Tuesday, October 23, 2012

MKOA WA IRINGA WATAKIWA KUSHIRIKIANA NA RUBADA




Mkuu wa Mkoa wa Iringa ametoa wito kwa viongozi wa mkoa wake kutoa ushirikiano wa kutosha kwa mamlaka ya uendelezaji wa bonde la mto Rufiji (RUBADA) ili kuwawezesha kuratibu na kusimamia vizuri mipango kabanbe ya kuendeleza shughuliza kilimo kwa ukanda wa kusini mwa Tanzania (SAGCOT).

Katika hotuba ya ufunguzi wa kikao cha viongozi na wataalamu wa mkoa wa Iringa kuhusu uendelezaji wa SAGCOT uliofanyika katika ukumbi wa VETA mjini Iringa iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Gerald Guninita kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma.

Mgeni rasmi Gerald Guninita ambae ni Mkuu wa Wilaya ya Kilolo (katikati) akisoma hotuba wakati wa ufunguzi wa kikao cha viongozi na wataalamu wa mkoa wa Iringa kuhusu uendelezaji wa SAGCOT


wajumbe wa kikao cha viongozi na wataalamu wa mkoa wa Iringa kuhusu uendelezaji wa wa SAGCOT 


Amesema RUBADA imepewa majukumu ya kusimamia na kuratibu mipango ya SAGCOT ili malengo ya mipango hiyo yaweze kutekelezwa vizuri na kuinua hali ya wananchi nchini. Amesema katika kufanikisha hili RUBADA inatafuta na kutenga maeneo kwa ajili ya uwekezaji wa kilimo chenye tija na viwanda kwa lengo la kuleta mapinduzi ya kijani. Amesema katika hilo RUBADA kwa kushirikiana na wilaya husika itaandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji ili maeneo ya uwekezaji yabainishwe na kutengwa kwa ajili ya wawekezaji watakayoyaendeleza pamoja na wakulima wadogo wadogo wanaoyazunguka maeneo ya miradi hiyo.

Guninita amesema kwa kuzingatia kazi nzuri inayofanywa na RUBADA katika kutekeleza mipango hiyo, ushirikiano wa viongozi na wataalamu hao ni chachu katika ufanikishaji wa malengo hayo. Ameelezea matarajio yake kwa viongozi na wataalamu hao baada ya kikao hicho kuwa watakuwa mabalozi wazuri wa kuwaelimisha wananchi katika maeneo yao ili wawe washiriki wazuri katika kutekeleza mpango huo.

Akiwasilisha mpango wa SAGCOT Mkurugenzi Mkuu wa uendeshaji wa bonde la Rufiji, Aloyce Masanja amesema kuwa hakuna nchi iliyofanikiwa duniani kuichumi na kuondokana na umasikini pasipo mapinduzi ya kilimo na viwanda. Akiongelea takwimu, amesema kuwa asilimia 65 ya malighafi za viwanda zinatokana na kilimo wakati asilimia zaidi ya 55 ya mfumuko wa bei huchangiwa na mazao ya kilimo. Amesema katika hekta milioni 44 zinazofaa kwa kilimo ni asilimia 23 pekee ndiyo zimetumika.
Akiongelea tofauti kati ya kilimo kwanza na sera nyingine zilizopita, Masanja amesema kuwa mipango na jitihada za zamani ziliibuliwa, kupangwa na kutekelezwa na serikali na mashirika yake pasipo kuwahusisha wadau wengine kikamilifu. Amesema tofauti na mipango ya awali kilimo kwanza ni mtazamo mpana wa mabadiliko ya kisekta na uzoefu uliopatikana kutokana na mipango iliyotekelezwa hapo awali na sasa kilimo kwanza kimeshirikisha wadau wote.   

Mkurugenzi Mkuu wa uendeshaji wa bonde la Rufiji ameyataja malengo ya SAGCOT kuwa ni kutatua matatizo yanayoikabili sekta ya kilimo hasa upatikanaji wa mitaji, vyama vya wakulima, miundombinu ya kilimo, uharibifu wa mazingira, ukosefu wa masoko, uwekezaji mdogo katika kilimo na uboreshaji wa sera zinazohusu kilimo. Amesema malengo mengine ni kuwahamasisha wakulima wadogo na kuwaunganisha katika vikundi na kuwafanya walime kilimo cha kibiashara.

Masanja amesema kuwa RUBADA imekuwa pia ikiwapa kipaumbele vijana katika shughuli mbalimbali za kujiongezea kipato. Amesema “kila tunapoanzisha miradi ya RUBADA tunakuwa tukianzisha kambi za vijana ambapo tunawafundisha mbinu bora za kilimo na matumizi ya dhana za kilimo” amesisitiza Masanja.

=30=