rasilimali nyingi na ardhi nzuri inayofaa kwa shughuli za kilimo.
Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika sekondari ya Mavanga katika siku yake ya kwanza ya ziara ya kuzitembelea Wilaya za Mkoa wa Iringa akianza na Wilaya ya Ludewa.
Dkt. Ishengoma amesema “Ludewa ni Wilaya nzuri kwa kilimo na imejaaliwa kuwa na rasilimali nyingi pamoja na madini mengi”. Amesema kuwa Wilaya hiyo inabahati ya kuwa na madini ya makaa ya mawe na  chuma pamoja na madini mengine.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.)(kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Ludewa BIBI. Georgina Bundala (kulia) wakibadilishana mawazo walipotembelea eneo la Chuma cha Liganga wilayani Ludewa.
Vilevile, amewataka wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuchangamkia fursa zitokanazo na madini hayo hasa pale yatakapoanza kuchimbwa rasmi. Amesema kuwa viwanda vikianza kujengwa lazima viwanufaishe wananchi wa Ludewa kwa wao kuchangamkia fursa za ajira pasipo kubweteka ili maisha bora yawezekane kwao. Amesisitiza kuwa maisha bora hayatawezekana kwa wananchi kubweteka ila pale tu watakapojishughulisha kwa kufanya kazi kwa bidii.
Akiongelea elimu Dkt. Ishengoma amewataka wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kwa sababu sekta hiyo inamuwezesha mwananchi kukabiliana na changamoto za kimaisha.
Amesema kuwa wananchi wanawajibika katika kuendeleza sekta ya elimu kwa kusaidiana na serikali yao ili kuinua kiwango cha elimu Wilayani hapo. Amesema “katika kumuwezesha mwananchi kukabiliana na changamoto za leo za kimaisha ni lazima kuwekeza katika sekta ya elimu kwa kuwa elimu inampelekea mwananchi katika kupata ufumbuzi wa changamoto za kimaisha”.
Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Bibi. Georgina Bundala amesema kuwa wananchi wa Wilaya ya Ludewa ni wasikivu na wachapa kazi sana hasa wanapopatiwa maelezo sahihi kutoka kwa viongozi wao wanaowasimamia na wataalamu. Amesema kuwa Wilaya yake imejikita katika shughuli kadhaa za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na kilimo, uvuvi, ufugaji na ujasiliamali.
=30=

RC ASISITIZA MASOMO YA SAYANSI LUDEWA

Mkuu wa Mkoa wa Iringa awataka wanafunzi wa shule ya sekondari ya Lugarawa kitilia mkazo masomo ya sayansi ili waweze kulitumikia taifa katika fani hizo.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akifungua daharia ya wasichana katika shule ya sekondari ya Lugarawa iliyopo katika kata ya Lugarawa Wilayani Ludewa.

Dkt. Ishengoma amesema kuwa wanafunzi wengi hasa wa kike wamekuwa wakiyakimbia masomo ya sayansi kwa kisingizio cha ugumu wa masomo hayo jambo alilolikanusha. Amesema “masomo ya sayansi si magumu kama yanavyodaiwa na wengi, masomo yote yanahitaji juhudi na kujituma ili kuweza kufaulu”.  Amesisitiza kuwa elimu ni msingi wa maisha na maendeleo katika kila jamii inayohitaji kustaarabika.
Amesema “wazazi wamekuwa wakijitahidi kujenga miundombinu ya kielimu kama shule, maabara na daharia kutokana na mapenzi yao kwenu (wanafunzi)”. Amesisitiza kuwa kwa msingi huo wanafunzi nao wanajukumu la kurudisha shukrani zao kwa wazazi kwa kufauli vizuri mitihani yao na hatimae kuwa raia wema watakaolijenga taifa lao.
Aidha, amewataka wazazi na jamii ya Ludewa kugeukia pia uwekezaji katika ujenzi wa daharia za wavulana kwa sababu nazo ni muhimu sana katika kudhibiti makuzi ya wanafunzi hao wavulana.
Kwa mujibu wa taarifa ya wananchi wa Kata ya Lugarawa iliyowasilishwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ujenzi wa daharia hiyo ulianza mwaka 2008 hadi mwaka 2010 lengo likiwa ni kuwawezesha wanafunzi wa kike 48 katika shule hiyo kukaa shuleni na kufuatilia masomo yao na kuepukana na hadha za kukaa nje ya shule ikiwa ni pamoja na kupata mimba.
Daharia hiyo iligharimu shilingi milioni 30,785,500 na wananchi wamechangia kiasi cha shilingi milioni 28,085,500 zikiwa ni gharama za kufyatua tofari na fedha taslimu. Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa ilichangia shilingi milioni 2,700,000 kwa upigaji bati na saruji.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, yupo katika ziara ya kujitambulisha na kuzifahamu changamoto zinazozikabili Wilaya za Mkoa wa Iringa na kukagua na kuhimiza shughuli za maendeleo.
=30=

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.)(katikati) na Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Bibi. Georgina Bundala (kushoto) wakibadilishana mawazo alipowasili Wilayani Ludewa.