Wednesday, October 16, 2013

RAIS KIKWETE ATOA ZAWADI YA IDD MKOANI TANGA

 Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Gallawa akimkabidhi zawadi za IDD kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania msimamizi wa Mahabusu ya watoto, Bi. Ng’wanza John.





Wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 60 wanaolelewa katika kituo cha serikali cha kulea wazee kilichopo Mwanzange jijini Tanga wakifurahia zawadi za IDD zilizotolewa na Rais Dkt. Kikwete. 




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Kikwete ametoa zawadi za Idd kwa vituo 12 vya watoto yatima na makundi maalumu nchini kwa ajili ya kusherehekea sikukuu ya Idd El Haji. 

Zawadi hizo zilikabidhiwa kwa vituo vya Msongola (Ilala), Dar Al Argram (Temeke), Furaha (Kinondoni), Makao ya wazee (Temeke), Makao ya Watoto ya Mother Thereasa (Kinondoni).

Vituo vingine ni Malaika kids Home (Mkuranga), Makazi ya wazee Kilima (Bukoba), Mahabusu ya watoto (Arusha), Mahabusu ya watoto (Tanga), Makazi yawazee Mwanzage (Tanga), Makao ya watoto Istikama (Pemba), Makazi ya wazee sebuleni (Unguja).

Zawadi zilizokabidhiwa ni pamoja na mchele, mbuzi na mafuta ya kula vyote vikiwa na thamani ya Tshs. 5,505,000.

=30=








MKE WA RAIS AZINDUA JENGO LA WATOTO KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA




Serikali inatambua na kuthamini mchango unaotolewa na wananchi wa Italia katika kuboresha huduma za matibabu kwa watoto kwa lengo la kupunguza vifo vya watoto.

Kauli hiyo imetolewa na Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete katika hotuba yake kwenye uzinduzi wa jengo la huduma za watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa.


            Mama Salma Kikwete akizindua jengo la Watoto 
 
Mama Salma amesema “tupo hapa kuzindua jengo la kutolea huduma za watoto. Lakini kabla ya kuzindua jengo hili, naomba niwashukuru sana serikali ya Italia kwa msaada waliotoa kulijenga jengo wa Tshs. 1,842,000,000”. Amesema kuwa serikali ya Tanzania inatambua na kuthamini mchango mkubwa waliotoa wananchi wa Italia kwa wananchi wa Tanzania. “Kwa mchango huu, wananchi wa Italia wametambua umuhimu wa kuboresha huduma za matibabu kwa watoto, ambazo zitasaidia kupunguza vifo vya watoto” alisisitiza Mama Salma. Ameongeza kuwa jengo hilo litapunguza msongamano wa watoto wagonjwa wodini na kuboresha huduma za afya ya watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa.

Akiongelea uhusiano kati ya hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa na hospitali ya Vicenza ya mkoa wa Veneto nchini Italia Mama Salma amesema kuwa uhusiano huo unapaswa kuimarishwa na kuheshimiwa kwa sababu unaboresha utoaji wa huduma za afya katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa.

Kutokana na hospitali nyingi kulalamikiwa kuhusu utoaji huduma usiridhisha, Mama Salma ameitaka hospitali ya rufaa ya mkoa kuwa mfano katika utoaji huduma bora kwa wananchi. Amewataka madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo kutoa huduma kwa kujituma, uadilifu, uzalendo na kutumia lugha rafiki inayoweza kumfariji mgonjwa.

Akiwasilisha taarifa ya mradi wa kuboresha huduma za mama na mtoto inayohusisha ujenzi wa jengo la kujifungulia mama wajawazito na ujenzi wa wodi ya watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa, mganga mkuu wa mkoa wa Iringa, Dk. Robert Salim amesema kuwa lengo la mradi ni kuboresha huduma za kujifungua, kupunguza vifo vya wajawazito na vifo vya watoto wachanga vinavyotokana na baridi, kukosa hewa na kupunguza msongamano. Amesema mradi huo pia utapunguza maambukizi ya magonjwa kwa mama waliojifungua na kuboresha utoaji wa huduma kwa urahisi kwa mama wajawazito wanaojifungua wanaojifungua kwa kuwa na eneo kubwa la kufanyia kazi.

Dk. Salim amesema kuwa kutokana na kuongezeka kwa magonjwa ya kuambukiza na vifo vya watoto chini ya miaka mitano, msongamato katika wodi ya watoto, kukosekana kwa chumba cha kuhudumia watoto walio mahututi, chumba cha kuhudumia watoto njiti na wenye utapia mlo mkali, ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na hospitali rafiki ya Vicenza ya Italia iliona ni vema kuwa na wodi maalumu kwa ajili ya kuwahudumia watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa.
=30=




RAIS KIKWETE WAUTAJA 2014 MWAKA MAALUMU



RAIS Jakaya Kikwete amesema Mwaka 2014 ni mwaka maalumu na wa aina yake katika historia ya Tanzania kwa kuwa utakuwa na mambo makubwa matatu yatakayofanywa.

Jambo kubwa alililosisitiza ni mchakato wa Katiba Mpya ambao alisema ni lazima ukamileke mwakani kama mambo yatakwenda sawa sawa.


             Rais Dk. Jakaya Kikwete akihutubia umma wa wananchi
 
Akiyataja mambo mengine alisema “Tutasheherekea miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar yaliyoondoa udhalimu na kuwarudishia wazanzibari heshima ya mwanadamu na utu wake, na tutasherehekea miaka 50 ya Muungano wetu,” alisema.

Aliwaomba watanzania wajiandae kuyafanikisha vizuri mambo hayo ili historia mpya ifunguliwe nchini.

“Wazanzibar waanze miaka mingine baada ya miaka hamsini ya uhuru wao, muungano uanze miaka mingine baada ya miaka hamsini na katiba mpya itupeleke miaka mingine tukiwa wamoja,” alisema.

Aliyasema hayo jana wakati akiadhimisha kilele cha mbio za Mwenge Uhuru zilizofanyika katika uwanja wa Samora mjini Iringa.
Maadhimisho hayo yalitaka kuingia dosari baada ya mtu mmoja (mwanaume) ambaye hata hivyo jina lake halikuweza kupatikana mara moja kujichomeka katika kundi la wanahabari akiwa na nia ovu.

Wakati Rais Kikwete akiwa ameshuka chini katika jukwaa dogo akisubiri kukabidhiwa Mwenge huo, mtu huyo alichomoka kutoka katika kundi hilo na kujaribu kumvaa kiongozi wa mbio za mwenge, Juma Ali Sima aliyekuwa kaubeba Mwenge huo.

Lengo lake likiwa halieleweki, mtu huyo alitaka kuunyang’anya Mwenge huo kutoka kwa kiongozi wa mbio hizo kabla hajadhibitiwa vikali na askari Polisi na baadhi ya walinzi wa Rais waliokuwa jirani.

Wakati tukio hilo likitokea Rais Kikwete pamoja na wasaidizi wake wengine walikuwa mita kama kumi kutoka katika eneo la tukio akisubiri kukabidhiwa Mwenge huo.
Sherehe hizo zilizofana zilihudhuriwa na maelfu ya wakazi wa mjini Iringa na vitongoji vyake, na zilisindikizwa na burudani za vikundi mbalimbali vya ngoma za asili, kwaya na Bongo fleva.
 
        Maelfu ya wananchi wakisikiliza hotuba ya Rais Kikwete
 
Wengine waliohudhuria sherehe hizo ni viongozi mbalimbali wa serikali kutoka wizarani, mikoani na wilayani mbalimbali za Tanzania Bara na Visiwani.

Akifafanua umuhimu wa Mbio za Mwenge wa Uhuru, Rais Kikwete alivipongeza vyombo vya kufikisha ujumbe wa mwenge kwa wananchi kwa uhodari mkubwa.

“Bila vyombo vya habari wapotoshaji hawakosekani, na wasiopenda mwenge pia wapo, hawawezi kukosekana

Alisema kilele cha maadhimisho ya mbio za Mwenge imefanywa kuwa pia siku ya kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere tangu afariki miaka 14 iliyopita.

Alisema watanzania wote bila kujali itikadi zao wanawajibu wa kuyakumbuka mema yoote yaliyofanywa na baba wa Taifa, mafundisho yake na urithi kwa Taifa hili.
                                  Vijana wa Halaiki

“Nia ya maadhimisho haya, watu wasimsahau kiongozi huyu maalumu katika hostoria ya nchi; tunahitaji kumkumbuka hasa wakati huu wa mchakato wa Katiba,” alisema.

Alisema “tunahitaji kujikumbusha mawazo ya mwalimu kuhusu umoja wa nchi yetu, umoja wa watu wake na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.”

Alisema “hotuba zake na maandishi yake kuhusu mambo hayo yana mafundisho mazuri na yenye manufaa, tukiyaelewa na kuyazingatia yatatusaidia katika mjadala unaoendelea na tutakamilisha mchakato huu salama na tutakuwa na katiba nzuri.

Alisema fikra za Mwalimu na mtazamo wake kuhusu umoja wa watanzania na muungano tulioanao bado vina maana mpaka leo hii ikiwa ni miaka 14 baada ya kifo chake.

Ili kumkumbuka zaidi Mwalimu Nyerere alipendekeza siku yake ya kuzaliwa ndiyo iitwe Nyerere Day na ianze kusheherekewa kwa mbwembwe, iwe na mijadala ya kazi zake na itumiwe kufanya shughuli mbalimbali kuenzi kazi zake.

Alisema pamoja na mtazamo wake huo hana maana kwamba hataki mabadiliko, lakini akayasema mabadiliko anayoyata kuwa ni yale yatakayoipeleka nchi mbele sio kuirudisha nyuma.

Aliwapongeza watanzania wanaokataa ushawishi wa kugawanya kwa misingi ya dini, siasa na mambo mengine.

Alisema dhambi kubwa ya kubaguana kwa misingi yoyote ile ni kupotea kwa amani na kwamba amani ikipotea watu watatumia muda mwingi kujihami badala ya kufanya shughuli zao za maendeleo.

Alisema kama watanzania watakubali nchi ifike hapo, itayumba na hakuna atakayebaki salama hivyo ni muhimu kuziba nyufa zinazoweza kuleta hali hiyo.

Alisema serikali yake itaendelea kukemea vitendo vyote vya kuvuruga amani na watakaohusika watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Katika maadhimisho hayo Rais Kikwete alizungumzia mkakati wa serikali yake wa kupambana na madawa ya kulevya, mapambano ya Ukimwi, rushwa na maendeleo katika sekta mbalimbali kupitia mpango wa Matokeo Makubwa Sasa.

=30=
Habari hii ni kwa Hisani ya Mtandao wa Bongo Leaks