Tuesday, October 4, 2011

'LUDEWA ONGEZENI KASI KATIKA MAENDELEO ASEMA RC'

Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameitaka Wilaya ya Ludewa kuongeza kasi katika kujiletea maendeleo kutokana na kuwa na rasilimali nyingi na ardhi nzuri inayofaa kwa shughuli za kilimo.
Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika sekondari ya Mavanga katika siku yake ya kwanza ya ziara ya kuzitembelea Wilaya za Mkoa wa Iringa akianza na Wilaya ya Ludewa.
Dkt. Ishengoma amesema “Ludewa ni Wilaya nzuri kwa kilimo na imejaaliwa kuwa na rasilimali nyingi pamoja na madini mengi”. Amesema kuwa Wilaya hiyo inabahati ya kuwa na madini ya makaa ya mawe na  chuma pamoja na madini mengine.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.)(kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Ludewa BIBI. Georgina Bundala (kulia) wakibadilishana mawazo walipotembelea eneo la Chuma cha Liganga wilayani Ludewa.
Vilevile, amewataka wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuchangamkia fursa zitokanazo na madini hayo hasa pale yatakapoanza kuchimbwa rasmi. Amesema kuwa viwanda vikianza kujengwa lazima viwanufaishe wananchi wa Ludewa kwa wao kuchangamkia fursa za ajira pasipo kubweteka ili maisha bora yawezekane kwao. Amesisitiza kuwa maisha bora hayatawezekana kwa wananchi kubweteka ila pale tu watakapojishughulisha kwa kufanya kazi kwa bidii.
Akiongelea elimu Dkt. Ishengoma amewataka wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu kwa sababu sekta hiyo inamuwezesha mwananchi kukabiliana na changamoto za kimaisha.
Amesema kuwa wananchi wanawajibika katika kuendeleza sekta ya elimu kwa kusaidiana na serikali yao ili kuinua kiwango cha elimu Wilayani hapo. Amesema “katika kumuwezesha mwananchi kukabiliana na changamoto za leo za kimaisha ni lazima kuwekeza katika sekta ya elimu kwa kuwa elimu inampelekea mwananchi katika kupata ufumbuzi wa changamoto za kimaisha”.
Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Ludewa, Bibi. Georgina Bundala amesema kuwa wananchi wa Wilaya ya Ludewa ni wasikivu na wachapa kazi sana hasa wanapopatiwa maelezo sahihi kutoka kwa viongozi wao wanaowasimamia na wataalamu. Amesema kuwa Wilaya yake imejikita katika shughuli kadhaa za kimaendeleo ikiwa ni pamoja na kilimo, uvuvi, ufugaji na ujasiliamali.
=30=

No comments:

Post a Comment