Sunday, December 9, 2012

MATUKIO YA MAADHIMISHO YA MIAKA 51 YA UHURU KATIKA PICHA

 Baadhi ya viongozi walioshiriki maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara kimkoa

 Baadhi ya viongozi na maafisa waandamizi walioshiriki maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara kimkoa katika tarafa ya Mahenge Wilayani Kilolo

  Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Dickolagwa (wapili kushoto) akisaini kitabu cha wageni


 Viongozi wakitafakari kwa kina juu ya miaka 51 ya Uhuru wa tanzania Bara

Ritta Kabati, Mbunge (CCM) Viti Maalum akisaini kitabu cha wageni (kulia) Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Dickolagwa

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (katikati) akisaini kitabu cha wageni kushoto ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Joseph Muhumba na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Helman Msua (kulia)


Baadji ya wananchi waliojumuika katika maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara

UHURU UENDE SAMBAMBA NA UWAJIBIKAJI NA UZALENDO




Wananchi na viongozi Mkoani Iringa wametakiwa kuongeza uwajibikaji na uadilifu kwa kutanguliza mbele uzalendo na maslahi ya Taifa katika shughuli zao za kila siku za kujiletea maendeleo yao na maendeleo ya Taifa.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akiwahutubia wananchi wa Mkoa wa Iringa wakati wa maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Tanzania Bara yaliyofanyika kimkoa katika Tarafa ya Mahenge Wilayani Kilolo.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (katikati) akisaini kitabu cha wageni, kushoto ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Josheph Muhumba na Helman Msua, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Wilaya ya Kilolo (kulia)

Dkt. Christine amesema “ni ukweli usiopingika tukiwajibika ipasavyo, tukiwa waadilifu, na wazalendo kuanzia kwenye kaya hadi Taifa tutalitumikia Taifa na kupata maendeleo yanayohitajika. Hivi vitu vitatu ni msingi mkubwa sana wa maendeleo ya nchi yetu, hivyo kila mmoja inampasa kutimiza kauli mbiu hii”.

Akiongelea mafanikio yaliyopatikana mkoani Iringa tokea Uhuru, Mkuu wa Mkoa ameyataja kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa pato la Mkoa na pato la mkazi. Amesema mwaka 1961 pato la Mkoa lilikuwa ni shilingi 5,693,000 na wastani wa pato la mtu kwa mwaka lilikuwa shilingi 103. Amesema kwa mwaka 2011 pato la Mkoa limekuwa na kufikia shilingi 1,985,708,000 wakati pato la mkazi limeongezeka na kufikia shilingi 1,225,503.
Katika ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri, Mkoa wa Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa kumekuwapo na ongezeko kubwa la ukusanyaji wa mapato hayo kwa mwaka 2011/2012 mapato ya Halmashauri yaliyokusanywa ni shilingi 9,357,013,391 kutoka vyanzo vya ndani, kukiwa na ongezeko la shilingi 9,355,366,502 yakilinganishwa na mapato ya mwaka 1961/1962 ya shilingi 1,646,889.
Kwa upande wa kilimo ambacho ni shughuli kuu ya kiuchumi, Dkt. Christine amesema kuwa Mkoa wa Iringa umefanikiwa kuongeza eneo linalolimwa kutoka Hekta 305,208.65 mwaka 1961/1962 hadi kufikia Hekta 411,116 mwaka 2011/2012. Amesema kuwa sambamba na kuongeza eneo hilo, pia elimu juu ya kilimo bora imeendelea kutolewa kwa wakulima na jumla ya mashamba darasa 1,603 yameanzishwa wakati wakulima 49,075 wamepatiwa mafunzo kwa vitendo kupitia mashamba hayo kwa kipindi cha kuanzia mwaka 1961 hadi mwaka 2011. Amesema katika kuhakikisha kuwa elimu inawafikia wakulima wengi, Mkoa umeanzisha vituo vya rasilimali watu wa kilimo katika kata 17.

Amesema kuwa Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya mbolea katika kilimo ili kuwawezesha wakulima kupata mazao mengi na bora. Amesema Mkoa wa Iringa umeweza kuongeza matumizi ya mbolea toka tani 16,826 na tani 300 za mbegu hadi kufikisha tani 42,250 za mbolea na tani 3,142 za mbegu kwa mwaka 2011.

Katika salamu zake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, Joseph Muhumba, amesema kuwa matunda ya Uhuru wa Tanzania Bara ni mengi na katika wilaya ya Kilolo wanayachukulia kuwa ni heshima kubwa na kuipa uzito mkubwa. Amesema kuwa ili heshima hiyo iendelee kuenziwa, ni lazima wananchi kufanya kazi kwa bidii, kutunza amani na utulivu vilivyopo katika Wilaya, Mkoa na Taifa kwa ujumla. Muhumba ambaye pia ni diwani wa Kata ya Image amesema kuwa Uhuru utaendelea  kumhamasisha kila mwananchi kuongeza juhudi katika kufanya kazi halali za kujiletea maendeleo yake binafsi ya maendeleo ya ujumla.  

Akiwasilisha Taarifa fupi ya maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru na maendeleo yaliyopatikana katika wilaya ya Kilolo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Helman Msua, amesema kuwa pamoja na Wilaya hiyo kuanzishwa mwaka 2002 bado imepiga hatua sana katika nyanza mbalimbali. Akitolea mfano juhudi za kukuza kilimo kupitia matumizi ya zana bora za kilimo, amesema mwaka 2002 Wilaya yake ilikuwa na matrekta makubwa 41 na hadi kufikia mwaka 2002 matrekta hayo yameongezeka hadi kufikia 52. Amesema kuwa vyama vya ushirika vimeongezeka toka 15 mwaka 2002 hadi kufikia 54 mwaka 2012.

Miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara inaadhimishwa nchini kote ikiongozwa na kauli mbiu isemayo “uwajibikaji, uadilifu na uzalendo ni nguzo ya maendeleo ya Taifa letu”.
=30=


HOTUBA YA MKUU WA MKOA WA IRINGA MHESHIMIWA DR. CHRISTINE G. ISHENGOMA (MB) WAKATI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA UHURU WA TANZANIA BARA 09/12/2012 KIMKOA KATIKA TARAFA YA MAHENGE WILAYA YA KILOLO

Ndugu Kaimu Katibu Tawala Mkoa,
Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya,
Mheshimiwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo,
Mheshimiwa Mbunge,
Mhe. Mwenyekiti wa CCM (W),
Ndugu Katibu wa CCM (W),
Makatibu Tawala Wasaidizi Sekretarieti ya Mkoa,
Waheshimiwa Madiwani,
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Kilolo,
Viongozi wa Madhehebu ya Dini,
Viongozi wa Vyama vya Siasa,
Waandishi wa Habari,
Mabibi na Mabwana.
Ndugu Wananchi,

Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa wananchi wa Tarafa ya Mahenge kukusanyika katika Viwanja hivi tukiwa na lengo la kuadhimisha na kuyakumbuka yale yote yaliyofanyika toka tumepata uhuru 9/12/1961.


Aidha, natumia fursa hii kuwashukuru Viongozi na Wananchi wa Wilaya ya Kilolo kwa maandalizi mazuri na kwa kukubali kwao kuadhimisha siku hii muhimu kwa Watanzania wote.

Vilevile, nawashukuru Vikundi vya burudani kwa kutumbuiza vizuri, na kwa ujumbe ambao mumetuachia na kutuasa. Nasema asanteni sana.


Ndugu Wananchi,
Mkoa wa Iringa ulianzishwa Mwaka 1964 kutoka Mkoa wa zamani ambao uliitwa Jimbo la Kusini la Nyanda za Juu. Makao Makuu yakiwa Mbeya. Mkoa ulikuwa na Wilaya mbili ambazo ni Njombe na Iringa. Wilaya ya Mufindi ilianzishwa Mwaka 1964, Wilaya ya Ludewa Mwaka 1975, Makete Mwaka 1979 na Kilolo  Mwaka 2002.
Na Mwaka huu 2012 Mwezi Julai Mkoa wa Iringa uligawanywa rasmi na kuunda Mkoa mpya wa Njombe. Haya ni mafanikio makubwa sana.

Mkoa wetu wa Iringa kiutawala umegawanyika katika Wilaya tatu ambazo ni Iringa, Kilolo na Mufindi. Mkoa pia umegawanyika katika Halmashauri nne ambazo ni Halmashauri ya Manipaa ya Iringa na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Kilolo na Mufindi.  Aidha Mkoa umegawanyika katika Tarafa 15 Kata 93, vijiji 357 na Mitaa 164.

Ndugu Wananchi,
Shughuli kuu za uchumi za Mkoa wa Iringa ni Kilimo, ufugaji, upasuaji mbao, uvuvi, biashara na ajira za maofisini na viwandani.  Asilimia 85 ya wakazi wa Iringa hujishughulisha na kilimo au kilimo na ufugaji na katika shughuli hizi tumepata mafanikio makubwa.

Ndugu Wananchi,
Tuko hapa leo kuadhimisha sherehe za miaka 51 ya uhuru wa Tanzania bara. Kauli mbiu ya sherehe za uhuru mwaka huu ni uwajibikaji , uadilifu na uzalendo ni nguzo ya maendeleo ya Taifa letu.

Ni ukweli usio pingika tukiwajibika ipasavyo, tukiwa waadilifu, na wazalendo kuanzia kweye kaya hadi Taifa tutalitumikia Taifa na kupata maendeleo yanayohitajika. Hivi vitu 3 ni msingi mkubwa sana wa maendeleo ya Nchi yetu, hivyo kila mmoja inampasa kutimiza kauli mbiu hii.


Ndugu Wananchi,
Mkoa wa Iringa umepata mafanikio makubwa toka tulipopata uhuru mpaka sasa kutokana na Waasisi wetu, wazazi na walezi wetu kuwajibika, kuwa waadilifu na kuwa wazalendo wa kweli katika kutekeleza majukumu yao. Miongoni mwa Mafanikio hayo ni pamoja na:- Mwaka 1961 pato la Mkoa lilikuwa ni Sh. 5,693,000 na Wastani wa pato la mtu kwa mwaka lilikuwa ni Sh. 103. Aidha, pato la Mkoa kwa mwaka 2011 lilikuwa Sh. 1,985,708,000 na pato la mkazi lilikuwa Sh. 1,225,503. Hii ni hatua kubwa kwa Mkoa wa Iringa.

Katika ukusanyaji wa Mapato ya Halmashauri mwaka 2011/12 Sh.9,357,013,391 zilikusanywa kutoka vyanzo vya ndani, kumekuwa na ongezeko la Sh. 9,355,366,502 ikilinganishwa na mapato ya Sh. 1,646,889 ya mwaka 1961/62.

Ndugu Wananchi,
Kilimo,  
Eneo linalolimwa mazao mbalimbali limeongezeka kutoka Hekta 305,208.65 mwaka 1961/62 hadi kufikia Hekta 411,116 zilizolimwa msimu 2011/12. Elimu ya kilimo bora ilitolewa kwa wakulima na jumla ya mashamba darasa 1,603 yalianzishwa na jumla ya wakulima 49,075 wamepatiwa mafunzo kwa vitendo kupitia mashamba haya kwa kipindi cha 1961 hadi 2011.Pia ili kufikisha Elimu kwa Wakulima waliowengi Mkoa umeanzisha vituo vya rasilimali watu wa Kilimo katika Kata 17.

Mbolea,
Mbolea zilizotumika mwaka 1961/62 zilikuwa tani 16,826 na tani 300 za mbegu. Ukilinganisha na tani 42,250 za mbolea na tani 3,142 za mbegu mwaka 2011 hii ni sawa na ongezeko la asilimia 251 kwa matumizi ya mbolea.

Ndugu Wananchi,
Mifugo,
Mwaka 1961 Mkoa ulikuwa na Idadi ya Ng`ombe wa Kienyeji 9,176, Idadi ya ng’ombe wa maziwa na nyama 19,  Majosho 69, Uzalishaji wa Maziwa lita 1,592,662. Hadi kufikia mwaka 2012 Mkoa una Ng’ombe kienyeji 568,749, Ng’ombe wa Maziwa 28,081, Majosho 211, uzalishaji wa Maziwa Lt 7,676,481.

Sekta ya Ushirika
Mwaka 1961 Mkoa ulikuwa na Vyama vya ushirika 2 vyenye Idadi ya Wanachama 460 na mtaji wa Tsh. 1,620,000. Hadi sasa Mkoa una jumla ya Vyama vya Ushirika hai 205 Vyenye Idadi ya Wanachama 36,873 na Mtaji wa Tsh 7,870,145,046.

Viwanda na Biashara
Mkoa hadi sasa unavyo viwanda 29 vinavyojihusisha na usindikaji wa bidhaa mbalimbali.  Sekta ya Viwanda na Biashara, inaajiri watu takriban 15,000 hii ni sawa na   asilimia 1.5 ya wakazi 1,006,731 wa Mkoa wa Iringa. 

Vyanzo vya maji
Hadi kufikia 2012 jumla ya vyanzo vya maji 2600 vilikuwa vimetambuliwa na jumla ya vyanzo 1752 vimehifadhiwa. Mkoa unaendelea na jitihada za kuhakikisha vyanzo vyote vinahifadhiwa.

Upandaji wa miti
Mwaka 1961 Jumla ya miti 3,507,802 ilipandwa katika Mkoa wa Iringa, Mwaka 2011 Mkoa umefanikiwa kupanda Jumla ya miti 43,515,611. Wananchi wanahamasishwa kuendelea kupanda miti ili kuweza kujipatika kipato na kuhifadhi mazingira. Mizinga hadi kufikia 2012 Mkoa unajumla ya Mizinga 25,783 ya asili ni 17,389 na ya Kisasa ni 8394.

Utalii
Katika kipindi cha 1961 hadi 2012, Mkoa umeainisha vivutio vya Utalii na unaendelea na zoezi hili kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Zaidi ya vivutio 78 vilikuwa vimetambuliwa hadi kufikia 2012.


Ndugu Wananchi
Elimu,
Kwa kipindi cha 1961 hadi 2012 yamepatikana mafanikio yafuatayo:
·        Kuongezeka kwa madarasa ya awali toka 67 hadi 425.
·        Kuongezeka kwa wanafunzi toka 3,015 Hadi 28,725.

Elimu ya Msingi.
Mkoa umekuwa na Maendeleo ya kuridhisha ya utoaji taaluma kwa kutumia kigezo cha matokeo ya mtihani wa kuhitimu Elimu ya Msingi. Katika kipindi cha 1961 hadi 2011 idadi ya wanafunzi waliofaulu imeongezeka kutoka 347 hadi 27,899 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 27,552.


Elimu ya Sekondari
Mwaka 1961 Mkoa ulikuwa na shule za Sekondari zipatazo 6, hadi Mwaka 2012 Mkoa unajumla ya shule za Sekondari 148, kati ya hizo za umma 104 na za Binafsi (Non-Government Secondary Schools) i.e. Seminari, na za Watu na Mashirika mbalimbali ya Binafsi 44.

Ndugu Wananchi,
Afya,
Mkoa wa Iringa hadi kufikia mwaka 2012 una jumla ya vituo vya kutolea huduma za Afya 254 vilivyogawanyika kama ifuatavyo; Hospitali 7, Vituo vya Afya 21 na Zahanati 226.

Kiwango cha mama wajawazito wanaojifungulia katika vituo vya tiba imeongezeka kufikia asilimia 88 mwaka 2011 ikilinganishwa na asilimia 5 mwaka 1961.

Ndugu Wananchi
Maji,
Asilimia ya wakazi wa Mkoa wa Iringa waliokuwa wakipata huduma ya maji safi na salama Desemba 1961 ni 10%.  Asilimia ya wakazi wanaopata huduma ya maji safi na salama Desemba 2011 ni 67.3 %.  Ongezeko la asilimia ya wakazi wanaopata huduma ya maji ni 56.4%.
Ndugu Wananchi,
Barabara,
Mwaka 1961 Mkoa ulikuwa na mtandao wa barabara upatao Km. 1,209.5 kati ya hizo Km. 76.0 ni barabara za vumbi na Km. 1,133.5 ni changarawe.  Mtandao huo Desemba 2011 umeongezeka hadi kufikia Km. 4,786 kati ya hizo Km. 359 ni Lami, Km. 2123 changarawe  na Km.2,304 ni udongo. 

Ndugu Wananchi, Teknolojia,
Mwaka 1961 Technolojia ya Kompyuta, Mawasiliano na habari haikuwepo Mkoani Iringa. Tulikuwa na Radio moja tu,  Radio Tanzania. Lakini hadi kufikia Mwaka, 2012 Mkoa wa Iringa umekuwa na Technolojia ya Habari, TV, Radio katika maeneo yote ya Mkoa wa Iringa. Mawasiliano yameimarika na wananchi wanafurahia maendeleo ya habari Mfano radio Ebony, Nuru, Country, Furaha, Ovecomers, Qibraten N.k.

Ndugu Wananchi,
Pamoja na mafanikio haya mkoa umepata changamoto mbalimbali ambazo ni pamoja na Mkoa wa Iringa umeathirika kwa kiwango kikubwa sana na tatizo la UKIMWI (asilimia 15.7). Hivyo nawaasa kila mmoja wetu anapaswa kubadili tabia ili kupunguza kiasi cha maambukizi.

Pia, naomba akibnababa msiwanyanyase akinamama na pia akinamama msiwanyanyase akinababa. Muendelee kuishi kwa upendo, utulivu na amani katika maisha yenu yote. Tupunguze kabisa unyanyasaji wa kijinsia.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ubariki Mkoa wetu wa Iringa.


Asanteni kwa Kunisikiliza.