Sunday, August 5, 2012

WAKULIMA NA WASINDIKAJI WAWEZESHWE ASEMA RC IRINGA



Halmashauri za Wilaya na Manispaa zimeshauriwa kuwasaidia wakulima na wajasiliamali wasindikaji katika kuhakikisha bidhaa zao zinafikia viwango vya ubora vinavyotakiwa ili kujihakikishia soko la uhakika.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipotembelea mabanda ya wajasiliamali na wasindikaji katika maonesho ya Nanenane katika Uwanja wa John Mwakangale -Uyole Mbeya katika siku ya Iringa Day.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. christine Ishengoma (kulia) akibadilishana mawazo na Mkurugenzi wa Fama Food Processing, Genovefa barnabas katika Uwanja wa Maonesho ya NaneNane Mbeya

Dkt. Christine amesema kuwa wakulima wasindikaji wanafanya kazi kubwa sana katika kusindika bidhaa za kilimo kwa kutumia juhudi zao wenyewe, hivyo kujikuta wakikwama katika utaalam na kushauri wawe wanapatiwa mafunzo na ushauri wa kitaalam ili kuufanya usindikaji wao uwe wa kisasa zaidi.

Amesema ni vizuri Halmashauri za Manispaa na Wilaya ziangalie jinsi ya kuwasaidia kitaalam na kiufundi ili bidhaa za usindikaji ziweze kufikia viwango vinavyokubalika na kupata lebo ya shirika la ubora (TBS). “watu wengi sasa wanaangalia lebo ya TBS ili kijihakikishia ubora hivyo ni vizuri mkahakikisha bidhaa zenu zinafikia ubora unaopkubalika na kupata lebo ya ubora” amesisitiza Dkt. Christine.

Akiongelea changamoto zinazowakabili wajasiliamali wasindikaji, mjasiliamali na mmiliki wa Fama Food Processing, Genovefa Barnabas amesema kuwa changamoto kubwa inayowakabili wajasiliamali hasa wa Mkoa wa Iringa ni maeneo mahususi ya kuwawezesha kuzalishia bidhaa zao ili ziweze kupata uthibitisho wa ubora unmaotakiwa.  Akifafanua zaidi amesema “ili mjasiliamali anu wajasiliamali tuweze kutimiza ndoto zetu za kufanya shughuli za ujasiliamali vizuri ni vizuri serikali ikatusaidia kutenga maeneo ambayo yatakuwa mahususi kwa shughuli za ujasiliamali ambapo kila kitu kitakuwa kinafanyika hapo”. Amesema “kuanzia mazao na bidhaa zinapoletwa kutoka maeneo mbalimbali zinapokelewa katika eneo hilo, zinaanza kutengenezwa katika eneo hilo, zinapakiwa katika kontena, kufungwa na kuwekwa lebo hapohapo, kwa lugha nyingine mchakato wote unafanyika katika eneo moja hadi kwenda kwa mlaji”.

Akitetea umuhimu wa eneo hilo kwa wajasiliamali, Barnabas amesema kuwa eneo hilo lina umuhimu mkubwa kwa sababu kupatikana kwake kutawawezesha kupata cheti cha ubora wa bidhaa toka shirika la viwango (TBS). Amesema kitendo cha kupata lebo ya ubora toka TBS kutawafanya watu wengi zaidi kujiridhisha na ubora wa bidhaa hizo.  

Nunu Mtatifikolo ambaye ni Mwenyekiti kikundi cha Wanawake cha JAFAKU amesema changamoto ya watanzania kukubali bidhaa zinazozalishwa na wajasiliamali wazalendo wa ndani ni mwiba katika ukuaji wao. “amesema ipo kasumba inayoendelea kutudidimiza ya wananchi kupenda bidhaa za nje tofauti na zinazozalishwa na wajasiliamali wa ndani”.

Amesema ili kuondokana na kasumba hiyo elimu inahitajika kutolewa kwa wananchi ili waweze kutumia bidhaa zinazozalishwa ndani ya nchi. “Elimu hiyo itasaidia sana kubadili kasumba hii na elimu hii inatakiwa kuambatana na matangazo ya bidhaa za wajasiliamali” amesisitiza Mtatifikolo.

Mwenyekiti wa kikundi cha Wanawake wa KKKT-Nduli, Laurencia Malila amesema katika banda la Manispaa ya Iringa amesema kuwa wanawake wajasiliamali Mkoani Iringa wanakabiliwa na changamoto ya masoko kwa maana ya wanunuzi wa bidhaa zao. Amesema “pamoja na kuwa na bidhaa nzuri bado wananchi wanamuitikio mdogo wa kuzinunua jambo linalowafanya washindwe kuzalisha bidhaa kwa wingi”.  

Malila ambaye pia kikundi chake kinajihusisha na kilimo cha kisasa na ufugaji wa nyuki kikiwa na mizinga 47 ya nyuki ya kisasa, ametoa wito kwa watu wanaopenda kujifunza kilimo cha kisasa cha mahindi na maharage pamoja na ufugaji wa nyuki kuwatenbelea ili kujifunza katika mashamba darasa yao yaliyopo katika kata ya Nduli.

=30=

DR. ISHENGOMA ASISITIZA KILIMO CHA KISAYANSI



Zana ya Kilimo Kwanza itafanikiwa kwa wakazi wa kanda ya Nyanda za Juu Kusini kulima kilimo cha kisayansi na kiteknolojia zaidi na kukifanya kilimo kiwe cha kibiashara.

Ushauri huo umetolewa katika majumuisho baada ya mgeni rasmi Dkt. Christine Ishengoma kutembelea mabanda ya maonesho ya Nanenane kanda ya nyanda za Juu Kusini katika siku ya mkoa wa Iringa (Iringa Day) iliyofanyika katika uwanja wa maonesho ya Nanenane wa John Mwakangale Uyole Mbeya.

Dkt. Chrisrine ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema “kimsingi kilimo kwanza ni Nyanda za Juu Kusini yaani Mikoa ya Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Rukwa na Katavi kwa kuwa mikoa hii ndio wazalishaji wakubwa nchini, hivyo huwezi kutenganisha Kilimo Kwanza na Nyanda za Juu Kusini”.  Amesema katika kuendeleza kilimo katika ukanda huo ni lazima kilimo kiwe cha kisayansi na kiteknolojia zaidi ili kuwawezesha wakulima kulima maeneo madogo lakini kwa kupata mazao mengi zaidi na yenye ubora unaotakiwa. Amesema kuwa wakulima wameendelea kupata hasara katika kilimo kwa kutokufuata kanuni za kilimo bora jambo linalowafanya waweke nguvu nyingi katika kilimo lakini matokeo wanayoyapata hayaendani na nguvi halisi waliyowekeza katika kilimo hicho. Aidha, ametoa wito kwa wataalam wa kilimo kuwa karibu zaidi na wakulima ili kuwafundisha waweze kuepukana na kilimo cha kizamani na kimazoea.
Hapa huitaji maelezo zaidi ya picha kujieleza yenyewe

Akiongelea kuhama kutoka katika kilimo kidogo kwa ajili ya kujitosheleza kwa chakula, amesema “umefika wakati sasa wa kuhama kutoka katika kilimo cha kawaida na kukifanya kilimo chetu kiwe cha kibiashara. “Na hili litawezekana pale tu tutakapokifanya kilimo chetu kuwa kilimo cha kisayansi zaidi” amesema Dkt. Christine.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Iringa amesema baada ya kutembelea mabanda ya maonesho mikoa yote inafanya vizuri. Amesisitiza kuwa ili maonesho hayo yawe mazuri zaidi ni vema maandalizi yake yakaanza mapema zaidi katika Halmashauri zote.

Akielezea nini amejifunza katika maonesho hayo, amesema kuwa amejifunza mambo mengi sana ambayo baadhi hakuwa akiyafahamu kabisa, baadhi amejikumbusha baada ya kupita muda mrefu tokea ayafahamu na kusema “maonesho yaha yamekuwa ni shamba darasa kwa watu wengi”. Baada ya kujionea ubunifu wa kiteknolojia kutoka kwa wananchi mbalimbali, ametoa wito kwa mikoa hiyo ya nyanda za juu kusini kuwaangalia wabunifu hao kwa jicho la pekee ili waweze kuwaendeleza zaidi na wao kunufaika na ubunifu wao. Amesema kuwa imani yake ni kwamba pale juhudi za pamoja zitakapowekwa hakika kilimo kitatoka katika hali yake ya sasa na kuwa bora zaidi.

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameweka rekodi katika maonesho hayo ya Nanenane baada ya kutembelea mabanda 40 ya maonesho kwa siku na kupokea maelezo na kuuliza baadhi ya maswali kwa waoneshaji mbalimbali.

=30=

RC IRINGA ALIPOTEMBELEA MABANDA YA 8 8 KATIKA UWANJA WA JOHN MWAKANGALE



 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma (mwenye sutu ya zambarau) akikagua zana alipotembelea Banda la Halmashauri ya Wilaya ya Iringa


  Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma (mwenye sutu ya zambarau) akikagua Mambo ya Lishe alipotembelea Banda la Halmashauri ya manispaa ya Iringa


 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma (mwenye sutu ya zambarau) akipokea maelezo ya Malisho ya Mifugo


 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma (mwenye sutu ya zambarau) katika picha ya pamoja alipotembelea banda la Mamlaka ya Hali ya Hewa. 


Mama Kiula ajumuika na wadau katika kutembelea Maonesho ya Nanenane Mbeya

 Banda la Manispaa ya Iringa 

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr. Christine Ishengoma akisaini Kitabu cha Wageni katika banda la Manispaa ya Iringa

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dr Christine Ishengoma akibadilishana mawazo na Mjasiliamali jasiri, Genoveva Barnabas

Dr. Ishengoma katika banda la ASAS  

 RC Iringa akikagua banda la Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, kulia ni kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa


 Mkuu wa Mkoa wa Iringa  akikagua mabanda ya Maonesho kulia kwake ni Shenal Nyoni

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa akipokea maelekezo katika banda la Halmashauri ya Wilaya Wilaya ya Iringa

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dr. Christine Ishengoma akisaini Kitabu cha wageni katika banda la Halmashauri ya Wilaya ya Iringa

Dr. Christine Ishengoma akioneshwa note feki na noti halisi za 10,000.