Wednesday, May 16, 2018

IRINGA KUENDELEZA MAZAO YA BIASHARA


Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Mkoa wa Iringa unaendelea kuweka mikakati ya kuendeleza mazao ya korosho, pamba na kahawai ili yachangie katika kukuza uchumi wa wakulima na mkoa kwa ujumla.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifungua jukwaa la ushirika mkoa wa Iringa kililofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo hivi karibuni.

Masenza alisema kuwa serikali inatambua mazao matano ya kimkakati na kuyataja kuwa ni korosho, kahawa, tumbaku, pamba na chai. 

Mkoa wetu wa Iringa una hali ya hewa nzuri inayofaa kwa kilimo cha mazao yote. Kumekuwa na maendeleo mazuri katika kilimo cha chai ambapo uzalishaji umefikia kiasi cha tani 18,930 kwa mwaka 2016/2017, kwa mazao ya korosho, pamba na kahawa mkoa wetu unaendelea kuweka mikakati thabiti wa kuyaendeleza” alisema Masenza.

Halmashauri zimeanza kuweka jitihada za kuhamasisha kulima mazao hayo alisema. “Kupitia jukwaa hili nawaagiza wakurugenzi wa halmashauri kukaa chini na vyama vya ushirika kuandaa mpango wa miaka mitano wa kuendeleza mazao hayo” aliagiza Masenza.

Alisema kuwa wananchi wakihamasishwa kuzalisha mazao hayo kwa wingi, kutawaongezea wanaushirika kushiriki shughuli za uzalishaji mazao ya kibiashara na kuongeza kipato cha wanaushirika na wananchi kwa ujumla.

Akiongelea zao la tumbaku, mkuu wa mkoa alisema kuwa mkoa wa Iringa umekuwa ukizalisha tumbaku kwa zaidi ya miaka 50 lakini zao hili halijatoa mchango mkubwa kiuchumi kwa wananchi. 

Napenda kutoa rai kuwa tunatakiwa kujipanga upya ili kuendeleza uzalishaji wa zao hili. Uzalishaji wa zao la tumbaku umekumbwa na changamoto mbalimbali zikiwemo ukosefu wa soko na uwepo wa madeni makubwa katika vyama vya msingi ambayo yanasababishwa na wanachama kutouza kupitia vyama vyao. Nachukua fursa hii kuwaasa wakulima wa zao hili kuzingatia taratibu za kilimo hicho hasa kutowatumia watoto, kupanda miti na kuuza kwa uaminifu kupitia vyama vya ushirika” alisisitiza Masenza.

Jukwaa la ushirika ni jukwaa la pili kufanyika ngazi ya mkoa, likishirikisha Katibu Tawala Mkoa, wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa, wadau wa taasisi za kifedha na wanaushirika.
=30=

No comments:

Post a Comment