Saturday, November 5, 2011

...CLUB RAS IRINGA YAAGWA

Mwenyekiti wa Kamati ya michezo ya Mkoa wa Iringa ameitaka timu ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa (Club ya RAS Iringa) kuhakikisha inafanya vizuri katika michuano ya shirikisko la michezo na wizara, mikoa, idara na wakala wa serikali kuu (SHIMIWI) na kurudi na kombe la ubingwa.

Mwenyekiti wa kamati ya michezo mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka (kushoto) akimkabidhi viatu vya michezo Mwenyekiti wa Club ya RAS Iringa Dr. Oscar Gabone tayari kwenda Tanga kushiriki mashindano ya SHIMIWI

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Michezo wa Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka leo wakati akiiaga timu hiyo maarufu kama Ras Iringa inayojiwinda na michuano ya SHIMIWI inayotarajiwa kuanza kurindima jijini Tanga leo tarehe 5.11. 2011.

Mpaka amesema kuwa michezo ni furaha, upendo na afya hivyo ni jukumu lenu wanamichezo kuhakikisha michezo inatumika katika kudumisha furaha, upendo na afya.

Amesema hayo yakizingatiwa ni dhahiri kuwa timu hiyo itafanya vizuri na pamoja na kurudu na kombe la ushindi pia ameigaziza kurudi na ushindi wa nidhamu.
Akiongea kwa kujiamini, Mpaka ambaye pia ni Katibu Tawala Mkoa wa Iringa na aliyeanzia kazi katika Mkoa wa Tanga kwa nafasi hiyo aliyonayo kwa sasa amesema ninajivunia timu ya wanamichezo iliyojiandaa kiushindani na yenye wachezaji walioshiba vilivyo.

Amesema “SHIMIWI tunaenda kushindana pia kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru chini ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo” na kuwataka wanamichezo kushindana huku wakitafakari mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika miaka hiyo 50.

Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa Michezo Mkoa wa Iringa, Mwenyekiti wa SHIMIWI Club ya RAS Iringa, Dk. Oscar Gabone amesema kuwa wanamichezo hao wameiva na kutokana na ari waliyonayo wanaona kama wanachelewa kuanza michuano hiyo ikiwa ni pamoja na kukabidhiwa ushindi wake.

Akitoa shukrani kwa niaba ya timu hiyo, Afisa Michezo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kenneth Komba, amemshukuru Katibu Tawala Mkoa wa Iringa kwa utayari wake kuwasaidia wanamichezo na michezo kwa ujumla katika Mkoa wa Iringa. Paamoja na kuahidi kurudi na kombe pia alimhakikishia kuendelea kuwa wamoja.

Michezo hiyo inatarajiwa kufunguliwa na Waziri ,wenye dhamana ya michezo nchini, Dk. Emmanuel Nchimbi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ametoa salamu za Iddi El Hajji kwa watoto wa makao ya watoto ya Tosamaganga akiwatakia heri katika sherehe hiyo.

Salaam hizo zimetolewa na katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka kwa niaba ya Rais, Dk. Kikwete katika kituo cha makao ya kulelea watoto ya Tosamaganga.
 Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka (kulia) akikabidhi zawadi ya mbuzi kutoka kwa Rais Kikwete kwa kituo cha makao ya watoto cha Tosamaganga




 Baadhi ya watoto wqanaolelewa katika kituo cha makao ya watoto Tosamaganga


Gertrude amesema “nimekuja hapa kufanya mambo makubwa mawili: jambo la kwanza nimekuja kuwafikishia salamu za Iddi El Hajji kutoka kwa Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anawatakia heri na fanaka kwa iddi El Hajji”.

Gertrude amesema Mhe. Rais amefarijika sana kushiriki na watoto hao katika kusherehekea sikukuu hiyo ya Iddi El Hajji “alipenda kuwa nanyi hapa, lakini kutokana na majukumu kuwa mengi ametuma salamu za kuwatakia heri na fanaka kwa Iddi El Hajji”. Vilevile, amesema kuwa Mhe. Rais anawatakia watoto wote kusherehekea sikukuu ya Iddi El hajji kwa furaha, amani na kudumisha upendo.

Katibu Tawala Mkoa amelitaja jambo la pili kuwa ni zawadi alizotoa mhe. Rais. “ili muweze kusherehekea vizuri sikukuu hii, Mhe. Rais ametoa zawadi kwenu akiamini mtasherehekea pamoja nae kwa furaha”.

Zawadi alizotoa Rais Kikwete ni mchele kilo 150, mbuzi watatu na mafuta ya chakula lita 40 vyote vikiwa na thamani ya shilingi 555,000.

Akimkaribisha Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Tinna Sekambo amesema Halmashauri yake inavituo vine vinavyotoa huduma ya kulea watoto na kusema kuwa kituo hiki cha Makao ya watoto Tosamaganga ndicho kikubwa na kuushukuru uongozi wa kitaifa kwa kuutambua mchango wa kituo hicho na kuweza kuungana nao katika malezi ya watoto.

Akitoa shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, msimamizi wa kituo hicho Sr Hellen Kihwele amesema “namshukuru sana Rais. Kikwete kwa kutukumbuka mara kwa mara hali inayoonesha upendo wake kwetu sote”.

Sr. Hellen ameyataja matarajio ya baadae ya kituo hicho kuwa ni kukamilisha jingo la shule ya chekechea ambalo halijamalizika kutokana na ukosefu wa fedha na kuiomba jamii iweze kusaidia kukamilisha ujenzi huo.