Wednesday, May 16, 2018

IRINGA YATEKELEZA AGIZO LA SERIKALI KUIMARISHA USHIRIKA


Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Mkoa wa Iringa unatekeleza agizo la serikali ya awamu ya tano la kuufanya ushirika kuwa nguzo ya kuwasaidia wakulima.

Kauli hiyo ilitolewa na kaimu Mrajis msaidizi wa vyama vya ushirika mkoa wa Iringa, Robert George alipokuwa akisoma taarifa ya hali ya ushirika katika mkoa wa Iringa katika jukwaa la ushirika mkoa wa Iringa lililofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa hivi karibuni.
Kaimu Mrajis Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Iringa, Robert George

George alisema kuwa mkoa unaendelea kutekeleza agizo la serikali la kujenga ushirika imara unaomsaidia mkulima. 

“Katika kuhakikisha kuwa ushirika unakuwa imara na kuongeza idadi ya wanachama kama lilivyo agizo la Serikali ya awamu ya tano ambalo linatuhitaji sisi kama wasimamizi wa ushirika kuhakikisha kuwa ushirika unakuwa ndio nguzo ya kumsaidia mkulima. Kwa mwaka 2017/2018 jumla ya vyama vya ushirika 8 vimeandikishwa zikiwepo SACCOS 5 na AMCOS 3” alisema George.

Uhamasishaji wa vyama vilivyosinzia ili viweze kuamka umefanyika kupitia chama kikuu cha ushirika na maafisa ushirika, jumla ya vyama vya ushirika vitano vimeamka ambavyo ni Magulilwa AMCOS Ltd, Ipilimo AMCOS Ltd, Matanana AMCOS Ltd, MVIKIMA SACCOS Ltd na Ikimo AMCOS Ltd.

Akiongelea utekelezaji wa maagizo ya serikali kuhusu mazao ya kimkakati, Mrajis msaidizi mkoa wa Iringa alisema kuwa halmashauri zimehamasisha kilimo cha mazao ya korosho na pamba katika kata za Nzihi na Malengamakali kupitia vyama vya ushirika vya Nzihi mixed na Usolanga.

Aliongeza kuwa mkoa unaendelea kusimamia na kuviimarisha vyama vya ushirika vitatu vinavyojishughulisha na kilimo cha chai. Vyama hivyo alivitaja kuwa ni Mkonge Amcos, Sawala Amcos na Luhunga Amcos. 

Kwa mwaka 2017/2018 jumla ya vijiji vitano vimehamasishwa kuanzisha vyama vya ushirika vya kilimo cha chai katika halmashauri ya Mufindi. Vijiji hivyo ni Igoda, Kibao, Udumka, Mninga na Makalala” alisema George.

Halmashauri zinaendelea kuhamasisha kilimo cha kahawa, korosho na pamba aliongeza. “Kwa msimu huu wa mwaka 2017/2018 wakulima wa halmashauri wilaya ya Iringa wamepanda karosho kwa wingi hivyo, kwa maeneo yote yaliooteshwa korosho uhamasishaji wa kuanzisha vyama vya ushirika utafanyika katika msimu wa 2018/2019. Kutokana na jiografia ya maeneo mbalimbali ndani ya mkoa wetu mazao yote ya kimkakati yanaweza yakastawishwa na wanachama wa vyama vya ushirika” alisema George.

Jukwaa la ushirika ni jukwaa la pili kufanyika ngazi ya mkoa, likishirikisha Katibu Tawala Mkoa, wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa, wadau wa taasisi za kifedha na wanaushirika.
=30=

No comments:

Post a Comment