Saturday, January 1, 2011

HOSPITALI YA MKOA IRINGA YAPONGEZWA

Hospitali ya Mkoa wa Iringa imepongezwa kwa kutoa huduma nzuri kwa wagonjwa wanaohudhuria hospitali hiyo kwa matibabu.

Pongezi hizo zimetolewa na Mbunge wa viti maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Ritta Semotto Kabati alipofanya ziara fupi ya kuwatembelea wagonjwa waliolazwa katika wodi ya akina mama na wodi ya watoto leo kwa lengo la kuwapa pole, na kuwatakia heri ya mwaka mpya 2011.
Mhe. Ritta Kabati, Mbunge wa CCM viti maalum (kulia) akimkabidhi baadhi ya zawadi
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa Iringa, Dkt. Oscar Gabone
katika viwanja vya Hospitali hiyo leo

Mhe. Kabati amesema “naipongeza hospitali ya mkoa wa Iringa kwa kutoa huduma nzuri na bora jambo linalowafanya wagonjwa kuridhika na huduma inayotolewa”. Ameongeza kuwa ametembelea hospitali mbalimbali lakini katika suala la usafi hospitali ya mkoa ipo juu.

Mhe. Kabati amesema lengo la kufanya ziara hiyo fupi ni kuwafariji na kuwatia moyo akina mama na watoto na kuwapa zawadi mbalimbali ikiwa ni pongezi zake kwa kufanikiwa kuuona mwaka mpya wa 2011.  “Nawapa pole sana wagonjwa wote na nawatakia afya njema kwani kuugua si kufa na pia naomba wote tuuanze huu mwaka mpya kwa furaha na uwajibikaji ili kuweza kujiletea maendeleo”.

Sikujua Filango, mama aliyejifungua mtoto saa tisa usiku wa tarehe 01.01.2011 ameelezea kurithishwa na huduma za hospitalini hapo tangu alipowasili hadi alipojifungua.

Akielezea changamoto zinazoikabili hospitali ya mkoa, Katibu wa Hospitali, Dotto Zambalesi amesema kuwa hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa watumishi wenye taaluma stahiki akidai waliopo kuwa ni wachache hatimae kuwa na jukumu zito kidogo kwa wataalamu waliopo kuweza kuziba pengo la watumishi wanaopungua. Aidha changamoto nyingine ameiongelea kuwa ni ufinyu wa bajeti jambo linalokwamisha ufanisi katika baadhi ya shughuli.

Mhe. Rita Kabati Mbunge viti maalum CCM (katikati) akiwa na
mama Felisha (kushoto) na mama ambaye mtoto hajampatia jina (kulia)
baada ya kuwakabidhi zawadi alipotembelea wodi ya akina mama leo

Akitoa shukrani zake kwa ziara hiyo mganga mfawidhi wa hospitali hiyo Dkt. Oscar Gabone amemshukuru Mhe. Mbunge na msafara wake na zawadi walizozitoa katika wodi ya akina mama na wodi ya watoto na kueleza matumaini yake kuwa ziara ijayo itahusisha zawadi za akina baba pia.

Katika ziara hiyo Mbunge huyo aliambatana na akina mamawa UWT mkoa na wilaya na baadhi ya waheshimiwa madiwani na kutoa zawadi za sabuni, maziwa, juice na biskuti pamoja na vitu vingine.


Baadhi ya wajumbe katika ziara ya Mhe. Kabati wakibadilishana mawazo na viongozi wa Hospitali ya Mkoa
WANANCHI WATAKIWA KUTAFAKARI CHANGAMOTO ZA KIJAMII

Serikali mkoani Iringa imetoa wito kwa waumini na wananchi kutafakari changamoto zilizojitokeza katika jamii na kusababisha uvunjaji wa amani na mshikamano katika kuukaribisha mwaka mpya 2011.

Kauli hiyo imetolewa na kaimu Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kanali Issa Machibya katika hotuba yake iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista Kalalu katika mkesha mkubwa wa kitaifa uliofanyika katika uwanja wa Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa.



       Askofu Dkt. Oderdenburg Mdegela akiteta jambo la Mwakilishi wa
Mkuu wa Mkoa wa Iringa ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista Kalalu. 
Bibi Kalalu amesema “natoa wito kwa waumini na wananchi wote kwamba tunapoukaribisha mwaka mpya, kila mmoja wetu atafakari ni mambo gain au changamoto zipi zilizojitokeza katika jamii na kusababisha uvunjifu wa amani na mshikamano wetu”. Amezitaja changamoto hizo kuwa ni pamoja na rushwa, mauaji ya walemavu wa ngozi (Albino), ubakaji, utoaji mamba, mauaji ya vikongwe na mauaji ya watu yanayoendelea kujitokeza.

Aidha, amesema kuwa changamoto hizo zimesababishwa na mmomonyoko wa maadili katika jamii na kusisitiza kuwa waumini wa dini zote na madhehebu yote kuweka nguvu katika kuliombea taifa liepukane na mmomonyoko wa maadili. Amewataka kila mmoja kuwa mwalimu wa kutenda matendo mema yenye kumpendeza Mungu na kuendelea kudumisha amani iliyopo.

Vilevile amewataka waumini wote kuwaombea viongozi wa taifa kwa Mungu ili hekima, busara na ujasiri wa kutawala kwa moyo wa uadilifu. Ameongeza kuwa kila mwanajamii kwa nafasi yake awajibike katika kuleta maendeleo yake binafsi, kudumisha amani, mshikamano na maadili mema katika jami nzima.

Katika neno la utangulizi lililotolewa na Mhashamu Baba Askofu Dr.Oderdenburg Mdegela amesema dhumuni la mkesha huo ni kuiombea nchi ili iwe na amani, “tumekuja kuomba na kutembea pamoja ili nchi iwe na amani”. Amesema kuwa toba ni msingi wa kumkaribia Mungu na Mungu huleta mabadiliko katika familia, kazi, biashara na Taifa. Amesema kuwa mkesha huo ni mafuriko na utamfunika kila mtu katika kutenda mema. Aidha, aliwashukuru wale wote waliohusika kuruhusu uhuru wa kuabudu nchini pasipo kuvunja sheria.

Baadhi ya wakazi wa Manispaa ya Iringa wakipokea
baraka kavika uwanja wa Samora mkesha wa mwaka 2011



...MAISHA BORA YANATOKANA NA KUFANYA KAZI KWA JUHUDI NA MAARIFA!

Wananchi wamekumbushwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kujiletea maisha bora na si kutegemea kuwa maisha mazuri yanateremka kutoka juu.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Bibi Evarista Kalalu katika hafla fupi ya kukabidhi mkopo wa zana za kilimo trekta kubwa manane na ndogo 25 uliotolewa na Idodi SACCOS iliyofanyika katika viwanja vya ofisi ya Idodi SACCOS zilizopo katika Kata ya Idodi, Tarafa ya Idodi katika  Halmashauri ya Iringa.
Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista Kalalu akikabidhi mkopo wa Trekta

Bibi Kalalu amesema kuwa maisha rahasi kwa jamii yanatengenezwa kwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa na si kukaa na kusubiri muujiza kutoka juu. Ameongeza kuwa vijana wengi wamekimbilia maisha wanayodhani ni rahisi hasa mijini na kujikuta wanaharibikiwa na kupoteza muelekeo hivyo kuagiza vijana washawishiwe kutokimbilia maisha hayo na wajiingize katika kilimo na vyama vya ushirika wa akiba na mikopo (SACCOS). Ametanabaisha kuwa usalama wa Tarafa ya Idodi na Mkoa wa Iringa utatokana na kushawishiwa huko kwa vijana kufanya kazi mbalimbali na si kupoteza muda na muelekeo katika maisha.

Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Iringa ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Mufindi amefafanua madhumuni ya kuanzisha vyama vya ushirika vya akiba na mikopo (SACCOS) mwanzoni mwa miaka ya 2000 kuwa ni mkakati wa serikali kuwakomboa wananchi wake. Amesema “nguvu za wananchi zikiwekwa pamoja kwa malengo mahususi unakuwa ni mtaji mkubwa sana” hivyo kuwataka wananchi wengi zaidi kujiunga katika vyama vya akiba na mikopo ili kuunganisha nguvu zao. Amesema “wanaidodi wengine wasio wanachama wawe tayari kujifunza na kujiunga kutoka SACCOS”.

Alichukua nafasi hiyo kuzitaka kata nyingine kubuni bidhaa nyingine isiyopatikana katika Kata ya Idodi ili kuongeza wigo wa utoaji huduma katika Tarafa mzima ya Idodi jambo litakalodumisha ushirikiano na udugu.  

Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Lucy Nyallu amesema kuwa kilimo cha kisasa hakitegemei kubahatisha bali kinategemea matumizi sahihi ya mbolea, uchaguzi wa mbegu bora na ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wataalamu wa kilimo.

Mwenyekiti wa SACCOS hiyo Ngoola Mwangosi amezitaja changamoto zinazoikabili SACCOS hiyo kuwa ni pamoja na wadau wa mikopo ya stakabadhi mazao kutotoa mikopo ya kukopesha kwa wakati, na baadhi ya wanancha kutorejesha mikopo kwa wakati. Ameitaja changamoto nyingine kuwa ni wananchama kutokuwa na zana za kisasa za kilimo na kusababisha uzalishaji duni.

Chama cha ushirika wa akiba na mikopo (Idodi SACCOS DYK) kilisajiliwa rasmi Disemba, 2004 kikiwa na wanachama 178 na vikundi vya wajasiliamali sita kikiwa na hisa zenye thamani ya Tsh. 3,600,000, akiba Tsh. 107,286,400 na amana Tsh. 7,200,000.