Sunday, December 9, 2012

UHURU UENDE SAMBAMBA NA UWAJIBIKAJI NA UZALENDO




Wananchi na viongozi Mkoani Iringa wametakiwa kuongeza uwajibikaji na uadilifu kwa kutanguliza mbele uzalendo na maslahi ya Taifa katika shughuli zao za kila siku za kujiletea maendeleo yao na maendeleo ya Taifa.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akiwahutubia wananchi wa Mkoa wa Iringa wakati wa maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Tanzania Bara yaliyofanyika kimkoa katika Tarafa ya Mahenge Wilayani Kilolo.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (katikati) akisaini kitabu cha wageni, kushoto ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Josheph Muhumba na Helman Msua, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Wilaya ya Kilolo (kulia)

Dkt. Christine amesema “ni ukweli usiopingika tukiwajibika ipasavyo, tukiwa waadilifu, na wazalendo kuanzia kwenye kaya hadi Taifa tutalitumikia Taifa na kupata maendeleo yanayohitajika. Hivi vitu vitatu ni msingi mkubwa sana wa maendeleo ya nchi yetu, hivyo kila mmoja inampasa kutimiza kauli mbiu hii”.

Akiongelea mafanikio yaliyopatikana mkoani Iringa tokea Uhuru, Mkuu wa Mkoa ameyataja kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa pato la Mkoa na pato la mkazi. Amesema mwaka 1961 pato la Mkoa lilikuwa ni shilingi 5,693,000 na wastani wa pato la mtu kwa mwaka lilikuwa shilingi 103. Amesema kwa mwaka 2011 pato la Mkoa limekuwa na kufikia shilingi 1,985,708,000 wakati pato la mkazi limeongezeka na kufikia shilingi 1,225,503.
Katika ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri, Mkoa wa Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa kumekuwapo na ongezeko kubwa la ukusanyaji wa mapato hayo kwa mwaka 2011/2012 mapato ya Halmashauri yaliyokusanywa ni shilingi 9,357,013,391 kutoka vyanzo vya ndani, kukiwa na ongezeko la shilingi 9,355,366,502 yakilinganishwa na mapato ya mwaka 1961/1962 ya shilingi 1,646,889.
Kwa upande wa kilimo ambacho ni shughuli kuu ya kiuchumi, Dkt. Christine amesema kuwa Mkoa wa Iringa umefanikiwa kuongeza eneo linalolimwa kutoka Hekta 305,208.65 mwaka 1961/1962 hadi kufikia Hekta 411,116 mwaka 2011/2012. Amesema kuwa sambamba na kuongeza eneo hilo, pia elimu juu ya kilimo bora imeendelea kutolewa kwa wakulima na jumla ya mashamba darasa 1,603 yameanzishwa wakati wakulima 49,075 wamepatiwa mafunzo kwa vitendo kupitia mashamba hayo kwa kipindi cha kuanzia mwaka 1961 hadi mwaka 2011. Amesema katika kuhakikisha kuwa elimu inawafikia wakulima wengi, Mkoa umeanzisha vituo vya rasilimali watu wa kilimo katika kata 17.

Amesema kuwa Serikali imeendelea kuhimiza matumizi ya mbolea katika kilimo ili kuwawezesha wakulima kupata mazao mengi na bora. Amesema Mkoa wa Iringa umeweza kuongeza matumizi ya mbolea toka tani 16,826 na tani 300 za mbegu hadi kufikisha tani 42,250 za mbolea na tani 3,142 za mbegu kwa mwaka 2011.

Katika salamu zake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, Joseph Muhumba, amesema kuwa matunda ya Uhuru wa Tanzania Bara ni mengi na katika wilaya ya Kilolo wanayachukulia kuwa ni heshima kubwa na kuipa uzito mkubwa. Amesema kuwa ili heshima hiyo iendelee kuenziwa, ni lazima wananchi kufanya kazi kwa bidii, kutunza amani na utulivu vilivyopo katika Wilaya, Mkoa na Taifa kwa ujumla. Muhumba ambaye pia ni diwani wa Kata ya Image amesema kuwa Uhuru utaendelea  kumhamasisha kila mwananchi kuongeza juhudi katika kufanya kazi halali za kujiletea maendeleo yake binafsi ya maendeleo ya ujumla.  

Akiwasilisha Taarifa fupi ya maadhimisho ya miaka 51 ya Uhuru na maendeleo yaliyopatikana katika wilaya ya Kilolo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Helman Msua, amesema kuwa pamoja na Wilaya hiyo kuanzishwa mwaka 2002 bado imepiga hatua sana katika nyanza mbalimbali. Akitolea mfano juhudi za kukuza kilimo kupitia matumizi ya zana bora za kilimo, amesema mwaka 2002 Wilaya yake ilikuwa na matrekta makubwa 41 na hadi kufikia mwaka 2002 matrekta hayo yameongezeka hadi kufikia 52. Amesema kuwa vyama vya ushirika vimeongezeka toka 15 mwaka 2002 hadi kufikia 54 mwaka 2012.

Miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara inaadhimishwa nchini kote ikiongozwa na kauli mbiu isemayo “uwajibikaji, uadilifu na uzalendo ni nguzo ya maendeleo ya Taifa letu”.
=30=

No comments:

Post a Comment